Bandari ya Tanga yapokea meli iliyobeba Klinka tani 50,000 inayoelekea Rwanda

NA HADIJA BAGASHA

BANDARI ya Tanga imepokea meli kubwa iliyobeba shehena ya mzigo wa Klinka tani 50,000 malighafi itakayosafirishwa kuelekea nchini Rwanda katika kiwanda cha saruji cha Prime Cement Ltd.
Serikali ya Rwanda imeanza kuitumia Bandari ya Tanga kupitishia shehena ya mizigo yake ikiwa ni miezi miwili toka ziara ya Balozi wa nchi hiyo kutembelea Bandari ya Tanga na kuvutiwa na ufanyaji kazi wa bandari hiyo.

Meli hiyo yenye urefu wa mita zaidi ya 150 na kina cha mita 12 inayoitwa Star Fighter' Majuro yenye namba za usajili 9642198 kwa mujibu wa Wakala wa Kimataifa wa Bahari (IMO) imetia nanga siku ya Ijumaa iliyopita ikitokea nchini Saudi Arabia.

Katika kipindi cha mwezi Novemba katika bandari ya Tanga meli hiyo inakuwa ni ya pili kushusha shehena kubwa ya mzigo kutokea nchi za Mashariki ya Kati ambayo ilishusha shehena ya mzigo wa mafuta tani 30,000.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Adam Malima ameongoza viongozi wa Serikali, Mamlaka ya Bandari na waandishi wa habari kupokea meli hiyo na kusema kuwa ujio wa meli hiyo na shehena ya mzigo uliobeba si tu utaongeza mapato ya serikali kupitia kodi mbalimbali za bandari na TRA,pia itainua uchumi wa wajasiriamali wadogo wadogo haswa wanaotoa huduma za vyakula,malazi kutokana takribani malori 200 yanatarajiwa kuja kubeba mzigo huo,hivyo madereva watahitaji vyakula,maji na malazi.

Amesema kuwa, ujio wa shehena ya mizigo hiyo ni mafanikio ya uwekezaji mkubwa wa maboresho ya miundombinu katika Bandari ya Tanga ambao umeweza kufanywa na Serikali ya awamu ya Sita.

"Meli imekuja na neema,tutapata mapato ya serikali,wananchi watafanya biashara mbalimbali za vyakula,malazi na ujio huu ni juhudi za Serikali katika uwekezaji kwenye bandari hii ambapo zaidi ya shilingi bilioni 480 zimekwa katika upanuzi na ukarabati,"amesema.
"Pia nimewaomba Prime Cement Ltd kufanya mkutano na wamiliki wa magari makubwa ya mizigo ya Tanzania kuongea nao ili wabebe shehena hii badala ya kutumia magari yao tu ambayo ni machache na yatatumia muda mwingi kumaliza shehena hiyo,"ameongeza Mkuu huyo wa mkoa.

Pia amesema kuwa, baada ya kukamilisha hili la bandari ya Tanga kinachofuata sasa ni mradi mwingine mkubwa wa reli ili kuwawezesha wenye mzigo yao inapofika bandarini basi inakuwa rahisi kusafirisha kwa njia ya treni.

Kwa upande wake,Meneja wa Bandari ya Tanga,Donald Ngaile amasema kuwa ndani ya mwezi huu bandari hiyo tayari imeshahudumia tani 80,000 ya shehena za kichele (clinker) na kimiminika mbali na makontena.

Ngaile amesema kuwa, kutokana na maboresho yanayoendelea Bandari hiyo inatarajia kuongeza shehena ya mizigo kutoka tani laki 750 hadi Milioni 3 kwa mwaka.

Amesema kuwa, kuanza kutiririka kwa shehena ya mizigo ni mwanzo mzuri wa bandari hiyo kuanza kufungua na kuanza kufanya biashara kwa ufanisi kwa Bandari hiyo.

"Hii bandari ina miaka 130 kutokana na msukumo wa Serikali pamoja na mboresho yanayofanyika sasa tutaanza kupokea shehena kubwa ya mizigo katika Bandari yetu,"amesema Ngaile.

Meneja Uendeshaji Biashara wa Prime Cement Ltd, Mvayo Fabrice amesema kuwa, kampuni yake imeamua kutumia bandari hiyo kwa sababu kuu mbili ambazo ni kijografia kwani bandari hiyo ipo karibu sana kuhudumia moja kwa nchi za Afrika Mashariki na pia wameepuka msongamano wa meli katika nchi katika bandari ya Dar es Salaam.
DIRAMAKINI BLOG imeelezwa kuwa, kuja kwa meli hiyo katika bandari ya Tanga imeifanya kuwa na nguvu kubwa ya kuhudumia mizigo ya kimataifa ikiwemo mafuta,gesi,makontena na kemikali za viwandani.

Pia inatumika na meli za visiwa vya Unguja na Pemba kuja kuchukua bidhaa za biashara hasa za vyakula.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news