NEC yatoa uamuzi rufaa za wagombea Ubunge 113 na wagombea Udiwani 149

Tume ya Taifa ya Uchaguzi katika kikao chake cha jana tarehe 11 Septemba 2020 imepitia, imechambua na kuzifanyia uamuzi rufaa za wagombea Udiwani zilizowasilishwa na wagombea kupitia kwa wasimamizi mbalimbali wa uchaguzi nchi nzima.
Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Dkt.Wilson Mahera Charles akitoa taarifa ya tume kuhusiana na maamuzi ya rufaa za wagombea udiwani ikiwa ni utaratibu unaofanywa kila siku kadri wanavyokamilisha mchakato huo.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa NEC, Dkt.Wilson Mahera Charles amesema, rufaa hizo zimewasilishwa chini ya kifungu cha 44 (5) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292 ambacho kinatoa fursa kwa wagombea udiwani kukata rufaa wanapokuwa hawajaridhika na uamuzi wa wasimamizi wa uchaguzi kutokana na pingamizi zilizowasilishwa.

Amesema, katika kikao hicho, tume imezipitia, kuchambua na kuzifanyia uamuzi jumla ya rufaa 46 za wagombea Udiwani, kama ifuatavyo:
"Imekubali rufaa 24 na kuwarejesha wagombea katika orodha ya wagombea udiwani. Rufaa hizo ni kutoka kwenye kata za Dunda (Bagamoyo), Mtwivila (Iringa Mjini), Kikilo (Kondoa), Makurumla (Ubungo), Hezya (Vwawa), Makorongoni (Iringa Mjini), Bwawani (Arumeru Magharibi), Jinjimili (Magu), Kimnyaki (Arumeru Magharibi), Lemanyata (Arumeru Magharibi), Mkwawa (Iringa Mjini), Kisarawe II (Kigamboni), Makurumla (Ubungo), Mbabala (Dodoma Mjini), Mpanda Hotel (Mpanda Mjini), Lusungo (Kyela), Same (Same), Maisaka (Babati Mjini), Makuburi (Ubungo), Kibada (Kigamboni), Maore (Same Mjini) na rufaa tatu kutoka Kata ya Mshindo (Iringa Mjini).

"Imekataa rufaa 13 za wagombea ambao hawakuteuliwa. Rufaa hizo ni kutoka kwenye kata za Kawajense (Mpanda), Mjini Chirombola (Ulanga), Mabokweni (Tanga Mjini), Chanika (Karagwe), Mwamala (Manonga), Kiomboi (Iramba Magharibi), Mwasenkwa (Mbeya Mjini), Old Iramba (Iramba Magharibi), Magara (Babati Vijijini), Arri (Babati Vijijini), Chapwa (Tunduma) na rufaa mbili kutoka Kata ya Kibamba (Kibamba).

"Imekataa rufaa tisa za kupinga walioteuliwa. Rufaa hizo ni kutoka kwenye kata za Nonde (Mbeya Mjini), Mwagata (Iringa Mjini), Mabibo (Ubungo), Mkimbizi (Iringa Mjini), Kipanga (Sikonge), Nsoho (Mbeya Mjini), Ilemi (Mbeya Mjini), Bagara (Babati Vijijini) na Nkinga (Manonga). Matokeo ya rufaa zingine soma hapa.

"Idadi hii inafanya jumla ya rufaa za wagombea Ubunge zilizofanyiwa uamuzi na Tume kufikia 113 na za wagombea Udiwani 149. Tume itaendelea kutoa matokeo baada ya usajili na uchambuzi wa rufaa hizo kila siku. Wahusika wa rufaa hizo watajulishwa kwa barua juu ya uamuzi wa Tume.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news