Serikali kupitia Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA) imerejesha furaha na matumaini kwa wakazi wa Mkoa wa Pwani wanaoishi kisiwa cha Mafia na eneo la Nyamisati baada ya kutekeleza mojawapo ya ahadi zake iliyowekwa katika ilani ya uchaguzi ya chama tawala ya mwaka 2015-2020 kwa kuwapelekea kivuko kipya cha MV. Kilindoni Hapa Kazi Tu,anaripoti Mwandishi Diramakini.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo akikata utepe kuashiria kukipokea rasmi kivuko kipya cha MV. KILINDONI HAPA KAZI TU ambacho amekipokea leo kutoka kwa makandarsi Songoro Marine Transport Boatyard katika hafla fupi iliyofanyika katika kisiwa cha Mafia Mkoani Pwani. Kivuko hicho kimegharimu shilingi bilioni 5.3 na kina uwezo wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100 na kitakuwa kinatoa huduma kati ya Mafia na Nyamisati.
Kwa muda mrefu wakazi wa maeneo hayo hawakuwa na usafiri wa uhakika na
hiyo iliwalazimu kutumia boti ndogo na majahazi kwa ajili ya
kusafirishia mizigo na abiria na hivyo kuhatarisha maisha yao baharini
endapo ingetokea dharura ya ajali.
Kivuko hicho kipya
kilichogharimu shilingi Bilioni 5.3 mpaka kukamilika kwake na ambacho
ujenzi wake umegharamiwa na Serikali kwa kutumia fedha za ndani,
kimejengwa na kampuni ya kizalendo ya Songoro Marine Transport Boatyard
ya jijini Mwanza katika karakana yake ya kujengea na kukarabati vivuko
iliyopo Kigamboni jijini Dar es salaam na kina uwezo wa kubeba abiria
200 na magari 10 ambazo ni sawa na tani 100.
Akizungumza katika
hafla fupi ya kupokea kivuko hicho iliyofanyika katika kisiwa cha Mafia
na kuhudhuriwa na viongozi wa mkoa huo, mgeni rasmi, Mkuu wa Mkoa wa
Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano
kwa kuweza kutoa fedha zote hizo kwa ajli ya kuhudumia wananchi wake na
pia aliupongeza Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) kwa kuweza kusimamia
ujenzi wa Kivuko hicho hadi kukamilika kwake.
Kivuko cha MV. KILINDONI HAPA KAZI TU kikielea majini mara baada ya kupokelewa rasmi leo na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo katika hafla fupi iliyofanyika katika kisiwa cha Mafia Mkoani Pwani. Kivuko hicho kimegharimu shilingi bilioni 5.3 na kina uwezo wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100 na kitakuwa kinatoa huduma kati ya Mafia na Nyamisati.
‘’Kama mlivyosikia
katika hotuba zilizotangulia wakala umekamilisha miradi ya ujenzi wa
vivuko vipya vya Kayenze-Bezi, Bugolora-Ukara na Chato-Nkome na kufanya
vivuko vipya vilivyonunuliwa katika mwaka wa fedha 2019/20 kuwa vinne
kikiwepo hiki cha Kilindoni tunachokipokea leo kwa pamoja vikiwa
vimegharimu jumla ya Shilingi bilioni 15.3.
"Haya yote ni
matunda ya kazi nzuri inayoendelea kufanywa na Serikali ya awamu ya tano
chini ya Jemedari wetu Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,’’amesema.
Ndikilo ameongeza
kuwa, kwa kuwa kivuko hicho ni rasilimali muhimu ya Taifa na
kinahitajiwa na wananchi wa Mafia na Nyamisati, aliuagiza Wakala wa
Ufundi na Umeme (TEMESA) kusimamia kwa karibu uendeshaji wake ili
wananchi wafaidi matunda mazuri ya Serikali yao kwa fursa ya maendeleo
yao binafsi na nchi nzima kwa ujumla wake na pia aliwasisitizia wananchi
wa Mafia na Nyamisati kukitunza kivuko hicho na kuwapa ushirikiano wa
kutosha wahudumu wake kiweze kuwahudumia kwa kipindi kirefu.
