Tanzania, China zaahidi kuimarisha misingi ya kidplomasia

NA MWANDISHI MAALUM

Tanzania na China zimeahidi kuendelea kuimarisha misingi ya uhusiano wa diplomasia baina ya mataifa hayo iliyodumu kwa zaidi ya miaka 50 kwa lengo la kukuza na kuendeleza maendeleo endelevu kwa maslahi mapana ya pande zote mbili.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) akiongea na Balozi wa China hapa nchini Mhe. Chen Mingjian wakati walipokutana kwa mazungumzo leo katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

Ahadi hiyo imetolewa na Balozi wa China hapa nchini, Mhe. Chen Mingjian, wakati alipokutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) leo jijini Dar es Salaam.

Balozi Mulamula amesema kuwa pamoja na mambo mengine, wamejadili masuala mbalimbali ikiwemo suala la kukuza na kuendeleza misingi ya uhusiano wa kidiplomasia iliyowekwa wakati wa kuanzisha mahusiano ya kidiplomasia baina ya mataifa haya 1964.
Balozi wa China hapa nchini Mhe. Chen Mingjian akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) wakati walipokutana kwa mazungumzo leo katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

“Uhusiano wa Tanzania na China ni wa muda mrefu na umekuwa imara katika nyakati zote hii ni kutokana na kila taifa kuheshimu misingi ya taifa jingine na kutokuingilia masuala ya ndani ya taifa jingine, naamini kwa kuzingatia misingi hii uhusiano huu utaendelea kukua na kuimarika zaidi,”amesema Balozi Mulamula.

Balozi Mulamula ameongeza kuwa wakati wote Tanzania na China zimekuwa na maelewano mazuri ambayo yamechangia kuimarisha diplomasia kwa mataifa hayo.

Balozi wa China hapa nchini, Mhe. Chen Mingjian, ameishukuru Tanzania kwa ushirikiano ambao imekuwa ikimpatia tangu aliwasili na kuongeza kuwa China itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kukuza na kuendeleza ushirikiano wa kufanya kazi kwa pamoja kwa manufaa ya mataifa mawili.
Mazungumzo baina ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa China hapa nchini Mhe. Chen Mingjian yakiendelea katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.
Balozi wa China hapa nchini Mhe. Chen Mingjian akimkabidhi zawadi Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula katika Ofisi Ndogo za Wizara jijini Dar es Salaam.

“Naamini kuwa mimi ni kiungo cha kuimarisha na kuendeleza uhusiano baina ya China na Tanzania, tumekuwa tukishirikiana katia sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, biashara na uwekezaji, miradi ya mikopo nafuu na misaada, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), Uchukuzi, Utalii na utamaduni naahidi kuwa China itaendelea kushirikiana na Tanzania kwa maslahi mapana ya pande zote mbili,” amesema Balozi Mingjian.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news