Ukiwa na dalili hizi chukua hatua kupima Ukimwi

Leo Desemba Mosi ni Siku ya Ukimwi Duniani ambapo Kitaifa maadhimisho yamefanyika katika uwanja wa Mandela Moshi mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa kimataifa, Tujumuike Pamoja", anaripoti Mwandishi Diramakini.

Kwa mujibu wa uanishaji uliofanywa na wataalamu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kuna hatua kuu nne za ugonjwa wa Virusi Vya Ukimwi (VVU) ambazo ni;

Mosi, hatua ya kwanza au maambukizi ya mwanzo ya HIV. Kwa mujibu wa wataalam hao,hatua hii huwa ni ya muda wa wiki nne na ni asilimia 20 tu ya watu wenye maambukizi ya VVU walio kwenye hatua hii.

Watu hao hupata dalili na viashiria vikali vya ugonjwa huu, lakini mara nyingi madaktari hushindwa kutambua kama mgonjwa amepata maambukizi ya virusi vya ukimwi kutokana na dalili na viashiria vyake kufanana sana na dalili za magonjwa mengine.

Mgonjwa aliye katika hatua hii ya kwanza ya maambukizi ya VVU huweza kuonesha dalili na viashiria kama vile kuvimba tezi, kupatwa na homa kali, kuumwa koo, kujihisi mchovu, kujihisi maumivu sehemu mbalimbali mwilini kutokwa na vipele mwilini,kutapika, kuharisha au kuumwa tumbo. 

Mgonjwa anayepata dalili na viashiria hivi tunasema kwamba amepata "Acute HIV infection/Acute HIV retroviral infection au seroconversion illness." 

Dalili hizi hutokana na mwili wa mtu mwenye maambukizi ya VVU kuanza kutengeneza kinga dhidi ya VVU.

Hatua ya pili ni isiyokuwa na dalili au Clinically Asymptomatic Stage.

Katika hatua hii ambayo inaweza kudumu kwa muda wa miaka 10, mgonjwa haoneshi dalili au viashiria vyovyote vile isipokuwa anaweza kuwa na tezi zilizovimba. 

Kiwango cha VVU kwenye damu hupungua sana, lakini mgonjwa anaweza kuambukiza mtu mwingine yeyote na vipimo vya Ukimwi vina uwezo wa kutambua uwepo wa maambukizi ya VVU katika damu. 

Tafiti mbalimbali zimeonesha kwamba, VVU katika mwili huwa bado vinazaliana na hukimbilia na hujificha kwenye tezi. 

Kutokana na kujificha kwake katika hatua hii, kipimo cha kupima wingi wa virusi vya ukimwi au Viral load test katika mwili hutumiwa sana ili kuweza kutambua uwepo wa VVU. Kipimo hiki pia husaidia katika kumpangia mgonjwa tiba yake.

Hatua ya Tatu yenye viashiria au Symptomatic HIV infection. Katika hatua hii kutokana na kuongezeka kwa wingi VVU katika mwili, kinga ya mwili huzidi kudhoofika suala linalosababisha mambo kadhaa. 

Kwanza ni tezi na tishu zilizoathiriwa na VVU huharibika kutokana na maambukizi ya muda mrefu. Pili VVU hubadilika badilika na kuwa na uwezo zaidi wa kuathiri tishu na sehemu mbalimbali za mwili na hata kuziua au kuharibu seli zinazokinga mwili kutokana na maambukizi, zinazojulikana kama T helper cell, seli T saidizi. 

Pia mwili hushindwa kumudu uharibifu wa seli T saidizi na kushindwa kuzalisha seli nyingine mpya.

Matumizi ya ARV

Dawa za kufubaisha virusi vya ukimwi au ARV huanza kutumiwa wakati seli aina ya CD4 zinapopungua na kufikia kiwango cha chini sana. 

Kupungua kwa seli hizi za CD4 ni kielelezo kwamba kinga ya mwili imekuwa dhaifu. 

Matumizi ya dawa hizi huboresha kinga ya mwili na kumfanya mgonjwa kuishi kwa muda mrefu bila kuonesha dalili au viashiria vyovyote vile, yaani kumrudisha mgonjwa katika hatua ya pili ambayo mwili huwa hauoneshi dalili za maambukizi. 

Kama mgonjwa wa VVU hatumii dawa za kufubaisha VVU au anatumia ARV's ambazo hazimsaidii au hazifanyi kazi vyema mwilini mwake, basi huendelea kuingia kwenye hatua ya nne ya Ukosefu wa Kinga Mwili (Ukimwi) au AIDS. 

Kama nilivyoeleza huko nyuma, hatua hii hujulikani kama Ukosefu wa Kinga Mwilini [UKIMWI] au AIDS, ambapo mgonjwa hupata maambukizi ya magonjwa nyemelezi pamoja na saratani za aina mbalimbali kutokana na kupungua kwa kinga mwilini.

Vigezo vilivyopangwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) ili kuweza kutambua kama mgonjwa yupo kwenye hatua hii ya UKIMWI hutofautiana kati ya watu wakubwa na watoto chini ya miaka 5. 

Pamoja na kuwa WHO wameweka vigezo vya pamoja, utambuzi wa hatua za ugonjwa wa UKIMWI hutofautiana kati ya nchi na nchi, kutokana na miongozo tofauti ya nchi hizo.

