WAKAZI 60,000 BABATI KUPATA MAJISAFI NA SALAMA

Jumla ya wakazi 60,000 wa Mji wa Magugu wilayani Babati mkoani Manyara wanatarajia kunufaika na huduma ya maji pindi mradi wa maji unaotekelezwa kwa kutumia chanzo cha Mto Kou utakapokamilika, anaripoti Mohammed Saif.

Hayo yameelezwa Septemba 27, 2020 wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga wilayani humo ya kukagua hatua ya utekelezaji wa mradi huo na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Babati (BAWASA), Mhandisi Idd Msuya.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (wa pili kushoto) akielekeza jambo wakati wa ziara yake ya kukagua ujenzi wa mradi wa maji wa Magugu Wilayani Babati.

Mara baada ya kupokea taarifa na kujionea hali halisi ya hatua iliyofikiwa ya utekelezwaji wa mradi, Mhandisi Sanga aliielekeza BAWASA kufanya mapitio ya mradi kwenye baadhi ya maeneo ili kuongeza tija.

“Hakikisheni mtandao wa maji unaongezeka ili muweze kuwafikia wananchi wengi zaidi, lakini pia wananchi waweze kunufaika kwa saa 24 kila siku,” alielekeza Mhandisi Sanga.

Aidha, Katibu Mkuu Sanga aliielekeza BAWASA kuhakikisha mradi huo wa Magugu unakamilika kwa wakati na kwamba jitihada zifanyike ili utekelezwaji wake ufanyike bila kusimama.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga akijadiliana jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Babati (BAWASA), Mhandisi Idd Msuya wakati wa ziara yake kwenye mradi wa maji wa Magugu.

“Inatakiwa muongeze watendaji zaidi kwa ajili ya kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi ili ukamilike kwa muda uliopangwa; hakuna sababu ya kuchelewesha mradi,” alielekeza Mhandisi Sanga.

Katibu Mkuu Sanga alitembelea eneo la mradi ambapo alikagua ujenzi wa mitambo ya kuchuja maji pamoja na ujenzi wa chanzo cha maji kwenye Mto Kou.

Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga (kulia) akipitia taarifa ya mradi wa maji wa Magugu wakati wa ziara yake. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa BAWASA, Mhandisi Idd Msuya.

Mradi wa maji katika mji wa Magugu unatekelezwa na Wizara ya Maji kwa gharama ya Shilingi Milioni 575 kupitia Mamlaka ya Maji Babati kwa lengo la kuongeza hali ya upatikanaji wa maji pamoja na kuboresha ubora wa maji yanayotumika kwa sasa.

Mkurugenzi Mtendaji wa BAWASA, Mhandisi Idd Msuya akielekeza jambo wakati wa ziara ya Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi Anthony Sanga kwenye mradi wa maji wa Magugu. 

Kwa mujibu wa Mhandisi Msuya, mradi unatekelezwa na wataalam wa BAWASA na kwamba ulianza kutekelezwa rasmi Agosti,2020 na unatarajiwa kukamilika Desemba,2020.

Katibu Mkuu Sanga amekamilisha ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya maji wilayani Babati.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news