Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe.Selemani Jafo, ameipongeza Benki ya DCB kwa kuingiza faida ya shilingi bilioni 2.1 mwaka wa fedha ulioishia mwaka 2019 na hivyo kuweza kutoa gawio kwa wanahisa wake,anaripoti Majid Abdulkarim, Dar es Salaam.
Mhe. Jafo ametoa pongezi hizo kwenye hafla ya utoaji gawio kwa wanahisa wa benki ya biashara ya DCB iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Aidha,Waziri Jafo kwenye hafla hiyo amesema amefurahi kusikia kuwa halmashauri za jiji la Dar es Salaam ambazo ni wanahisa wakubwa wa benki ya DCB zimepata mgao.
Naye Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa benki ya Biashara ya DCB, Bi. Zawadia Nanyaro, amesema kiasi cha shilingi milioni 500 kimetolewa kama gawio kwa wanahisa wa benki hiyo kufuatia idhini ya Benki Kuu na azimio la wanahisa kupitia ushauri wa bodi ya wakurugenzi wa benki.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya biashara ya DCB, Godfrey Ndalahwa amesema benki hiyo imeendelea kupata faida kwa mwaka wa tatu na ndio maana imefanikiwa kutoa gawio kwa wanahisa wake.