Kwa watu wazima na watoto walio na umri zaidi ya miaka mitano, uwepo wa ugonjwa wowote nyemelezi pamoja na kushuka kiwango cha CD4 chini ya 200 mm3 au kushuka kwa seli za CD4 chini ya asilimia 15 hutambulika kama ugonjwa wa UKIMWI. 

Kwa watoto walio chini ya miaka mitano, uwepo wa ugonjwa wowote nyemelezi au kushuka kwa seli za CD4 chini ya asilimia 20 kwa wale wenye umri kati ya miezi 12-35 hutambulika kama wana ugonjwa wa UKIMWI. 

Watoto wenye umri chini ya miezi 12, kupungua kwa seli za CD4 chini ya asilimia 25 ndiyo hutumika kutambulisha wana ugonjwa wa UKIMWI. Lakini hebu sasa tueleze CD4 ni nini?.

CD4 ni aina ya protini inayopatikana katika ukuta wa seli zinazojulikana kama seli T saidizi. VVU hushambulia na kujishikiza kwenye protini hii kabla ya kupata uwezo wa kuathiri seli T saidizi. 

Seli hizi za T helper ndizo hulinda mwili dhidi ya maambukizi mbalimbali na hivyo kuchangia katika kustawi kwa kinga ya mwili. Kupungua kwa seli hizi mwilini husababisha kupungua kwa kinga ya mwili na hivyo mtu kupata magonjwa mbalimbali.

Magonjwa nyemelezi

Baadhi ya magonjwa nyemelezi yanayoweza kumpata mtu mwenye ugonjwa VVU/UKIMWI ni pamoja na;

1.Magonjwa ya mfumo wa kupumua kama vile ugonjwa wa homa ya mapafu, kifua kikuu (TB) na saratani aina ya Kaposi's sarcoma.

2. Magonjwa ya mfumo wa chakula kama vile Cryptosporidiosis, fangasi za Candida, Cytomegolavirus (CMV) na Isosporiasis.

3. Magonjwa ya mfumo wa fahamu kama vile Cytomegolavirus, Toxoplasmosis, Cryptococcosis, saratani aina ya Non Hodgkin's lymphoma, Varicella Zoster ugonjwa unaojulikana kama mkanda wa jeshi na Herpes simplex.

4. Magonjwa mbalimbali ya ngozi kama vile Herpes simplex, Kaposi's sarcoma (saratani ya ngozi) na Varicella Zoster (mkanda wa jeshi).

Kutokana na uhaba wa vifaa vya kupimia kiwango cha seli aina ya CD4 katika nchi mbalimbali, Shirika la Afya Duniani WHO limetengeza mwongozo mwingine ambao utamsaidia mhudumu wa afya kuweza kutambua kama mgonjwa amefikia hatua gani ya ugonjwa wa UKIMWI na anastahili kuanza tiba au la. Uainishaji wa namna hii huitwa clinical classification of HIV/AIDS.

Hatua ya kwanza katika uainishaji huo ni: Mgonjwa hana dalili zozote, kuwepo kwa uvimbe katika tezi ambao hauondoki au hubakia muda mrefu. 

Hatua ya pili ya uainishaji wa hatua ya maambukizo ya Ukimwi ni, kupungua uzito chini ya asilimia 10 ya uzito wa mwili bila sababu maalumu, magonjwa ya mara kwa mara kwenye mfumo wa upumuaji kama magonjwa ya masikio, kinywa, tezi la koo na kadhalika na mkanda wa jeshi.

Dalili nyingine anazokuwa nazo mgonjwa wa Ukimwi anapokuwa kwenye hatua hii ni kuwa na vidonda pembezoni mwa mdomo, vidonda vya mara kwa mara kwenye kinywa, vipele mwilini, ugonjwa wa ngozi na maambukizi ya fangasi katika kucha.

Viashiria vingine

Viashiria na dalili zinazoainisha kwamba mgonjwa aliyeambukizwa Ukimwi yupo katika hatua ya tatu au Clinical stage III, ni

• Kupungua uzito kwa zaidi ya asilimia 10 ya uzito wa mwili bila sababu yoyote maalumu.

• Kuharisha zaidi ya mwezi mmoja bila sababu yoyote maalumu

• Kuwa na homa isiyoelezeka (homa hii inaweza kuwa inapona na kujirudia au homa ambayo inakuwepo kwa zaidi ya mwezi mmoja).

• Maambukizi ya fangasi kwenye kinywa (Persistent oral candiadiasis).

• Oral hairy leukoplakia

• Ugonjwa wa kifua kikuu kwenye mapafu (kwenye mapafu).

• Maambukizi hatari ya vimelea vya bakteria [homa ya mapafu, ugonjwa wa uti wa mgongo, maambukizi katika mifupa na jointi, empyema, pyomyositis, bacteraemia]

• Maambukizi hatari kwenye kinywa [Acute necrotizing ulcerative stomatitis, gingivitis or periodontitis]

• Upungufu wa damu mwilini bila sababu yoyote maalumu [Unexplained anaemia (below 8 g/dl), neutropenia (below 0.5 billion/l) and/or chronic thrombocytopenia (below 50 billion/l).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news