Kiwanda kingine cha uchenjuaji dhahabu chazinduliwa Itumbi wilayani Chunya 

Imeelezwa kwamba, katika kuboresha mazingira na shughuli za wachimbaji wadogo wa madini nchini, Serikali ilitenga kiasi cha shilingi Bilioni 4.7 kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vitatu vya uchenjuaji wa madini ya dhahabu ili kuwasaidia wachimbaji hao kupata mafunzo kwa vitendo katika hatua mbalimbali za upatikanaji wa dhahabu,anaripoti Nuru Mwasampeta na Steven Nyamiti (WM).

Mafunzo hayo yatakayokuwa yakitolewa kwa wachimbaji wadogo ni pamoja na elimu ya utafutaji, uchimbaji na uchenjuaji wa dhahabu ili kuwawezesha kufanya uchimbaji wenye tija na kusaidia kuinua vipato vyao na kuongeza mchango wa sekta kwenye pato la taifa.

Hayo yameelezwa leo Oktoba 21, 2020 na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo wakati wa makabidhiano na uzinduzi wa kiwanda hicho kilichogharimu takribani shilingi bilioni 1.7 mpaka kukamilika kwake.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akikata utepe kuashiria uzinduzi wa kiwanda cha kuchenjua dhahabu Itumbi Chunya. Kulia kwake ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila. (WIZARA YA MADINI).

Naibu Waziri Nyongo ametumia fursa hiyo kuishukuru Kampuni ya Tan Discovery Mineral Consultancy kwa kukamilisha ujenzi wa viwanda hivyo na kuvikabidhi vikiwa katika ubora kwa mujibu wa makubaliano.

Aidha, Nyongo amebainisha kuwa, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) lilipewa jukumu la kuhakikisha linasimamia na kuhakikisha ujenzi wa viwanda hivyo vitatu unakamilika kwa wakati na kwa viwango vilivyokusudiwa.

Ameendelea kusema kuwa, kwa sasa STAMICO limeonesha kuwa ni shirika linalojiendesha kwa faida baada ya kuanza kutoa gawio kwa serikali kwa kiasi kisichopungua shilingi bilioni moja mwaka 2019 na bilioni 1.1 mwaka huu 2020.

Pamoja na hayo, Naibu Waziri Nyongo ameitaka STAMICO kuthamini gharama kubwa iliyotumika katika ujenzi wa miradi hii na kuweza kuisimamia ipasavyo ili kuleta matokeo chanya hususani katika kuwawezesha wachimbaji wadogo kuzalisha kwa tija kwa kutumia vifaa vyenye teknolojia rahisi na bora walivyowekewa na serikali yao.

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, akizungumza na wananchi waliofurika kilipo kiwanda cha kuchenjua dhahabu Itumbi mkoani Mbeya alipokwenda kwa ajili ya uzinduzi wa kiwanda hicho leo tarehe 21 Oktoba, 2020. (WIZARA YA MADINI).

Ameendelea kuisisitiza Stamico kuhakikisha wanatoa kipaumbele kwa wakazi wa maeneo jirani na kilipo kituo ili waweze kunufaika na matunda ya kuwepo kwa mradi huu.

Naibu Waziri, Nyongo ametoa wito kwa wachimbaji wadogo wa Itumbi na maeneo jirani kukitumia kituo hicho kujifunza na kupata taarifa mbalimbali kuhusiana na shughuli za utafutaji, uchimbaji, uchenjuaji pamoja na biashara ya madini kwani kituo kimejengwa kwa ajili yao.

Akielezea muda uliotumika katika ujenzi wa miradi hiyo, ikiwa ni pamoja na Lwamgasa, Katente mkoani Geita na Itumbi unaokabidhiwa leo, Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Augustine Ollal amesema, mradi ulianza mnamo mwaka 2016 ambapo mwezi Aprili 2020 viwanda viwili vya Katente na Lwamgasa vilikabidhiwa na uzinduzi wa kiwanda cha Itumbi kinakamilisha mradi wa tatu uliokuwa umesalia.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Prof. Simon Msanjila akizungumza jambo wakati wa hafla ya makabidhiano na uzinduzi wa kiwanda cha mfano cha uchenjuaji wa dhahabu cha Itumbi wilayani Chunya mkoani Mbeya leo tarehe 21 Oktoba, 2020. (WIZARA YA MADINI).

