Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhandisi Joseph Nyamhanga ametoa siku saba kwa uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro kuhakikisha inakamilisha ujenzi na kuanza kazi kwa soko la kisasa la Morogoro,anariooti Angela Msimbira, MOROGORO.
Akikagua maendeleo ya ujenzi wa soko hilo leo Desemba 7,2020 mkoani Morogoro, Mhandisi Nyamhanga amesema kuwa kuna masoko 22 yamejengwa na Serikali ambayo yamegharimu zaidi ya shilingi bilioni 120 ambapo kwa soko la Morogoro limegharimu shilingi bilioni 17.6.
Mhandisi Nyamhanga ameeleza kuwa, umuhimu wa masoko hayo ni kuboresha miundombinu kwa wafanyabiasha ili waweze kufanyabiashara zao katika mazingira mazuri na yaliyoboreshwa na kuwapunguzia adha ya kukaa kando ya barabara na kufanyabiashara katika mazingira mazuri.
“Maeneo mengi wafanyabiashara walikuwa wanafanyia biashara zao barabarani, kwenye mavumbi na matope, lakini kwa sasa soko la Morogoro kuna vizimba 900 ambavyo vitawasaidia wafanyabiashara kufanya shughuli zao katika mazingira bora,” amesisitiza Mhandisi Nyamhanga.
Ameagiza kukamilika kwa kazi ndogondogo zilizobaki na ifikapo Disemba , 15 mwaka huu soko hilo lianze kazi ili wananchi wapate huduma katika manzingira yaliyoboreshwa.
Aidha, kumalizika kwa ujenzi wa soko hilo itasaidia kuongeza ajira kwa wananchi ambapo ajira 2500 ikiwemo wale wenye ajira rasmi na wasiorasmi hii itasaidia kupunguza umaskini na kuongeza kipato kwa wananchi.
Naye Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro, Bi. Sheilla Lukuba amesema ujenzi ukikamilika soko litakuwa na maeneo ya biashara ya maduka 304, meza, 900, maeneo makubwa 16 ya kupangisha kwa mita za mraba kwa biashara kama mabenki, maduka makubwa, ofisi, migahawa, stoo 3 , vioski 34 vya mitumba na mabucha 3.
Amesema kuwa matarajio ya makusanyo ya biashara zitakazofanyika baada ya soko kukamilika shilingi bilioni 2 kwa mwaka ambapo itaipunguzia Halmashauri hiyo kutegemea ruzuku kutoka Serikali kuu.
Pia ameongeza kuwa mapato yatakayokusanywa yatasaidia kutoa huduma bora za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.