"Ndugu zangu, kuna tofauti ya mbunge anayetokana na wananchi na Mbunge anayetafuta ubunge kwa ajili ya kuwahudumia wananchi na Mbunge anayekwenda kutumikia chama chake na biashara zake, ndugu zangu hiyo tofauti lazima muielewe. Mimi ninataka kuwa Mbunge wa Kinondoni ili nikasimamie maslahi na maendeleo ya wananchi Kinondoni,anaripoti Mwandishi Diramakini.
Hayo yamebainishwa leo Septemba 27,2020 na Mgombea Ubunge wa Jimbo la Kinondoni jijini Dar es Salaam, Saed Kubenea kupitia Chama cha ACT-Wazalendo.
Amesema, iwapo wana Kinondoni watampa ridhaa atahakikisha wananchi wananufaika kiuchumi kupitia uwezeshwaji ambao unatokana na fedha za Mfuko wa Jimbo.
Kubenea amesema, kupitia fedha hizo atahakikisha zinatumika kuwajengea uwezo juu ya namna ya kutumia fursa zinazowazunguka kujiongezea vipato na kupatiwa mikopo ambayo itawawezesha pia kuimarisha biashara na miradi yao.
Kubenea anasema, suala la ajira kwa vijana ni kipaumbele ambacho atakifanyia kazi haraka kwa kuhakikisha kila fursa inapojitokeza na hata fungu la mfuko huo wanapewa kipaumbele ili waweze kujiajiri, kujitegemea na kuondokana na umaskini. Pia mgombea huyo alitumia nafasi hiyo kuwaombea kura wagombea udiwani, na urais kupitia chama hicho ili wakalifanye Jiji la Dar es Salaam katika viwango bora vya kiuchumi.