Naye
mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Arch. Elius Mwakalinga,
Mhandisi Elizabeth Manzi akizungumza katika hafla hiyo alisema ni
dhamira ya Serikali kutaka kutoa huduma iliyo bora yenye kukuza uchumi
wa nchi ya Tanzania na katika mwaka wa fedha 2019/20, Serikali ilitoa
jumla ya Billioni 12,245,214,800.00 kwa ajili ya miradi ya vivuko na
maegesho ambayo inatekelezwa na Wakala wa Ufundi na Umeme na fedha hizo
zinatokana na Mfuko Mkuu wa Serikali na Mfuko wa Barabara.
Awali,
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Mhandisi Japhet
Maselle, akisoma taarifa fupi ya ujenzi wa kivuko hicho amesema, kazi ya
ujenzi huo imefanywa kulingana na viwango vinavyokubalika Kimataifa
(IMO Standards).
"Kivuko hiki kimefanyiwa ukaguzi wa mwisho
kabla ya kuanza kazi na Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC)
ambao walikuwa wakishiriki ukaguzi wakati wa ujenzi ili kuthibitisha
viwango vya usalama wa abiria, magari na mizigo,’’alisema Mhandisi
Maselle ambapo aliongeza kuwa baada ya ukaguzi wa mwisho TASAC wamefanya
usajili wa kivuko hiki kabla hakijaanza kazi kwa jina la MV
Kilindoni-Hapa Kazi Tu.
Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo katikati akipewa maelezo na nahodha wa kivuko cha MV. KILINDONI HAPA KAZI TU wakati akikagua kivuko hicho mara baada ya kukipokea rasmi leo hafla fupi iliyofanyika katika kisiwa cha Mafia Mkoani Pwani. Kivuko hicho kimegharimu shilingi bilioni 5.3 na kina uwezo wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100 na kitakuwa kinatoa huduma kati ya Mafia na Nyamisati.
‘’Ili kuhakikisha usalama wa kivuko hiki
kinapofanya kazi kimefungwa vifaa stahiki vya kuongozea kama vile Radar,
GPS, Echo Sounder, vifaa vya mawasiliano (Communication equipment) na
vifaa vya uokoaji vya kutosha kwa watu wazima na watoto ambavyo ni
makoti ya kujiokoa (life jackets) na maboya (life rafts na life
buoys),’’amesema.Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikilo akisisitiza jambo wakati wa mapokezi ya kivuko cha MV. KILINDONI HAPA KAZI TU, hafla iliyofanyika katika kisiwa cha Mafia mkoani Pwani. Kivuko hicho kimegharimu shilingi bilioni 5.3 na kina uwezo wa kubeba abiria 200 na magari 10 sawa na tani 100 na kitakuwa kinatoa huduma kati ya Mafia na Nyamisati.
Mtendaji Mkuu ambapo alishukuru Serikali kwa
kuendelea kuuamini wakala katika kutekeleza miradi hiyo na pia kuendelea
kutenga fedha kwa ajili ya miradi ya vivuko kwa lengo la kuboresha
huduma za usafirishaji katika maeneo mbalimbali nchini na kuahidi
kukitunza kivuko hicho kwa kukifanyia matengenezo kama inavyotakiwa ili
kiweze kudumu na kutoa huduma bora kwa wananchi kwa wakati wote.
Kukamilika
kwa ujenzi wa kivuko cha MV.Kilindoni Hapa Kazi Tu kunafanya idadi ya
vivuko kote nchini kufikia 33 hadi hivi sasa na hivyo kuifanya serikali
kuendelea kuboresha miundombinu ya usafiri kwa manufaa ya wananchi
wengi.