Shaka ang'aka, atoa maelekezo mazito kwa DC wa Rungwe, abaini hujuma

NA MWANDISHI DIRAMAKINI, Mbeya

Chama cha Mapinduzi kimesikitishwa na ongezeko la matatizo ya ujauzito na utoro yaliokithiri kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari katika halmashauri ya wilaya ya Rungwe tabia ambayo inachangiwa na vitendo vya rushwa na urasimu uliokithiri.

Kimebainisha kuwa ni ajabu katika halmashauri hiyo wamejiwekea utaratibu wa kuwapiga faini wazazi ambao watoto wao ni watoro au wamepata ujauzito. Kwa wazazi ambao wanafunzi wao wamepeana ujauzito wanapigwa faini ya shilingi laki mbili na elfu arobaini na tano kila mmoja.

Vitendo hivyo vimemchefua Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa Itikadi na Uenezi Ndugu Shaka Hamdu Shaka wakati akiwa katika mkutano wa Shina 3 Kata ya Kandete, kijiji cha Mwela Busekelo mkoani hapa na kumuagiza Mkuu wa wilaya ya Rungwe Dkt. Vincent Anney kusitisha utekelezaji wa uamuzi wa bodi za shule na kurejeshwa kwa fedha zote zilizokusanywa kama faini kwa waliowapa na waliopokea (wanafunzi) wa shule za sekondari na msingi.

"Hatuwezi kukomesha vitendo vya kuwapa mimba watoto wetu wa kike kwa kuendelea kutozana faini kwa wazazi wote, yaani mtu mwanaye anapewa mimba na pesa anatozwa (245,000) na mifuko 10 ya saruju pamoja na mtenda kosa hilo halafu wote wanarejea kwenye jamii,"amesema Shaka.

Amefahamisha kuwa jambo hilo ni kinyume na sheria ya elimu na kwa namna yoyote haiwezekani kwa waliopewa dhamana ya kuisimamia na kutafsiri sheria kubadilisha maudhui na kutasiri wanavyotaka wenyewe.

"Maelekezo ya Chama, mkuu wa Wilaya sitisha utekelezaji wa uamuzi huu kwa shule zote, na fedha zote zilizokusanywa zirejeshwe kwa wahusika na hatua stahiki kwa mujibu wa sheria zichukuliwe kwa waliohusika na tupewe mrejesho ndani ya siku saba,"amesisitiza Shaka.

Shaka amefahamisha kuwa rushwa na urasimu ni vitendo na tabia ambazo hazitavumiliwa hata kidogo na CCM na serikali zake katika kuwaletea maendeleo endelevu wananchi haitutakubali kuona baadhi ya watumishi, watendaji na viongozi waliokosa uadilifu wanawagombanisha na wananchi watatendaji hao CCM itaielekeza serikali wapishe mapema ili watanzania wengine wapewe dhamana hizo kuendeleza gurudumu la maendeleo.

"Niwaombe na nitoe raia kwa mawaziri, manaibu mawaziri na watendaji wote waliaminiwa na Rais Samia kumsaidia wanapokuja ziara mikoani washuke hadi vijijni kusikiliza wananchi kama anavyofanya Waziri Mkuu Majaliwa, huku kuna shida kubwa wasiridhike na ripoti za mapambio wanazopatiwa, washuke waje waone uhalisi itawasaidia sana kuwatathmini wasaidizi wao wa ngazi za chini kama wanakidhi haja ya mbio za kuwaletea wananchi maendeleo,"amefahamisha Shaka.

Shaka amesema inasikitisha kuona mama mjane mwenye miaka 67 ambaye binti yake alipewa ujauzito na anapigwa faini 245,000 na mifuko 10 saruji, kinyume na sheria ya elimu huku mkurugenzi, Tarafa wapo lakini mtendaji wa kata anavunja sheria za nchi wanaeleana wakati wananchi zaidi kuumia na kuwarudisha nyuma kiuchumi.

"Waliopewa dhamana lazima mtafisiri kwa usahihi sheria za nchi ili kutoibua kero zaidi kwa wananchi. Jamii iwalinde watoto ili wakue katika malezi mazuri na kupata elimu waje kutumikia nchi yao,"amesema Shaka.

Hata hivyo katika katika kikao hicho wananchi walilalamikia utaratibu wa wao kutakiwa kununua mbolea toka kwenye maduka ya pembejeo ya maafisa ugani ndio wapewe mbolea iliyotokana na ruzuku ya serikali bila kufanya hivyo hawapati mbolea ya ruzuku jambo ambalo sio sawa.

Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Ndugu Daniel Chongolo na Sekretarieti yake ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa anaendelea na ziara yake mkoani Mbeya.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news