Wanafunzi 37,731 wapangiwa mikopo ya Bilioni 99.9/- katika Awamu ya Kwanza

Lengo ni wanafunzi wapya 70,000 kwa mwaka 2021/2022,fedha zaanza kutumwa vyuoni, orodha ya pili wiki ijayo

NA MWANDISHI MAALUM

Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imetangaza leo (Jumapili, Oktoba 17, 2021) orodha ya Awamu ya Kwanza yenye wanafunzi 37,731 wa mwaka wa kwanza waliopangiwa mikopo yenye thamani ya TZS 99.9 bilioni kwa mwaka wa masomo 2021/2022 unaotarajiwa kuanzia wiki ijayo.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Bw. Abdul-Razaq Badru amesema kuwa kati ya wanafunzi hao (37,731), wanaume ni 23,379 sawa na asilimia 62 na wanawake ni 14,352 sawa na asilimia 38.

Badru ameongeza kuwa HESLB imeanza kupeleka fedha za wanafunzi waliopangiwa mikopo katika vyuo mbalimbali na kuwataka wanafunzi kupata taarifa za kina katika akaunti walizotumia kuomba mkopo maarufu kama SIPA (Student’s Individual Permanent Account) na kujiandaa kwenda vyuoni kwa ajili ya kujisajili.

“Serikali imeshatupatia fedha na tumeanza kuzipeleka vyuoni … lengo letu ni kuhakikisha wanafunzi wanaopangiwa wanazikuta fedha vyuoni ambako watajisajili na kupokea ili watimize ndoto zao,” amesema Badru.

Tarehe ya kutolewa orodha ya Awamu ya Pili

Kuhusu kutangazwa kwa orodha ya Awamu ya Pili, Badru amesema imepangwa kutolewa Alhamisi, Oktoba 21, 2021 baada ya kukamilisha uchambuzi wa maombi unaoendelea na kuwataka waombaji mikopo kutembelea akaunti zao ya SIPA kupata taarifa kuhusu maombi yao.

“Orodha hii ya kwanza inajumuisha wanafunzi wenye sifa zikiwemo kuwa wahitaji, wameomba kwa usahihi na wana udahili wa chuo kimoja … tunakamilisha uchambuzi wa maombi mengine na tutaoa orodha ya pili katika siku mbili zijazo, yaani Jumatamo, Oktoba 20, 2021,” amesema Badru.

TZS 570 Bilioni zimetengwa kwa mikopo ya elimu ya juu 2021/2022

Kwa mujibu wa Badru, Serikali imetenga TZS 570 bilioni kwa ajili ya mikopo ya jumla ya wanafunzi 160,000. Kati yao, wanafunzi 70,000 watakuwa ni wanufaika wapya na wanafunzi zaidi ya 90,000 ni wale wanaoendelea na masomo baada ya kufaulu mitihani yao ya mwaka.

Fedha zimeanza kutumwa vyuoni

Wakati huohuo, Badru amesema HESLB imeshapokea fedha kwa ajili ya malipo ya wanafunzi na taratibu za malipo zimeanza ili fedha hizo ziwe zimefika vyuoni kuanzia Jumanne, Oktoba 19, 2021.

Wito

Aidha, Bodi inapenda kuwasihi waombaji wa mikopo kuwa watulivu wakati mchakato wa upangaji wa mikopo kwa wanafunzi wenye sifa kwa awamu inayofuata ukiendelea.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news