Rais Dkt.Mwinyi azungumza na wafanyabiashara

Wafanyabiashara na wadau mbalimbali kutoka sekta binafsi nchini wameiomba Serikali kuongeza ushirikiano na sekta hizo kwa msingi kuwa zina mchango mkubwa katika uimarishaji wa uchumi wa Zanzibar, anaripoti Mwandishi Diramakini.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi (kulia) akitoa hotuba yake kwa wafanyabiashara wa Zanzibar katika mkutano wao uliofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idriss Abdul Wakil Kikwajuni jijini Zanzibar ili kujua kero mbalimbali zinazowakabili katika uendeshaji wa biashara zao nchini.
 
Hayo yameelezwa leo Desemba 5, 2020 na wafanyabiashara kutoka sekta mbalimbali nchini katika salamu zao walipozungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Ali Mwinyi, katika mkutano uliofanyika kwenye Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil, Kikwajuni jijini Zanzibar.

Viongozi walioshiriki katika mkutano huo ni pamoja na sekta ya Kilimo na Ufugaji, Viwanda, TEHAMA, Usafirishaji, ZATO, ZATI Ujenzi, sekta ya Fedha, Usafiri, sekta ya Wanawake, Mafuta pamoja na Mafuta ya Ndege.

Wamesema, kuna umuhimu wa Serikali kuongeza mashirikiano na kufanya juhudi ili kuhakikisha taasisi hizo zinaondokana na changamoto mbali mbali zinazokabili,huku zikibainisha kuwa kuimarika kwake kutachochea ukuaji wa uchumi.

Mkurugenzi Mtendaji kutoka MD-QBC, Khamis Ali Said amesema, miongoni mwa changamoto zinazoikabili sekta hiyo ni hali iliyopo hivi sasa ambapo hakuna utaratibu wa kurudishiana kodi ya ongezeko la thamani (VAT) kati ya Zanzibar na Tanzania Bara.

Amesema, kuna umuhimu kwa serikali zote mbili kukaa pamoja na kulipatia ufumbuzi wa kudumu suala hilo kwa msingi kuwa lina athari kubwa kwa wafanyabiashara wa Zanzibar.

Amesema upatikanaji wa rasilimali ya mchanga kwa ajili ya ujenzi, hususan katika miradi mikubwa nao hauko sawa kiasi ambacho huwalazimu wakanadarasi kusitisha shughuli za ujenzi baadhi ya nyakati kutokana na ukosefu wa rasilimali hiyo.

Amesema Serikali ina wajibu wa kuhakikisha mchanga unaopatikana nchini unafaa kwa matumizi sahihi ya miradi inayoendelezwa.

Ameiomba Serikali kufuatilia na kuhakikisha sheria ya manunuzi iliopo inatekelezwa na watendaji wake pamoja na kufuata kikamilifu vifungu vilivyoainishwa, sambamba na kuwataka watendaji hao kuacha utamaduni wa kutoa visingizio kuwa baadhi ya vifungu havijawekewa kanuni.

Aidha, ameiomba Serikali kuondoa mazingira yanayowanyima fursa wakandarasi wazalendo kutekeleza miradi mikubwa inayotangazwa , pamoja na kutaka kufanyike marekebisho ya viwango vya chini vya miradi vya shilingi bilioni mbili.

Nae, Meneja wa Benki ya Afrikam Juma Burhan amesema sekta ya fedha inakabiliwa na changamoto nyingi, ikiwemo ya kutokuwepo sera na sheria za usajili wa mali zinazohamishika.

Ameeleza kuwa, mbali na Benki ya Tanzania (BoT) kutoa katazo la kutokuwepo sehemu ‘bubu’ za kubadilishia fedha za kigeni nchini, lakini maeneo hayo yameendelea kuwepo na hivyo kuhusika katika biashara haramu.

