Waziri
wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani akizindua Mradi wa Ujazilizi Umeme
Vijijini Fungu la Pili A katika Kijiji cha Bukene wilayani Nzega mkoani
Tabora amesema kuwa,Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 190.7
kufikisha umeme kitongoji kwa kitongoji katika vitongoji 1,103 vya mikoa tisa, anaripoti Mwandishi Diramakini (Tabora).
“Uzinduzi
huu wa Mradi wa Ujazilizi Fungu la Pili A ni muendelezo wa usambazaji umeme kwa wananchi wote. Kazi hii bado inaendelea, ndani ya miaka miwili
toka sasa, tutakuwa tumevifikia vijijini vyote takribani 12,304 na vitongoji vyake vyote 64,839 nchini,”amesema Dkt.Kalemani.
Waziri
Kalemani amewataka Watanzania ambao hawajafikiwa na
huduma ya umeme kuwa watulivu kwani lengo na mipango ya Serikali ni
kuwafikishia wananchi wote umeme ambao bado hawajafikiwa na huduma hiyo
ndani ya kipindi cha miaka miwili toka sasa.
“Tumepeleka
umeme kijiji kwa kijiji na sasa tunakaribia kumaliza vijiji vyote nchini, sasa tunakwenda kitongoji kwa kitongoji, kaya kwa kaya mpaka
tutakapowafikia wananchi wote,”amesema Waziri.
Kwa
upande wa wananchi wa Bukene, waliohudhuria katika uzinduzi huo
walionesha kufurahishwa na kufarijika sana na mradi huo wa ujazilizi
kuanzia na kuzinduliwa kitaifa katika kijiji na vitongoji vyao vya Kijiji cha Bukene Migombani.
Mwandu
Igusule mkazi wa eneo la Bukene amesema kuwa, wanatarajia kutumia
umeme huo kwa maendeleo yao ya kijamii pamoja na kujikwamua kiuchumi kwa
kuanzisha miradi na shughuli mbalimbali zinazotegemea nishati ya umeme.