BAWACHA:Mdee, wenzake 18 acha waondoke

Halima Mdee,Asia Mohamed, Felista Njau, Naghenjwa Kaboyoka, Sophia Mwakagenda, Kunti Majala, Stella Simon, Anatropia Theonest,Salome Makamba, Conchester Lwamraza, Grace Tendega, Ester Matiko,Secilia Pareso,Ester Bulaya, Agnes Kaiza, Nusrat Hanje, Jesca Kishoa, Hawa Mwaifunga na Tunza Malapo si chochote, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Hayo yamesemwa leo Novemba 28, 2020 na viongozi wa Baraza la Wanawake wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAWACHA) kutoka mikoa mbalimbali nchini.
Viongozi hao wamekutana kuzungumza na vyombo vya habari ambapo kwa umoja wao wamelaani vikali kitendo kilichofanywa na wanachama hao 19 wa chama hicho kwenda kula kiapo cha ubunge bila ridhaa ya chama na kupongeza maamuzi yaliyotolewa ya kuwafukuza uanachama.

Makamu Mwenyekiti wa BAWACHA Zanzibar, Sharifa Suleimani amesema kuwa, licha ya kwamba maamuzi yaliyofanywa na wanawake wenzao wakiongozwa na aliyekuwa mwenyekiti wa baraza hilo Halima Mdee, kiliwahuzunisha lakini wao wataendelea kusonga mbele.

"Ninaunga mkono maamuzi ya Kamati Kuu ya kuwavua uanachama, kutoka hivi sasa wanawake wote tunatakiwa turudi majimboni mwetu, kuendelea kufanya kazi za chama, kuondoka kwao siyo lolote si chochote wacha waende,"amesema Sharifa.

Kwa upande wake Mweka Hazina wa baraza hilo, Catherine Ruge amesema kuwa, wanawake wengi waliopo CHADEMA walimuamini sana Halima Mdee, lakini amewaangusha kwa maamuzi yake.

"Wanawake wengi wa CHADEMA tulimuamini Mwenyekiti wetu Halima Mdee, ambaye amefukuzwa uanachama na tulimuona kama mwanamke wa mfano, kiongozi shupavu, jasiri, mwenye msimamo na anayejitambua, lakini Novemba 24, aliamua kuibadilisha historia yake heshima aliyoijenga kupitia CHADEMA kwa zaidi ya miaka 15 imefutika kwa kweli tunasikitika sana,"amesema Ruge.

Novemba 27, 2020, "Kamati Kuu imewavua dada zetu hawa nyadhifa zote za uongozi na mamlaka ndani ya chama, kamati kuu imeona wamepoteza sifa;
    

 Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Freeman Mbowe.

Mbowe aliyasema hayo usiku wa jana wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam ambapo amesisitiza kuwa, chama hicho  hakikuteua wabunge wa viti maalum.

Novemba 24,2020 Mbunge wa Viti Maalum wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA),Bi. Halima Mdee aliwaahidi wanachama wa chama hicho kuwa wanakwenda bungeni kufanya kazi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa.Mdee aliyasema hayo katika viwanja vya Bunge leo muda mfupi baada ya kula kiapo pamoja na wabunge wenzake 18.

Mbunge huyo ambaye awali alikuwa Mbunge wa Kawe na ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la CHADEMA (BAWACHA) aLImshukuru Mheshimiwa Spika, Job Ndugai kwa kusimamia kiapo chao.

"Mheshimiwa Spika nikushukuru kwa kiapo kufanyika na kukamilika, nikishukuru chama changu kupitia wao sisi tumepata nafasi hii ya kukiwakilisha chama chetu. Viti hivi sio hisani ni sehemu ndogo ya ushindi mkubwa ambao chama chetu kilipata.

"Nikuhakikishie Mheshimiwa Spika tutafanya kazi kwa uaminifu kama kambi rasmi ya upinzani bungeni na kwa uadilifu mkubwa kwa viwango vilevile tulivyokuwa tunavifanya. Kuna vijana wapya sisi kama dada zao tunakuhakikishia watafanya kazi bora. Niwahakikishie wana CHADEMA tutafanya kazi mliyotutuma kwa uaminifu na uadilifu mkubwa sana,"amesema.
 
Freeman Mbowe ameongeza kuwa, Kamati Kuu ya chama hicho iliyoketi leo Novemba 27,2020 imeazimia kuwavua uanachama wanachama na viongozi hao.
 
"Wamekinajisi chama na wamekataa kuja kwenye Kamati Kuu. Chama chetu hakijateua wabunge wa Viti Maalum tunaona tu watu wetu wanaapishwa na hatuna taarifa, hatujapeleka majina, fomu za tume zipo ofisini, mama zetu hawa, dada zetu hawajajaza fomu, ila tunaona tu wanaapishwa. Kamati Kuu imewavua uongozi wale wote ambao walikuwa viongozi kwenye mabaraza kati ya hao dada zetu 19 sitaki kupoteza muda kuwataja majina, kwa hiyo kuanzia sasa hawapaswi kushughulika na lolote kama viongozi na tumeelekeza nafasi zao zizibwe haraka,"amefafanua Freeman Mbowe.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news