Amesema kuna, umuhimu kwa serikali kujenga ushirikiano na benki binafsi ili ziweze kutoa mikopo na kuchochea uimarishaji w auchumi, wakati huu ambapo serikali haijazipa kipaumbele benki za ndani.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi akifuatana na Waziri wa Kazi,Uchumi na Uwekezaji, Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga wakati alipowasili katika ukumbi wa Sheikh Idriss AbdulWakil Kikwajuni jijini Zanzibar katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo.
Baadhi ya Wafanyabishara wa Makampuni mbalimbali wakisikiliza mada zilizotolewa katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni jijini Zanzibar chini Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi akitoa hotuba yake katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idriss AbdulWakil Kikwajuni jijini Zanzibar.
Baadhi ya Wafanyabishara wa Makampuni mbalimbali Zanzibar wakiwa katika Mkutano wa pamoja na taasisi mbali mbali za Serikali uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni Jijini Zanzibar chini Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi (katikati) akiwa katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni jijini Zanzibar kushoto ni Makamu wa Pili wa Rais, Mhe.Hemed Suleiman Abdulla na Waziri wa Kazi,Uchumi na Uwekezaji, Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi (katikati) akiongoza mazungumzo ya pamoja na Wafanyabishara wa Zanzibar yaliyofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idriss AbdulWakil Kikwajuni Jijini Zanzibar wakiwepo Waziri wa Kazi,Uchumi na Uwekezaji Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga (watatu kulia) Makamu wa Pili wa Rais Mhe.Hemed Suleiman Abdulla (wa tatu kushoto) pamoja na viongozi wengine.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Mwinyi akitoa hotuba yake katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idriss AbdulWakil Kikwajuni jijini Zanzibar (kutoka kushoto) Waziri wa Kazi,Uchumi na Uwekezaji Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga,Kaimu Mwenyekiti wa ZNCC,Ali Amour na Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi, Mhe.Idrissa Kitwana Mustafa.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi akitoa hotuba yake katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idriss AbdulWakil Kikwajuni Jijini Zanzibar (kutoka kushoto) Waziri wa Kazi,Uchumi na Uwekezaji Mhe. Mudrik Ramadhan Soraga,Kaimu Mwenyekiti wa ZNCC Nd.Ali Amour na Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Mhe.Idrissa Kitwana Mustafa.
Baadhi ya Wafanyabishara wa Makampuni mbalimbali wakisikiliza mada zilizotolewa katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni Jijini Zanzibar chini Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani).
Wafanyakazi wa taasisi mbalimbali za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar wakiwa katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni Jijini Zanzibar chini Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani).
Wafanyakazi wa taasisi mbalimbali za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar wakiwa katika Mkutano na Wafanyabiashara wa Zanzibar uliofanyika leo katika Ukumbi Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni Jijini Zanzibar chini Mwenyekiti wake Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani).
 
Nae Mkurugenzi wa Rahisi Solutions, Abdulrahman Hassan amesema, kuna changamoto mbalimbali zinazoikabili Zanzibar katika sekta ya TEHAMA ambazo zinaweza kutatuliwa na Wanzanibari wenyewe kwa kuwepo mashirikiano na serikali.

Amesema, kinachohitajika ni kuwajengea uwezo vijana kwa kuamini kuwa Wazanzibari wanaweza kwa vile wana ujuzi na uzoefu.

Aidha, Mwenyekiti wa UWAMWIMA, Salum Rehani amesema Zanzibar imefanikiwa kuzalisha asilimia 50 ya mahitaji ya bidhaa za mboga mboga na matunda na kuuza katika soko la utalii.

Amesema pamoja na mafanikio hayo ya uzalishaji wa bidhaa zilizo bora na salama, bado wakulima wanakabiliwa na changamoto kubwa ya soko la la kuuzia bidhaa hizo, kwani hivi sasa hupata fursa hiyo kwa asilimia 12 pekee, kwa vile wamiliki wa hoteli huagiza bidhaa za aina hiyo kutoka Tanzania Bara.

Amesema, bado taasisi za fedha hazijafanya vyema katika kuwawezesha na kuwawekea mazingira mazuri wakulima hao ili kupata mikopo na kuongeza uzalishaji.

Vile vile, amesema soko la maziwa yanayozalishwa Zanzibar bado limekuwa la mashaka, na kubainisha kuwa wafugaji huuza maziwa yao katika Kiwanda cha Bakharesa kiliopo Mtoni, wakati ambapo zaidi ya lita 8,000 ya bidhaa hiyo hukosa soko.

Rehani amesema, sekta ya Uvuvi wa Bahari Kuu ni eneo muhimu na mhili wa uchumi wa Zanzibar kuliko eneo jengine lolote lile, akibainisha uwepo wa fursa za kutosha za ajira, na hivyo akaiomba Serikali kuwekeza nguvu zake katika kufanya tafiti na kuweka mikakati ili kufanikisha azma ya Serikali ya kuwapatia vijara vijana.

