Rais wa Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron amemwandikia barua ya pongezi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuiwezesha Tanzania kuingia katika hadhi ya nchi ya uchumi wa kati ikiwa ni miaka mitano kabla ya muda uliotarajiwa, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Katika barua hiyo Rais wa Ufaransa, Mheshimiwa Emmanuel Macron amempongeza Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kuishi katika dhamira na mawazo ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kuiona Tanzania inayoendelea kisiasa, kiuchumi na iliyo huru.
Rais Macron ameongeza kuwa, ana imani kuwa katika muhula mpya wa miaka mitano ya kipindi cha pili cha Serikali inayoongozwa na Rais John Pombe Joseph Magufuli utaiwezesha Tanzania kufikia malengo yake katika nyanja ya kiuchumi inayotilia mkazo maendeleo ya wananchi, lakini pia inayounganisha demokrasia ya vyama vingi.
Pia amemhakikishia Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kuwa, Ufaransa itaendelea kushirikiana na Tanzania katika hatua ya kuendelea kukua kiuchumi na kimaendeleo.
Tags
Kimataifa