Mganga Mkuu wa Serikali atoa maagizo kwa wataalam wa afya

NA ATLEY KUNI-WAMJW

MGANGA Mkuu wa Serikali, Dkt. Wedson Sichalwe amesema, pamoja na kuendelea na mapambano dhidi Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19), Wataalam wa Afya nchini hawapaswi kuacha kuendelea na juhudi za kuwa na tahadhari na kufanya tafiti za magonjwa mengine ili kuweza kuwaepusha wananchi na magonjwa ya milipuko ikiwepo mafua makali ya virusi.
Akifungua mkutano wa mwaka wa ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko ikiwemo mafua makali na virusi vingine vinavyoathiri mfumo wa njia ya hewa, Dkt. Sichalwe, amewaambia wataalam hao wa afya kutoka kwenye vituo 15 vya kutolea huduma kuwa, kwa sasa magonjwa ya mlipuko hayapigi hodi, hivyo kila mara lazima wataalam wawe macho kusoma na kufanya tafiti mbalimbali zitakazo saidia kuzuia kabla hayajatokea.

“Tuna kila sababu ya kuendeleza ufuatiliaji wa magonjwa ya mfumo wa njia ya hewa kwakujenga uwezo wataalam wa nchi yetu kubaini aina ya virusi vilivyopo na pia endapo kitatokea kirusi kipya, lakini ugonjwa wa UVIKO- 19 hauondoi uwezekano wa kutokea mlipuko wa mafua inayotokana na kirusi kipya, Endapo mlipuko wa UVIKO-19 utapungua au kukoma kabisa itahitajika kuendelea na ufuatiliaji wa ugonjwa huo ( Post pandemic surveillance) kwani Mafua na UVIKO-19 vina dalili zinazoshabihiana hivyo ufuatiliaji magonjwa ni muhimu,”amesema Dkt. Sichalwe.

Dkt. Sichalwe, ametoa wito kwa viongozi kusimamia ufuatiliaji kwa kuwa karibu ili kuweza kuikinga jamii na majanga ya magonjwa yenye kusababisha mlipuko, huku akiwataka wataalamu waendelee kujengewa uwezo wa kufanya ufatiliaji wa magonjwa na usimamizi shirikishi ufanyike ili kujenga uwezo wa nchi yetu kubaini magonjwa ya mlipuko mapema na kudhibiti ili kupunguza madhara na vifo hapa nchini.
Dkt. Vida Mmbaga ambaye ni Mratibu wa Mkutano huo kutoka Wizara ya Afya, akielezea malengo ya mkutano muda mfupi kabla ya ufunguzi.

Awali akielezea malengo ya mkutano huo wa siku tatu, Dkt.Vida Mmbaga amesema, utawawezesha kupata mrejesho wa vipimo na tafiti zilizofanyika kipindi cha nyuma. 

“Kila kituo kitapata fursa ya kuelezea uzoefu wake kwa kipindi cha mwaka mzima na uzoefu uliopatikana sambamba na changamoto walizokumbana nazo. Aidha kikao hiki kitatumia fursa hiyo kipima ubora wa takwimu zinazopatikana maabara kwa vituo vyote kumi na vitano vinavyo shiriki mkutano huo,”amesema Dkt.Vida Mmbaga.
Mwakilishi kutoka kituo cha Ufuatiliaji Magonjwa cha Marekani ofisi ya Tanzania, Macelina Mponera, akizungumza wakati wa kikao hicho cha mwaka.

Naye Mwakilishi kutoka Kituo cha Ufuatiliaji Magonjwa cha Marekani ofisi ya Tanzania, Macelina Mponera, ameishukuru Serikali kwa kuendelea kushirikiana nao hata kufanikisha ujenzi wa maabaara ya taifa ya jamii.
Mkutano wa mwaka wa viongozi na watendaji wa ufuatiliaji wa ugonjwa wa mafua makali ya virusi na virusi vingine vinavyoathiri mfumo wa hewa unafanyika mkoani Morogoro kuanzia Novemba 22 hadi 24, 2021 na kuhudhuria na wataalam wa afya kutoka vituo 15.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news