Akigusia sekta ya usafiri wa anga, Mwenyekiti wa ZAT Mohamed Raza ameiomba serikali kuongeza juhudi kukamilisha matengenezo ya ‘terminal 3’ ili kuondokana na changamoto mbali mbali za usafiri kwa wageni.

Amesisitiza umuhimu wa wafanyabiashara kulipa kodi kwa kigezo kuwa ndio inayoongoza nchi na kusadia upatikanaji wa huudma mbali mbali za kijamii, ikiwemo Afya.

Nae, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watembeza Watalii Zanzibar (ZATO), Hassan Ali Mzee ameomba kuwepo ushirikiano wa pekee kati ya jumuiya hiyo na Serikali akibainisha utayari wa ZATO katika kukabiliana na changamoto mbalimbali inayokabili sekta hiyo.

Amesema, ZATO ina jukumu kubwa katika uimarishaji wa sekta ya Utalii nchini kwa kuingiza watalii wengi zaidi, ikizingatiwa utajiri mkubwa wa vivutio vya utalii viliopo nchini.

Aidha, Mwenyekiti wa ZATI Seif Mirskry alisema ugonjwa wa Covid-19 ulioikumba Dunia umeathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya utalii, hivyo akaishauri Serikali kuwa sio wakati muafaka wa kufikiria kuongeza viwango vya kodi na kusema huu ni wakati wa wafanyabiashara kupata tahfif.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara Wanawake Fatma Khamis, alitaka kuwepo ushirikishwaji na uwezeshaji kwa wafanyabiashara hao ili kuboresha biashara zao na hatimae kuinuwa uchumi wao .

Amesema, wajasiriamali wanawake wana changamoto mbali mbali ikiwemo ya upungufu wa elimu za biashara.

Aidha, Mkurugenzi wa Purma Enery inayotoa huduma ya Mafuta ya Ndege, Rehema Migambile amemhakikishia Rais Dkt. Mwinyi kuwa kampuni hiyo itaendelea kuwa kinara katika upatikanaji wa nishati hiyo ikilenga kuhakikisha safari za ndege zinafanyika bila vikwazo.

Rais Dkt.Mwinyi

Katika hatua nyingine, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa Serikali anayoiongoza itatoa msukumo mpya katika kutatua changamoto zinazokabili biashara hapa Zanzibar.

Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika mazungumzo kati yake na wafanyabiashara wa Zanzibar, hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil, Kikwajuni Jijini Zanzibar.

Katika hotuba yake Rais Dkt. Hussein Mwinyi amesema kuwa anataka kuweka ushirikiano na sekta binafsi pamoja na kuongeza na kuwepo mijadala ya wazi na yenye tija kwa lengo la kuweka mazingira mazuri kwa wafanyabiashara.

Rais Dkt. Hussein amesema kuwa, Serikali haifanyi biashara bali kazi yake ni kutengeneza Sera nzuri, sheria, kanuni, na kuweka mifumo ya udhibiti wa biashara lakini uchumi utaendeshwa na sekta binafsi.

Ameongeza kuwa, Serikali itaweka mfumo rafiki, kuondoa urasimu, rushwa na vikwazo vyote vinavyotakana na utendaji mbovu.

Rais Dkt. Hussein ameeleza maono yake ni kuifanya Zanzibar kuwa ni kituo cha biashara katika Afrika Mashariki hasa kutokana na mazingira yake kijiografia kwani Zanzibar inaweza ikawa kituo cha biashara, utalii, viwanda, bandari huru hiyo ni kutokana na jinsi ilivyo.

Rais Dk. Hussein amerejea kauli yake ya kuwataka viongozi wa wizara kutengeneza mipango yenye bajeti huku akisema kuwa kila sekta ina utaratibu wake na kwa upande wa ujenzi wa barabara Serikali itafanya na kuchukua jukumu lake hilo la kujenga barabara na sio sekta binafsi.

Amesema kuwa, madhumuni ya mkutano huo ni kutimiza ahadi yake aliyoahidi wakati wa Kampeni ya kukutana na wafanyabiashara na kutaka kujua changamoto zao na kuahidi pale atakapaingia madarakani watakaa pamoja huku akieleza kwamba changamoto zote amezisikia na zitafanyiwa kazi hasa ikizingatiwa viongozi wa Serikali walikuwepo katika mazungumzo hayon wakiwemo Mawaziri na Makatibu Wakuu.

