Wafanyakazi NCC waelimishwa kuhusu Ukimwi

Wakati Dunia leo Desemba 1, 2020 ikiadhimisha Siku ya Mapambano dhidi ya Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi, Baraza la Taifa la Ujenzi (NCC) limesema limefikia malengo yake ya kuhakikisha wafanyakazi wanaelimishwa kuhusu Ukimwi na maambukizi ya virusi visababishavyo ugonjwa huo kwa mwaka huu, anaripoti Mwandishi Diramakini.

Aidha, limesema litahakisha zana muhimu zinazohitajiwa na wafanyakazi kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya VVU na Ukimwi (kondomu) zinaendelea kupatikana kwa urahisi katika maeneo yote ambako zinapaswa kuwepo ndani ya ofisi hiyo, kwa ajili ya wahusika kuchukua na kwenda kuzitumia pindi wanapokuwa wakizihitaji.

Mtendaji Mkuu wa Baraza hilo, Dkt. Matiko Mturi amesema hayo jijini Dar es Salaam huku akifafanua kuwa, mpango wa kulinda wafanyakazi wake dhidi ya maambukizi ya magonjwa hasa Ukimwi ni endelevu na kwamba unatekelezwa kupitia mafunzo, ushauri nasaha na njia nyingine zinazotumika kufikisha ujumbe kwa wafanyakazi kuhusu namna bora ya kujikinga, kama vile semina na maandiko mbalimbali vikiwemo vipeperushi na ajenda maalumu kwenye vikao vyote vya wafanyakazi.

“Tunashukuru kwamba wafanyakazi wa NCC wamekuwa wakitoa ushirikiano wa hali ya juu kufanikisha utekelezaji wa mpango mkakati wetu wa kuwapa elimu kuhusu masuala ya afya hususan namna ya kujikinga na maambukizi ya VVU pamoja na mambo yote wanayopaswa kuyajua kuhusu Ukimwi,”alisema.

Kutokana na maelezo ya Dkt.Mturi, NCC ilifanikiwa kupima kwa hiyari wafanyakazi wake, baada ya kuwaandaa kisaikolojia na kufanikiwa kuwapa elimu iliyohitaji sit u kuhusu Ukimwi bali hata magonjwa mengine ambayo walipaswa kupata elimu kuyahusu.

Alisema lengo la kuweka mpango mkakati huo, pamoja na kutimizwa kwa matakwa ya Serikali ya kuhakikisha vita dhidi ya maambukizi ya VVU na Ukimwi vinapiganwa hata katika maeneo ya kazi kwa wafanyakazi kupewa elimu ya kujikinga na maradhi, ni kuhakikisha usalama wa afya za wafanyakazi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

“NCC inajali na kuthamini afya ya wafanyakazi wake, kwa sababu ndio watenda kazi wanaotegemewa katika uzalishaji wa kila siku, hivyo kutokuwa na afya njema kwao ni tatizo pia kwa mlolongo mzima wa utendaji katika baraza,”amesema.

“…Tunaendelea na tutaendelea kuhakikisha elimu zaidi inatolewa kwa wafanyakazi wote ili wajue namna bora ya kujilinda na kulinda wanajamii wengine wanaowazunguka dhidi ya magonjwa kama vile Ukimwi na mengine yanayoambukiza.,”

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news