Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia UMD,Mazrui Alfphan |
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha The Union for Multiparty Democracy (UMD),Mazrui Alfphan akiwa na Mgombea Mwenza wake, Mashavu Alawi Haji ameyasema hayo baada ya uzinduzi wa Ilani ya chama hicho yenye vipaumbele 29.
Uzinduzi huo umefanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mbagala Rangi Tatu viliyopo wilayani Temeke jijini Dar es Salaam.
Alfphan amesema, endapo watapa ridhaa ya kuchaguliwa na wananchi kuongoza nchi katika Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 28, mwaka huu utekelezaji wa ilani utaanza mara moja.
Mgombea huyo amesema, licha ya kuwepo kwa vipaumbele vingi, UMD imejipanga kurejesha shule za kati pamoja na kuhakikisha mfumo mzima wa elimu unaimarishwa.
Amesema, kuimarishwa kwa mfumo huo kutasaidia wanafunzi wanapomaliza elimu ya msingi wanakuwa wamepokea elimu ya kiwango kitakachosaidia kujiendeleza nje ya madarasa ya kawaida.
Mgombea urais huyo pia amesema, chama hicho kimedhamiria kuleta ajira kwa vijana kwa kuhimiza na kuendeleza vitenga uchumi katika nyanja mbalimbali kupitia sekta rasmi na isiyorasmi.
Pia amesema,chama hicho kitawahusisha vijana katika uandaaji, uendelezaji na utekelezaji wa mipango yote ya serikali na ya watu binafsi.
Mbali na hayo amesema, Chama cha UMD kimedhamiria kuhakikisha kuwa vijana wote wanashiriki kikamilifu katika uongozi wa chama na Serikali kuanzia ngazi za chini hadi katika ngazi za taifa.
Serikali ya chama hicho itatilia mkazo maendeleo ya vijana ambapo Jeshi la Kujenga Taifa litapewa majukumu mapya kwa lengo la kuwa chombo muhimu katika ufufuaji wa uchumi.
Kipaumbele kingine ni pamoja utaifa wa Zanzibar,tawala za majimbo,kazi za majeshi,huduma za walemavu, wanawake na maendeleo, mpango wa uchumi, sheria na haki,mpango wa kisiasa na kijamii,uhuru, Katiba ya Tanzania.Kwa habari mpya endelea hapa.
Ameongeza kuwa, vipaumbele vingine ni misingi muhimu ya Katiba huku Mgombea Mwenza wa kupitia chama hicho, Mashavu Alawi Haji akisema, Serikali yao itakuwa makini katika kuboresha utoaji wa huduma, ukuzaji wa nidhamu na uwekaji wa mazingira bora katika sekta hiyo.
Mashavu amesema, sekta hiyo ni muhimu kwa maisha ya kila binadamu ambapo suala la mafunzo kazini litapewa kipaumbele kwa lengo la kuboresha kima cha utumishi na nidhamu kazini ikiwemo mgawanyo madhubuti wa Serikali za majimbo.