Mahakama Kuu ya Sumbawanga imewatia hatiani, Michael Kazanda, Linus Luleiman Silukala, Ntongwa Cosmas Sharifu na Frank Bernard Ashenga kwa kosa kujaribu kumuua Maria Chambanenje ambaye ni mlemavu wa ngozi, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Inadaiwa, watuhumiwa hao waliukata mkono wa kushoto wa muathirika (Maria Chambanenje) na kuondoka nao huku wakimwacha akiendelea kuvuja damu.
Tukio hilo lilitokea Februari 11, 2013 katika Kijiji cha Mkowe Wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa, na kutolewa hukumu mbele ya Hakimu Mkeha na washtakiwa wote walitiwa hatiani na kuhukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 10 jela.
Hata hivyo, mwaka 2015 shauri hilo lilisikilizwa na Mahakama Kuu mpaka mwisho na washtakiwa kutiwa hatiani na kuhukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 20 jela, ambapo baadae walikata rufaa na wakaelekeza shauri lianze upya ( Retrial Order) kutokana na mapungufu wakati wa uendeshaji wa kesi hiyo na baada ya kuanza upya washtakiwa wote walikiri kosa na kutiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miaka 20.
Aidha, washtakiwa walikuwa wameshakaa jela kwa miaka saba, ukiongeza na 10 wanayoianza sasa, ikiwa na maana kuwa mwisho watakuwa wametumikia miaka kumi na saba 17 tofauti na ishirini (20) iliyotolewa kwenye adhabu ya awali.
Licha ya mafanikio ya hukumu hiyo, kumekuwepo na baadhi ya changamoto katika shauri hilo, hasa upatikanaji wa mashahidi kiasi kwamba muathirika (Albino) akalazimika kuhama na mpaka sasa hajulikani alipo.
Kesi hiyo iliyoendeshwa na Mawakili wa Serikali Scholastica Lugongo na Simon Peres Oktoba 20,mwaka huu ilitolewa hukumu rasmi.