Wizara ya Kilimo: Serikali haijazuia uuzaji mazao nje ya nchi

NA MWANDISHI MAALUM

SERIKALI imesema haijazuia mfanyabiashara yeyote kuuza mazao yake nje ya nchi, na kwamba mkulima wa nchi hii wajibu wake ni kulima, kuvuna,kuhifadhi na kuuza kwa kuwa hiyo ndio biashara yake.Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe akiangalia ubora wa mahindi katika moja ya maghala ya kuhifadhia mahindi katika kituo cha Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) Mpanda mkoani Katavi wakati alipokagua zoezi la ununuzi wa mahindi akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo kulia ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Bw. Milton Lupa na Katikati ni Marwa Range Kaimu Meneja wa NFRA Kanda ya Sumbawanga. (Picha na Wizara ya Kilimo).

Akizungumza katika ziara ya kikazi wilayani Mpanda mkoani Katavi baada ya kukagua kituo cha kununulia mahindi cha Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Naibu Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema, Serikali haijazuia uuzaji wa mazao nje ya nchi.

“Hivyo kama yupo ambaye amezuiwa kuuza mazao yake nje ya nchi, wizara inamkaribisha na itampa ushirikiano, kwani vibali vyote vya kusafirisha mazao nje ya nchi vinatolewa bure ili mradi awe na leseni ya kufanya biashara hiyo.”amesema.

“Serikali imeanza utaratibu wa kujenga na kukodi maghala katika nchi ambazo zina masoko ya mazao kama vile Sudan Kusini, DRC Congo, Kenya, tunaenda kuweka maghala katika nchi hizo ili Bodi yetu ya Mazao Mchanganyiko (CPB) na Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) waweke mazao hayo kwenye maghala hayo na kuyauza,”amesema.

Ameongeza kuwa, wataruhusu wafanyabiashara wa Tanzania waweze kuuza mahindi yao kupitia maghala hayo ili kurahisisha biashara yao. Kuhusu maombi ya Mkuu wa Mkoa wa Katavi, Mwanamvua Mrindoko aliyeomba kituo cha Mpanda kuongezwa tani zingine 10,000 kwa ajili ya wakulima kuuza mahindi yao amesema, kwa sasa wizara inapitia vituo vyote ili kujiridhisha na kujua mahitaji kamili ya vituo hivyo.
Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe akijadiliana jambo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Bw. Milton Lupa wakati alipotembelea katika kituo cha NFRA Mpanda mkoani Katavi na kukagua zoezi la ununuzi wa mahindi akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo, kulia ni na katikati ni Marwa Range ambaye ni Kaimu Meneja wa NFRA Kanda ya Sumbawanga na kulia ni Beatus Malema ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Maendeleo ya Mazao Wizara ya Kilimo. (Picha na Wizara ya Kilimo).

Amefafanua kuwa, wanafanya hivyo kwa sababu unaweza kuruhusu wanunue tani hizo kumbe mahindi yenyewe hayapo.

“Napita katika kila kituo kujiridhisha na tutafanya ukaguzi huo mpaka Oktoba 15, 2021 ili tukifanya maamuzi tujue kila mkoa utapata mgao wa kiasi gani tutakapowaruhusu kununua mahindi hayo kulingana na kiasi tutakachowaongezea.”ameongeza.

Bashe ameongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amejipambanua kuwalinda wakulima wa Tanzania na wanafahamu bei ya pembejeo imepanda katika soko la Dunia, hivyo njia pekee ya kumlinda mkulima ni kumpa ruzuku ya mbolea au kununua mahindi yake na hiyo ndiyo sababu Serikali inanunua mahindi ili kulinda wakulima wetu.

Ameongeza kuwa, mazao mengi ya wakulima yanaathiriwa na uhifadhi hii ni sehemu muhimu sana ndiyo maana serikali inajenga maghala mengi mpaka vijijini ili kuwasaidia wakulima namna ya kuhifadhi mazao kwa ubora lakini pia imekuwa ikitoa elimu sana kwa wakulima namna ya kuhifadhi mazao yao.

“Lakini Serikali inagawa mbegu za kisasa kupitia Taasisi ya Uzalishaji wa Mbegu Bora ya ASA kwa wakulima na imepunguza gharama za mifuko ya kuhifadhia mahindi inayozalishwa na A to Z na kupunguza hasara zinazotokana baada ya kuvuna mazao ambapo mkulima akiingiza mahindi katika mchakato wa kusafisha anapunguza kilo moja kwa kila kilo 100 kwa sababu mahindi yanakuwa na mchanga, magunzi pamoja na vumbi,”amesema.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news