Katibu Mkuu Wizara ya Madini,Profesa Simon Msanjila ameshuhudia biashara ya Madini ya Bati (Tin) ikifanyika ambapo Shirika la Taifa la Uchimbaji Madini (STAMICO) likifanya manunuzi ya kilo 2,271 ya madini ya Bati yenye thamani ya shilingi milioni 34 kutoka kwa wachimbaji wadogo, anaripoti Tito Msellem (WM).
Katika ziara yake hiyo, Prof. Msanjila alitembelea Soko la Madini la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera na kuzungumza na wachimbaji wadogo wadogo pamoja na wafanyabiashara wa madini hayo.
Katibu Mkuu Wizara Madini Prof. Simon Msanjila akisaini Kitabu katika Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa Rashidi Mwaimu.
Aidha, Prof. Msanjila amewataka wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa Madini ya Tin kulitumia Soko la Kyerwa kuuzia madini yao ili wanapotaka mkopo kutoka benki inakuwa rahisi kwa eizara kuthibitisha mauzo yao kwa kuwa yatatambuliwa kwenye mfumo wa eizara.
Pia, Prof. Msanjila amewasihi wachimbaji wadogo na wafanyabishara wa Madini ya Bati kufungamanisha biashara ya madini na chumi zingine kama kilimo, ufugaji n.k. ili kujiongezea wigo wa fursa zitokanazo na Sekta ya Madini.
Katika ziara hiyo yenye lengo la kuhakikisha Soko la Madini ya Bati la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera limeanza kufanya kazi, Prof. Msanjila aliambatana na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwemo Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa,Rashidi Mwaimu.
Vile vile, Prof. Msanjila amewasisitiza wachimbaji wadogo na wafanyabiashara wa Madini ya Bati kuongeza juhudi za uzalisha wa madini hayo kwani soko la uhakika kwa sasa linapatikana na kuwataka kuepuka utoroshaji wa madini hayo
Baadhi ya washiriki walioshiriki mkutano wa Katibu Mkuu Wizara Madini, Prof. Simon Msanjila katika Soko la Madini ya Bati la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera.
Pia, Prof. Msanjila ameipongeza Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kyerwa kwa ushirikiano na uzalendo waliouonesha katika kulinda rasilimali madini kwa manufaa ya nchi.
“Mwaka jana mwezi wa pili Tanzania tulifanikiwa kupata Cheti cha Uhalisia wa Madini ya Bati ambapo Waziri Mkuu Kassim Mjaliwa alikizindua cheti hicho hivyo, tuongeze juhudi kuzalisha madini kwa wingi na kuyaongezea thamani na hatimaye tuyapeleke nje ya nchi tukawauzie,"amesema Prof Msanjila.
Katibu Mkuu Wizara Madini Prof. Simon Msanjila (kulia) akiwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa, Rashidi Mwaimu.
Baadhi ya washiriki walioshiriki mkutano wa Katibu Mkuu Wizara Madini, Prof. Simon Msanjila katika Soko la Madini ya Bati la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera ambapo pia walipewa nafasi ya kuuliza maswali na kujibiwa papo kwa papo.
Baadhi ya washiriki walioshiriki mkutano wa Katibu Mkuu Wizara Madini, Prof. Simon Msanjila katika Soko la Madini ya Bati la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera.
Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa Serikali katika Soko la Madini ya Bati la Wilaya ya Kyerwa mkoani Kagera.
Aidha, Prof. Msanjila amewataka wachimbaji wadogo na wafanyabiashara ya madini ya bati kupendana, kuthaminiana na kuachana na mambo ya majungu ili waongeze tija kwenye shughuli yao ya uchimbaji madini.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kyerwa, Rashidi Mwaimu alimpongeza Katibu Mkuu kwa ziara yake hiyo ambayo imesaidia kuondoa changamoto za Wachimbaji Wadogo na Wafanyabiasha wa Madini ya Bati ambayo yalidumu kwa muda mrefu.