Bondia Amos Mwamakula ametambulisha mpambano wake wa kuzipiga na Hashimu Kilaga mpambano utakaofanyika katika ukumbi wa P.T.A uliopo viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam siku ya Februari 6, 2021, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Kocha wa mchezo wa masumbwi na mateke (kick boxing), Esmail Abdallah ‘Van Dame’ kushoto akimwinua mkono juu bondia Amosi Mwamakula kwa ajili ya kumtambulisha katika mpambano wake wa Februari 6, 2021 katika ukumbi wa P.T.A Sabasaba jijini Dar es Salaam dhidi ya Hashimu Kilaga.
Akizungumza na waandishi wa habari juu ya mpambano hUo kocha wa masumbwi na mateke (kick boxing), Esmail Abdallah ‘Van Dame’ amesema kuwa, Mwamakula amejiandaa vya kutosha hivyo mpinzani wake nae ajiandae vya kutosha kwani kwa sasa amerudi kivingine.
Van Dame ameongeza kuwa, kwa sasa wanaendelea na mazoezi kwa ajili ya pambano hilo ambalo linaandaliwa kwa ubora wa aina yake kwani maandalizi ya mpambano huo sasa yamepamba moto.
Ameeleza kuwa, mbali na pambano hilo la masumbwi pia kutakuwa na mapambano mengine ya ngumi ambapo bondia Lulu Kayage atazipiga na Agnes Kayange na Jitu Rajabu kutoka kwa Super D Coach atazipiga na Daniel Mwakafyale na Shabani Kaoneka atazipiga na Butel Obedi.
Van Dames amesema kuwa, mpambano huo unaletwa na Jamukaya kwa kushilikiana na Black Panda na utakuwa na kingilio cha shilingi 10,000 tu kwa siku hiyo.
Aidha, amesema kuwa, pia kutakuwa na ngumi za mateke (kick boxing) na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Innocent Bashungwa.