Wakazi wa Jiji la Dodoma wamekumbushwa kutekeleza wajibu wao wa kufanya usafi ili kulifanya Jiji la Dodoma kuwa safi na la kuvutia muda wote,anaripoti Mwandishi Diramakini.
Mkuu wa Idara ya Mazingira na Usafi wa Taka ngumu wa Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro ameyasema hayo alipokuwa akiongea na wananchi waliojitokeza kufanya usafi siku ya Jumamosi katika Kata ya Kiwanja cha Ndege jijini hapa.
Aidha. wito umetolewa kwa watendaji wa kata na mitaa kuhakikisha wanasimamia maelekezo hayo kikamilifu.
Pia amesema, wananchi wanatakiwa kufanya usafi katika makazi na biashara zao mita tano kuzunguka maeneo yao na kujiepusha na utupaji holela wa taka kwenye maeneo yasiyoruhusiwa.
"Usafi wa mazingira yetu utatuwezesha kuwa salama kiafya na kupunguza uwezekano wa kutokea magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu, kuhara na kadhalika,"amesema.
Vilevile, Kimaro amewahimizwa wakazi wa Jiji la Dodoma kupanda miti ya matunda na ile yenye kuleta kivuli katika msimu huu wa mvua.
“Faida ya miti sote tunaifahamu, miti hutusaidia kupata matunda na kivuli kwa ajili ya mapumziko, lakini pia tukipanda miti itasaidia kupunguza hali ya joto hasa wakati wa kiangazi, pia hupunguza kasi ya upepo uvumao na miti huongeza thamani ya maeneo tunayoishi,"amesema.
Picha na matukio wakati wa usafi kata ya Kiwanja cha Ndege leo.