Walimu 1,333 Kinondoni kupandishwa madaraja

Na Adili Mhina- TSC

Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC) Wilaya ya Kinondoni ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha zoezi la kupandisha vyeo/madaraja walimu 1,333 wa shule za msingi na sekondari wa Manispaa ya Kinondoni ambao wana sifa za kupanda vyeo kwa mujibu wa miongozo na taratibu za Serikali.
Kaimu Katibu Msaidizi wa TSC Wilaya ya Kinondoni, Theobald Kilindo akiwasilisha taarifa ya hatua ya utekelezaji wa zoezi la kuwapandisha vyeo walimu kwa Mkurugenzi wa Ajira, Maadili na Maendeleo ya Walimu kutoka TSC Makao Makuu, Christina Hape (hayupo pichani) wakati wa ziara ya Mkurugenzi huyo aliyoifanya wilayani hapo hivi karibuni.

Hayo yamebainishwa na Kaimu Katibu Msaidizi wa TSC wa Wilaya hiyo, Theobald Kilindo wakati akitoa taarifa kwa Mkurugenzi wa Ajira, Maadili na Maendeleo ya Walimu kutoka TSC Makao Makuu, Christina Hape juu ya hatua iliyofikiwa katika zoezi la kuwapandisha vyeo walimu wa Manispaa hiyo.

Kilindo alieleza kuwa ofisi yake imepitia hatua mbalimbali katika kufanya zoezi hilo, ambapo kila hatua ilifanyika kwa uangalifu mkubwa na pale zilipobainika changamoto ofisi yake iliwasiliana na mamlaka zingine kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi.

Alieleza kuwa zoezi hilo lilianza kwa mwajiri kuwasilisha orodha ya walimu waliopendekezwa kupandishwa vyeo ili ofisi yake iendelee na hatua zaidi kwa mujibu wa Sheria ya Tume ya Utumishi wa Walimu Na. 25 ya Mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2016.
Mkurugenzi wa Ajira, Maadili na Maendeleo ya Walimu kutoka TSC Makao Makuu, Christina Hape akisikiliza taarifa kutoka kwa Kaimu Katibu Msaidizi wa TSC Wilaya ya Kinondoni, Theobald Kilindo (hayupo pichani) wakati wa ziara ya Mkurugenzi huyo iliyolenga kuangazi zoezi la uoandishaji vyeo walimu wa Manispaa ya Kinondoni.
Mkurugenzi wa Ajira, Maadili na Maendeleo ya Walimu kutoka TSC Makao Makuu, Christina Hape akikagua baadhi ya majalada kwa lengo la kujiridhisha juu ya uzingatiaji wa taratibu katika zoezi la kupandisha vyeo walimu wa Manispaa ya Kinondoni.

“Tuliletewa barua na Mkurugenzi iliyotutaka tuanze zoezi la kupandisha vyeo walimu. Tuliitisha majalada yote ya walimu na kuanza kuyachambua ili tuweze kubaini walimu wenye sifa za kupanda vyeo. Tulianza zoezi la uchambuzi Mei 3 na kulihitimisha Mei 11,” alisema.

Alieleza kuwa katika hatua ya uchambuzi walibaini dosari ndogondogo katika ujazaji wa fomu za Mfumo wa Wazi wa Mapitio na Tathmini ya Utendaji Kazi (OPRAS) jambo ambalo liliwalazimu kuwasiliana na mwajiri pamoja na wakuu wa shule ili kuondoa kasoro hizo.

“Sio kwamba kuna madadiliko yoyote tuliyofanya kwenye OPRAS ila tuligundua kwamba wakati wa kujaza, wengi hawakuwa na uelewa wa kutosha wa nini kinatakiwa kijazwe wapi na kwa namna gani. Tuliona baadhi walikuwa wamekosea pale kwenye kutafuta wastani walikuwa wanaweka namba ambazo hazikuwa sahihi,” Silindo alifafanua.
Baadhi ya Watumishi wa TSC Wilaya ya Kinondoni wakifanya uchambuzi wa majadala ya walimu kwa lengo la kubaini wenye sifa za kupandishwa vyeo.

Aliendelea kueleza kuwa uchambuzi ulipokamilika walipitia Ikama ya walimu ya miaka mitatu (2018/2019, 2019/2020 na 2020/2021) na kuona kuwa Manispaa hiyo ina jumla ya nafasi 2874 za kupandisha vyeo walimu katika madaraja mbalimbali.

“Baada ya taratibu zote kukamilika, Kamati ya TSC Wilaya ambayo ndiyo yenye wajibu kisheria wa kupandisha vyeo walimu, ilifanya kikao chake Mei 12, 2021 na kuwapandisha vyeo walimu 1,333 ambao ndio waliokuwa na sifa,” alifafanua.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Ajira, Maadili na Maendeleo ya Walimu, Christina Hape alieleza kuwa Serikali ilifanya jambo la busara kwa kuamua kuchukua Ikama za miaka mitatu na kuzifanyia kazi kwa pamoja kwa kuwa hatua hiyo inaondoa kabisa malalamiko ya madaraja kwa walimu.
Mmoja wa Watumishi wa TSC Wilaya ya Kinondoni akifanya uchambuzi wa majadala ya walimu kwa lengo la kubaini wenye sifa za kupandishwa vyeo.

Pamoja na kupongeza hatua hiyo, Hape alitoa wito kwa Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kujitahidi kuwabadilishia mishara walimu mapema iwezekanavyo ili wakiingia kwenye vyeo vipya mishahara yao nayo iwe imebadilika.

“Unajua ukimwambia mwalimu umepanda cheo anataka aone mshahara umebadilika, kumpatia karatasi (barua) ya kupanda cheo peke yake bila yeye kuona maslahi yake yameboreshwa haitakuwa na faida sana kwake. Hivyo, napenda niwaombe wenzetu wa UTUMISHI kuhakikisha wanafanya kila linalowezekana ili mishahara ya walimu iendane na vyeo vyao kwa wakati”, alisema.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news