Katika maelezo yake amesema kwamba, zipo tabia ya kufanya mikutano mingi bila ya ufumbuzi ambapo katika utawala wake tabia hiyo hatoitaka na kusisitiza kwamba kuchukuliwa changamoto na kutofanyiwa kazi ni kupoteza muda hivyo ni lazima mikutano iwe na tija.

Hivyo, amewaeleza watendaji wote Serikalini kwamba ana miadi na wananchi katika miaka mitano hivyo ni lazima kufanya kazi kwa haraka ili kutatua changamoto zilizopo na kama zikitokezea kuwashinda apalekewe.

Amesema kuwa kwa upande wa bandari, katika mradi huo kuna uwezekano mkubwa wa kushirikiana na sekta binafsi.

Aidha, alieleza uwezekano wa kuwa na bandari hapa Zanzibar itakayotoa huduma za utalii, bandari za uvuvi na bandari za mafuta na bandari za kila kitu kwa ajili ya kuchukua meli kubwa ambapo kwa upande wa meli ndogo zinaweza kufanya kazi za kusambaza katika maeneo mengine kutoka Zanzibar.

Amewaahaidi kwamba Serikali iko tayari kushirikiana na sekta binafsi ili kuweza kuyatimiza hayo kwa mustakbali wa Zanzibar.

Amesema kuwa kwa pamoja inawezekana kufanyika hayo kwani uwezo upo, mtaji na upo , uzoefu upo, masoko na utayari wa Serikali upo na rasilimali ipo na kwa vile Zanzibar inajitangaza vyema nje ya nchi hatua hiyo itasaidia.

Amesema kuwa, mabenki kadhaa hapa nchini yameonesha nia ya kushirikana na Serikali katika kuijenga Zanzibar kwa masharti nafuu hivyo, uwezo wa kifedha upo na hayo yanawezekana na yanatekelezeka katika azma ile ile ya kuijenga Zanzibar kiuchumi.

Alirejea kutoa ahadi yake kwa wafanyabiashara ya kuondosha changamoto zote zinazokwamisha biashara hapa Zanzibar.

Akieleza changamoto ya kodi alisema kuwa yeye si muumini wa kodi kubwa kwani wapo watu wanaodhani kwamba kodi kubwa ndio pato kubwa kwa Serikali lakinhi ni kinyume chake na badala yake kodi kubwa ndio inayopunguza wafanyabiashara.

Aliongeza kwamba watakaofanya biashara kwa kodi kubwa ni wachache lakini ikipunguzwa kodi watakaofanya biashara ni wengi, lakini serikali haiishi kwa kodi pekee bali mzunguko wa biashara ndio unaoongeza fedha na kukuza uchumi.

Kwa upande wa suala la udhitibi, alisema kuwa kuna mamlaka za udhibiti zipo nyingi ambazo zote zinataka kutoza bidhaa moja bila ya kutokuwepo sababu na kutolea mfano wa badari ya Malindi, Zanzibar ambapo mamlaka zinazotoza kodi zipo karibu nne.

Alisema kuwa wakati umefika wa kuziunganisha baadhi ya mamlaka ili kuweza kupata ufanisi jambo ambalo linawezekana na litafanyika kwani Zanzibar ni ndogo na haiitaji kuwepo mamlaka nyingi.

Alieleza matatizo ya miundombinu ya usafiri ikiwemo bandari, ambapo hivi sasa watu wameigeuza bandari ni sehemu ya kuweka makontena yao.

Anataka kuweka utamaduni wa kufanyakazi kwa pamoja kati ya sekta binafsi na sekta ya umma katika serikali na kusisistiza kwamba sekta binafsi inaweza kushirikiana na serikali katika masuala mengi lakini wanaohitajika ni wale ambao wanaelewa.

Alisisistiza kuwa watu watakaoendesha mashirikia ya baishara ni lazia wawe wanajua biashara na haiwezekani kuona mtu anaongoza shrika halafu anapata hasara na kueleza tataizo la badanri na uwanja wa ndege yatakwisha.

Aliongeza kuwa hakuna Mamlaka ya Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) itakuwa onestope center kwa kujumuisha masuala yote muhimu kwa muwekezaji na wahusika wote ni lazima wawepo ZIPA ili kikitoka kibali kitoke kwa pamoja.

