Ripoti ya CAG yatua kwa Rais Dkt.Mwinyi, atoa onyo kali

Na Diramakini Blog (diramakini@gmail.com)

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameahidi kwamba hatua kali zitachukuliwa kwa wale wote waliohusika na kasoro zilitolewa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ili kasoro hizo zisije kurudiwa tena.
Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo leo mara baada ya kukabidhiwa Ripoti za Hesabu za Serikali kwa mwaka 2019 -2020, huko katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar, hafla ambayo imehudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa fedha nyingi za Serikali zinapotea kwa kiasi kikubwa na iwapo hali hiyo itaendelea maendeleo hayatoweza kupatikana katika kuijenga nchi.

Alisema kuwa lengo na madhumuni ya kupokea ripoti hiyo hadharani ni katika suala zima la kuhimiza uwajibikaji na utawala bora kwani ni lazima Serikali iwe wazi na kujulikana changamoto ndipo itakapowezekana kukabiliana na matatizo kama hayo.

Aliongeza kwamba katika Taasisi za ukusanyaji wa fedha bado kuna upotevu wa udhaifu wa mifumo na hata dhamira ovu ya watendaji katika ukusanyaji wa fedha za Serikali.

Rais Dk. Mwinyi alisisitiza kwamba mbali ya suala la ukusanyaji pia katika Taasisi hizo kunaonekana kwamba kuna udhaifu wa matumizi ambalo nalo limepelekea upotevu mkubwa wa fedha za Serikali ambapo hata kile kidogo kinachokusanywa hakitumiki vizuri.

Alisema kuwa hali hiyo ni vyema ikawafanya wote wakatafakari na kufanya ama kuchukua hatua za msingi za kudhibiti hali hiyo.

Hivyo, Dk. Mwinyi alisema kuwa haiwezekani ionekane kumepokewa tu taarifa hiyo bali ni lazima hatua zinazohitajika zikachukuliwa hasa ikizingatiwa kwamba fedha hizo zinahitajika katika kuimarisha miradi ya maendeleo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news