Waziri Mkuu akagua ujenzi wa daraja la Tanzanite

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amekagua ujenzi wa daraja la Tanzanite wa daraja jipya la Tanzanite (Salander) jijini Dar es Salaam na kwamba ameridhishwa na kasi ya mradi huo, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Picha ya juu na chini Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ujenzi wa daraja jipya la Tanzanite (Salander) jijini Dar es salaam, Desemba 22, 2020. Kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abubakar Kunenge. (Picha na ofisi ya Waziri Mkuu)
Amekagua ujenzi wa mradi huo leo Desemba 22, 2020. Daraja hilo lenye urefu wa kilomita 1.03 na upana mita 20.5 litagharimu sh. bilioni 243.75 na linatarajiwa kukamilika Oktoba 14, 2021.

“Nimekagua mradi na ujenzi wake unaendelea vizuri, sina mashaka na viwango na naamini utakamilika kwa wakati. Watanzania wanasubiri kwa hamu waanze kupita katika daraja hili,"amesema.

Waziri Mkuu amesema, ameridhishwa na ushiriki wa Watanzania katika ujenzi wa miradi mikubwa inayoendelea kutekelezwa nchini kwa kuwa inachangia katika kuongeza wataalamu.

Ujenzi wa daraja hilo una lengo la kupunguza msongamano wa magari kwenye barabara ya Ali Hassan Mwinyi ambayo inatumiwa na magari mengi yanayoingia na kutoka katikati ya jiji la Dar es Salaam.

Mkandarasi anayejenga mradi huo ni kampuni ya GS Engineering Corporation kutoka Korea Kusini na hadi Novemba 30, 2020 utekelezaji wake ulikuwa umefikia asilimia 60.8.

Awali, Mkurugenzi wa Miradi wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mhandisi Christianus Ako alisema hesabu ya mwaka 2017 ilionesha kuwa kiasi cha magari yanayopita kwenye barabara ya Ali Hassan Mwinyi kwa siku kuwa ni wastani wa magari 42,000.

Alisema hadi sasa mradi umeajiri jumla ya wafanyakazi 590, kati yao asilimia 92 ni Watanzania na asilimia nane tu ni wataalamu kutoka nje ya nchi.

Mhandisi Ako alisema mradi huo pia unaendelea kutoa mafunzo kwa wahandisi 24 wa Kitanzania kutoka Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (5), wahandisi wahitimu (12) na wanafunzi wa uhandisi kutoka vyuo vikuu (7). “Mafunzo haya yatawajengea uwezo na ujuzi utakaosaidia Taifa hapo baadae"amesema.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news