Kamati ya Uongozi MKURABITA kuanza ziara ya siku nne Zanzibar

Kamati ya Uongozi ya Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA), inatarajia kufanya ziara yake Zanzibar kuanzia tarehe 8 hadi 11 Februari 2021,anaripoti Mwandishi Diramakini.

Mratibu wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA), Dkt.Seraphia Mgembe.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kitengo cha Uongozi MKURABITA, ziara hii ni mwendelezo wa ziara iliyofanyika mwezi Januari 2021 katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, Mbarali na Mji Njombe kwa upande wa Tanzania Bara.

Lengo la ziara ni kufuatilia na kujionea utekelezaji wa shughuli za urasimishaji nchini ili kamati iweze kushauri na kutoa maelekezo kwa ajili ya kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa ajenda ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kupitia urasimshaji rasilimali ardhi na biashara.

Ikiwa Zanzibar, kamati inatarajia kukutana na watendaji wanaotekeleza na kusimamia shughuli za urasimishaji, kushiriki zoezi la utoaji wa hati za matumizi ya ardhi katika Wilaya ya Kaskazini A, kutembelea kituo jumuishi cha urasimishaji na uendelezaji biashara kilichopo Darajani, Wilaya ya Mjini pamoja na kuwatembelea baadhi ya wananchi walionufaika na shughuli za urasimishaji nakusikia shuhuda zao kuhusu tija na manufaa yaliyopatikana.

Aidha, Wajumbe wa Kamati pamoja na menejimenti ya MKURABITA watapata fursa ya kukutana na Rais wa Awamu ya Nane na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi kwa ajili ya kumpongeza na kuelezea jinsi MKURABITA ilivyojipanga katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi, 2025 kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 143.

Baadhi ya shughuli ambazo zimetekelezwa na MKURBITA Zanzibar kwa kushirikiana na Wizara za kisekta pamoja na taasisi mbalimbali za umma ni pamoja na upimaji wa jumla ya viwanja 8,552 ambavyo vimetambuliwa, hati za matumizi ya ardhi 7,625 zimesajiliwa na zinaendelea kutolewa kwa wananchi.
Aidha, MKURABITA kwa kushirikiana na wizara inayohusika na masuala ya biashara imetoa mafunzo kwa wafanyabiashara 2,600 na kurasimisha jumla ya biashara 1,289.

Shughuli za urasimishaji ardhi na biashara zinaendelea ikiwa ni pamoja na uanzishwaji wa vituo jumuishi vya urasimishaji na uendelezaji biashara Zanzibar na kutoa mafunzo ya kujenga uwezo wa wananchi waliorasimisha ardhi ili kuwawezesha kuunganishwa na huduma za ukuzaji wa mitaji yao na fursa mbalimbali za kiuchumi ikiwemo uwekezaji nje na ndani ya Zanzibar.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news