Kwa upande wake Mshauri Mwelekezi na Mjenzi wa kiwanda hicho, Rogers Sezigwa aliishukuru Serikali kwa kutambua uwezo wa kampuni yake inalojishughulisha na utafiti na ujenzi wa mitambo inayotumia teknolojia rahisi kwa wachimbaji wadogo na wa kati ili kuweza kutekeleza ujenzi wa mradi huo pamoja na ile ya Lwamgasa na Katente mkoani Geita.
Mshauri Mwelekezi na mjenzi wa kiwanda cha kuchenjua dhahabu cha Itumbi Chunya, Roggers Sezigwa akielezea moja ya mitambo kiwandani hapo inavyofanya kazi kulia kwake ni Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo na kushoto kwake ni Katibu Mkuu wa Wizara, Prof. Simon Msanjila akifuatiwa na Mwenyekiti wa Tume ya Madini. Prof. Idris Kikula. (WIZARA YA MADINI).

Amesema, wanatumia teknolojia rahisi ili kuwawezesha wachimbaji hao kutumia mitambo hiyo kwa elimu ndogo wanayopewa na wataalamu wake kwa kipindi kifupi.

Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango wa Wizara ya Madini, Augustine Ollal akielezea hatua za ujenzi wa kiwanda cha kuchenjua dhahabu cha Itumbi Chunya mbele ya mgeni rasmi, Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo kabla ya kukata utepe na kufanya ukaguzi katika kiwanda hicho leo tarehe 21 Oktoba, 2020. (WIZARA YA MADINI).

Amebainisha kuwa, mkataba waliopewa uliwataka kubuni na kujenga mtambo wa kuchenjua dhahabu, lakini wakaona ni vema kutumia fursa hiyo kwa kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo katika maeneo ilipo mitambo hiyo ili waweze kufahamu namna ya kuendesha mashine hizo pamoja na elimu nyingine zinazohusiana na uchimbaji, utafutaji na uchenjuaji wa dhahabu watakazokuwa wakipewa.

Aidha, amebainisha kuwa, vijana waliohusika katika ujenzi wa kiwanda hicho na vile vya Katente na Lwamgasa wamewawezesha kwa kuwapa mashimo ya kuchimba ili waweze kujipatia kipato kutokana na uchenjuaji watakaokuwa wakiufanya kiwandani hapo.

Pamoja na kuwapa mashimo hayo, Sezigwa amesema wamewatambulisha vijana hao katika ofisi za wilaya na mkoa ili waweze kuwatumia kutekeleza miradi mingine kwani wameonesha uwezo wa kufanya hivyo.

Aidha, amebainisha hatua ya juu zaidi waliyoichukua ili kuwawezesha vijana hao kwa kuanzisha kampuni inayoitwa Tanzim itakayokuwa ikijishughulisha na uendeshaji wa mitambo hiyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Stamico, Meja Jenerali mstaafu Michael Isamuhyo aliishukuru Serikali kwa namna ilivyoelekeza nguvu zake na fedha katika kuwasaidia vijana na kubainisha kuwa katika kipindi hiki vijana wanatazamwa kwa namna ya pekee katika kuharakisha maendeleo ya jamii.

Mwenyekiti wa Bodi ya Stamico, Meja Jenerali Mstaafu Michael Isamuhyo akitoa salamu za shukrani kwa serikali kwa ujenzi wa viwanda vya kuchenjua dhahabu kwa lengo la kusaidia wachimbaji wadogo, amesema ni uamuzi wa busara katika kuwainua vijana. (WIZARA YA MADINI).

Ametoa kauli hiyo baada ya kubaini kuwa, wananchi wengi wanaojihusisha na shughuli za uchimbaji na uchenjuaji wa dhahabu kuwa ni vijana na hivyo kukiri kuwa ukizungumzia wachimbaji wadogo unazungumzia vijana.

Pamoja na hayo, mstaafu Michael Isamuhyo amebainisha wajibu wa Shirika la Madini la Taifa kuwa ni pamoja na kufanya tafiti katika maeneo mbalimbali na kubaini mashapo yaliyopo na kutenga kwa ajili ya wachimbaji wadogo.


Ameongeza kuwa, katika kutekeleza hilo tayari shirika hilo limefanya tafiti 20 na tatu kati ya hizo zipo mkoani Chunya ambapo ni eneo la Itumbuli, Sangambi na Shoga
.
Jukumu lingine alilolibainisha ni kukuza uelewa wa wachimbaji kwa teknolojia rahisi na isiyokuwa na athari kwa afya na mazingira pamoja na majukumu mengine mengi.

Uzinduzi huo umehudhuriwa na viongozi waandamizi wa Chama na Serikali kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini, Stamico, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Chunya na wengine wengi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news