Serikali yatangaza ifikapo 2022 haitatoa vibali vya kuagiza sukari nje

Waziri wa Kilimo Prof. Adof Mkenda ametoa onyo kwa makampuni ya uzalishaji sukari kuwa ifikapo mwaka 2022 Serikali haitatoa vibali vya kuagiza sukari nje badala yake wanatakiwa waongeze uchakataji wa miwa ya wakulima na kuzalisha sukari ya kutosha mahitaji ya ndani, anaripoti Mwandishi Diramakini.

Ametoa kauli hiyo leo wakati akiongea na uongozi wa Mkoa wa Morogoro akiwa ziarani kukagua hali ya uzalishaji sukari na kuongea na wakulima wa miwa na kuwa serikali inafuatilia kwa karibu utendaji kazi wa viwanda vya kuchakata sukari nchini.

"Shida yetu ya sukari haitokani na kukosa miwa bali ni uwezo mdogo wa viwanda kuchakata miwa yote ya wakulima nchini hali inayosababisha baadhi ya miwa ya wakulima kukosa soko,"amesema Waziri Mkenda.

Prof. Mkenda alibainisha kuwa wizara ya kilimo ina mkakati wa kuhakikisha miwa yote ya wakulima inachakatwa na viwanda vilivyopo ili kuondoa tatizo la upungufu wa sukari na kuwa utaratibu wa sasa viwanda kupewa vibali vya kuagiza sukari nje hauna manufaa kwa taifa.

Ili kuwa na uhakika wa sukari Prof. Mkenda amesema, wizara inahamasisha matumizi ya mbegu bora na kilimo cha umwagiliaji pamoja na kuhamasisha ujenzi wa viwanda vipya vya sukari.

"Mwaka huu vibali vya kuagiza sukari itakayopungua itatolewa kwa makampuni kwa utaratibu wa kawaida lakini ifikapo mwaka 2022 hakutakuwa na vibali vya viwanda na ikilazimu basi Bodi ya Sukari ndio itapewa kibali cha kuagiza sukari itakayopungua,"amesisitiza Prof Mkenda.

Naye Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro Mhandisi Emanuel Kalobero amesema mkoa huo una viwanda vitatu vya kuzalisha sukari ambavyo bado uzalishaji wake ni mdogo hali inayopelekea miwa ya wakulima kukosa soko na kuharibika.

Ametaja viwanda hivyo na uzalishaji wake kwenye kuwa ni Kilombero Sugar Ltd I na Kilombero Sugar II kwa pamoja huzalisha (tani 126,000) na kiwanda cha Mtibwa (tani 50,000) huku uzalishaji wa miwa kwenye bonde la Kilombero unaofanywa na wakulima wadogo umefikia wastani wa tani 800,000 hadi 1,000,000 na uwezo wa kiwanda cha Kilombero ni kuchakata tani 600,000 tu za wakulima wadogo kwa mwaka.

"Mfano uzalishaji wa miwa ya wakulima wadogo outgrowers ni kati ya tani 800,000 hadi 1,000 000 na uwezo wa kiwanda ni tani 600,000,"amesema Kalobero.

Kwa mujibu wa takwimu za Bodi ya Sukari Tanzania uzalishaji kwa mwaka ni takribani tani 300,000 ambapo kwa mwaka 2020/21 ulifikia tani 377,527 na mahitaji ya sukari kwa matumizi ya kawaida na viwandani ni tani 655,000. Viwanda vinavyozalisha sukari ni pamoja na Kilombero, Mtibwa,Kagera,TPC na Manyara.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news