NA MWANDISHI DIRAMAKINI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Juni 21, 2021 amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Xi Jinping.
Taarifa iliyotolewa leo na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Jaffar Haniu, imesema, Rais Xi Jinping amempongeza Rais Samia kwa kuchukua kijiti cha uongozi na kumpa pole kwa kuondokewa na Rais wa Awamu ya Tano Hayati Dk. John Magufuli.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza kwa njia ya Simu na Rais wa China Xi Jinping Ofisini kwake Ikulu Chamwino Mkoani Dodoma leo tarehe 21 Juni, 2021. (PICHA NA IKULU).
Katika mazungumnzo hayo Tanzania na China zimekubaliana kukuza ushirikiano katika nyanja za uchumi, utamaduni na ushirikiano wa Kimataifa.
China imeahidi kufungua zaidi soko lake kwa bidhaa za Tanzania pamoja na kuongeza uwekezaji hususan katika sekta ya viwanda.
Aidha, kupitia mazungumzo hayo China imeahidi kuunga mkono jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika nyanja mbalimbali.
Rais Samia Suluhu Hassan ametumia fursa ya mazungumzo hayo kutoa salamu za pongezi kwa Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) kwa kuadhimisha Miaka 100 tangu kuanzishwa kwake na ameahidi kudumisha uhusiano wa kidugu na kihistoria uliopo kati ya Chama hicho na Chama cha Mapinduzi (CCM).
Tags
Habari