Alisema kuwa utaondoshwa urasimu, rushwa, watu kutowajibika katika taasisi hiyo na kueleza sababu ya kuiweka Wizara husika inayoshughulikia uwekezaji kuwa chini yake iili iwe chini ya macho yake na hilo ni kwa kila Wizara.

Aliwataka kila kiongozi ayachukue yale yaliyozungumzwa na wafanyabiashara ili wakikutana tena wazungumzie mafanikio na sio changamoto.

Kwa upande wa ajira alisisitiza haja ya kuekekeza katika kupata ajira 300,000, alizoziahidi wakati wa Kampeni kwa mashirikiano na sekta binafsi na kusisitiza haja ya kupatikana ajira zaidi ya hizo iwapo sekta ya viwanda itaimarishwa.

Alisema kuwa changamoto za watu kuekeza kwenye sekta ya viwanda zitaondoshwa na kusisistiza kwamba Serikali inataka kuekeza viwanda vyenye kuajiri watu wengi kwani viwanda vingi vinaweza kupatikana hapa Zanzibar ilimradi tu mazingira yawe mazuri huku akieleza haja ya kuvilinda viwanda vya ndani kwa lengo ni kumnufaisha Mzanzibari.

Rais Dk. Hussein alisema kuwa lazima kuwepo sera za kuwasaidia watu wa ndani na kutaka kuewa upendeleo kwa wazawa kwani hivyo ndivyo nchi nyengine zinazoyajenga makampuni yao.

Aliwasisitiza wafanyabiashara kulipa kodi huku akisema kuwa kodi maalum zimewekwa Zanzibar ili kuwasaidia Wazanzibari kupata unafuu katika bidhaa zao licha ya kuwa bado wananchi wa kawaida hawanufaiki.

Alisema kuwa wapo wafanyabiashara ambao hawalipi kodi “sina nia ya kufufua makaburi na kumtafuta mchawi lakini nataka kusema kuanzia sasa kila mtu alipe kodi”, alisema Dk. Hussein.

Alisema kuanzia sasa kwenda mbele kila mtu alipe kodi ikiwa ni pamoja na kulipa kodi inayolipwa kutoka kwa wafanyakazi kutoka nje, na kusisitiza kwamba kodi ndogo zilipwe na kutaka kulipwa jinsi inavyotakiwa kulipwa na kutaka kuwekwa mifumo mizuri ya kodi.

Alisema kuwa hapo zamani watu walikuwa wanakuja kununua bidhaa Zanzibar kwa sababu kodi ilikuwa ndogo na bei afadhali lakini hivi sasa wengi wao wanaelekea Kariakoo Dar-es-Salaam kwa sababu bei ya mwisho haimsaidii mwananchi.

Rais Dk. Hussein alisema kuwa ni vyema mfanyabiashara akapata faida, Serikali ikapata na mwananchi nae apate na isiwe upande mmoja tu wa wafanyabiashara pekee yao wakapata.

Alisema kuwa bado utamaduni wa kufanya kazi kwa mazoea utachukua muda lakini jitihada zitafanyika katika kuuondoa haraka na kusema kuwa hatowaachia Mawaziri pekee yao na kuahidi kuunda Kitengo kitakachokuwa chini ya Ofisi yake kitakachokuwa na kazi ya Ufuatiliaji wa Utekelezaji wa Miradi katika sekta mbali mbali “President’s Delivery Bureau” (PDB).

Alieleza kuwa kazi ya taasisi hiyo itakuwa ni kuuangalia uchumi wa Zanzibar unakwenda vile anavyotaka, itakuwa na wataalamu wa uchumi, wa fedha na maeneo mengine mbali mbali ambacho kitasaidia pia, kuwasukuma Mawaziri katika kutekeleza majukumu yao ambapo pia, wataalamu wa taasisi hiyo watakuwa wafuatiliaji wa maazimio yote yanayoazimiwa kufanywa.

Alisema kuwa miradi ya Serikali iko mingi na wote wanaweza kunufaika na kuwataka kuwa wawe tayari kushirikiana na kuwahakikishia wafanyabiashara hao kwua maoni yote waliyoyatoa yatafanyiwa kazi na kuwataka kwenda kukaa na Mawaziri ili kuyatekeleza yote hayo.

Sambamba na hayo, aliahidi kukutana na wafanyabiashara wa kila sekta, huku akisema kwua mazingira ya kufanya biashara Zanzibar yatakaa sawa na kusisitiza kwamba Mawaziri wote watafanya kazi na wafanyabiashara hao kwa karibu.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news