SERIKALI KUTATUA CHANGAMOTO YA USAFIRI BARABARA YA MALINYI NA MLIMBA

Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, amewahakikishia wananchi wa Malinyi na Mlimba, mkoani Morogoro, kuwa Serikali itaendelea kuboresha barabara za kitaifa zilizopo kwenye majimbo hayo ili kuhakikisha zinapitika kipindi chote cha mwaka.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri huyo wakati akikagua miundombinu ya barabara ya Lupiro- Malinyi Junction- Kilosa kwa Mpepo- Tunduru (Km 282.6) na barabara ya Ifakara- Mlimba- Taweta - Madeke (Km 220) ambapo pamoja na mambo mengine Naibu Waziri huyo amesema kuwa barabara hizo ni muhimu kwa kuwa zinarahisisha huduma za usafiri na usafirishaji kutoka mkoa huo na mikoa jirani ya Njombe na Ruvuma.
Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, akitoa maelekezo kwa Meneja wa Wakala wa Barabara(TANROADS) mkoa wa Morogoro, Mhandisi Nkolante Ntije, mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kalvati lililoko katika barabara ya Ifakara-Mlimba, Mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki.

"Nimefanya ziara katika maeneo haya na nimeona athari zilizotokea ikiwemo mashimo makubwa,makalvati kukatika,na maeneo mengine maji kupita juu ya madaraja na kusababisha kutopitika", amesema Kasekenya.

Aidha, ameongeza kuwa, ujio wa ziara yake katika majimbo hayo utasaidia kwa namna moja ama nyingine kutafuta fedha haraka ili barabara hizo ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Amefafanua kwa sasa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani humo utaendelea na matengenezo katika sehemu zilizoathirika baada ya mvua za masika kuisha.
Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya (mwenye miwani), akimsikiliza Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Morogoro, Mhandisi Nkolante Ntije, wakati akitoa maelezo kuhusu uboreshaji utakaofanyika katika daraja lililopo barabara ya Lupiro- Malinyi Junction – Kilosa kwa Mpepo –Tunduru (Km 282.2) Mkoani Morogoro, mwishoni mwa wiki.
Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, (mwenye miwani), akiangalia daraja linalotumiwa kwa sasa na wananchi wa Malinyi kuingia Malinyi Mjini baada ya daraja la awali kuzingirwa na maji kutokana na athari za mvua Mkoani Morogoro, mwishoni mwa wiki.

Amewataka wananchi wa mkoa huo kulinda miundombinu kwa kufanya shughuli za kilimo na ufugaji nje ya eneo la hifadhi ya barabara kwani kuingia ndani ya mipaka hiyo kumesababisha uharibifu mkubwa wa miundobinu.

Akiwa katika jimbo la Mlimba, Kasekenya pia amekagua hali ya utendaji kazi katika Stesheni ya reli ya Mlimba mkoani humo na kuwataka wafanyakazi wa Stesheni hiyo kufanya kazi kwa uweledi na ubunifu ili kuongeza mapato katika Stesheni hiyo.

Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Morogoro, Mhandisi Nkolante Ntije, amesema kuwa uwekaji wa changarawe na uchongaji wa barabara kuanzia Londo hadi Kihansi (km 71) umekamilika.
Muonekano wa Daraja linalounganisha kijiji cha na Malinyi Mjini linalojengwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Morogoro, ambalo ujenzi wake umesimama kutoka na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha mkoani humo.
Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya, akitoa maelekezo kwa Meneja Masoko wa Shirika la Reli ya Tanzania na Zambia (TAZARA), Stesheni ya Mlimba, Bw. Lucas Philemon (Wapili kushoto), mara baada ya Naibu Waziri huyo kukagua stesheni hiyo, Mkoani Morogoro mwishoni mwa wiki.

Aidha, Mhandisi Ntije amefafanua kuwa kwa sasa ujenzi wa makalvati mawili katika barabara ya Lukolongo hadi Ijia nao umekamilka.

Nao, wananchi wa Malinyi wameiomba Serikali kuhakikisha wanakarabati makalvati yaliyobomoka ili yaweze kupitisha maji ambayo yamekuwa yakituama na kusababisha kuingia kwenye makazi yao na hivyo kuhatarisha maisha yao.
Muonekano wa athari za mvua zinazoendelea kunyesha ziilizotokea kwenye barabara ya Ifakara-Mlimba -Tawete- Madeke (Km 220) Mkoani Morogoro. Barabara hiyo iko kwenye mpango wa kujengwa katika kiwango cha lami ambapo itaunganisha Mkoa wa Morogoro na Ruvuma.
Muonekano wa Daraja linalounganisha kijiji cha na Malinyi Mjini linalojengwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) mkoa wa Morogoro, ambalo ujenzi wake umesimama kutoka na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha mkoani humo.

Naibu Waziri Kasekenya amemaliza ziara yake ya kikazi ya siku mbili katika majimbo ya Mlimba na Malinyi mkoani Morogoro kujionea hali halisi ya miundombinu katika mkoa huo ambapo pamoja na mambo mengine alikagua utekelezaji wa kazi za matengenezo ya madaraja na barabara za Ifakara- Mlimba -Taweta - Madeke (Km 220) na Lupiro- Malinyi Junction- Kilosa kwa Mpepo- Tunduru (Km 282.6).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news