Ngamilo:Teknolojia ya Nyuklia kuwa mkombozi katika kuhifadhi mazao, vyakula na kuboresha biashara za bidhaa za viwandani

NA MWANDISHI MAALUM

MKUU wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania, Bw. Peter Ngamilo amesema TAEC imeanza rasmi ujenzi wa mtambo maalumu ambao utatumia teknolojia ya nyuklia/mionzi katika kuhifadhi vyakula, mazao ili kuyaongezea muda wa matumizi na kuzikinga dhidi ya uharibifu unaoweza kusababishwa na vimelea vya vijidudu.
Ujenzi ukiendelea. (Picha zote na TAEC).
Ngamilo ameyasema hayo katika Tamasha la Mawasiliano, Utalii, Utamaduni na Maonesho ya Biashara yanayoendelea kwenye viwanja Malamala Igoma jijini Mwanza ambapo TAEC inashiriki ili kutoa elimu juu ya udhibiti wa mionzi na uhamaishaji wa matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia hapa nchini.

Ngamilo amesema kuwa, teknolojia ya nyuklia inayojumuisha mionzi ya gamma, Xrei na elektroni (e-beam) hunurisha bidhaa mbalimbali za mazao ya kilimo, viwandani na vifaa vya matibabu ili kuua vijudu viharibifu na kuimarisha ubora wa bidhaa.

"Teknolojia hii ina faida kubwa katika kuboresha huduma za afya, chakula, mazao na kuboresha mazingira, hivyo kuchangia ukuzaji wa uchumi wa nchi.

"Vilevile teknolojia hii pia itaweza pia kutumika kwenye bidhaa za usafi, matibabu, waya, semiconductors, vifaa vya polymeric na uponyaji au makovu ya nyuso, phytosanitary na kupunguza uchafuzi wa mazingira,"amesema.

Bw.Ngamilo amesema kuwa,Tanzania bado iko nyuma kulinganisha na baadhi ya nchi nyingine jirani kwa suala la kiasi na ubora wa bidhaa zinazozalishwa na kupelekwa nje.
"Uongezaji wa thamani na ubora wa utengenezaji bidhaa na mazao bado umejikita katika sekta chache na kuifanya Tanzania iwe katika hatari ya ushindani wa masoko ya kimataifa.

"Chakula na vinywaji pekee ndivyo vinavyochangia karibu nusu ya usindikajii ulioongezwa thamani (value addition), wakati bidhaa za kilimo zina uongezaji wa thamani mdogo, hivyo lipo hitaji la kubadilisha uchumi wetu kwa sekta zenye kulenga zenye uchumi mdogo ili zilenge kwenye uchumi mkubwa na kuongeza thamani ya bidhaa (value addition).

"Teknoljia ya nyuklia inao mchango katika lengo hili katika mazao ya kilimo na mengineyo.

"Soko la kuhifadhi mazao na chakula duniani linakua kwa kiwango cha ukuaji wa kila mwaka wa karibu asilimia 4.8 katika muongo mmoja ujao kufikia takribani Dola za Marekani Milioni 232.5 ifikapo 2025,"amesema Bw.Ngamilo.

Pia amebainisha kuwa, dhima kubwa ya kutumia teknolojia hii ni kuondoa changamoto za kuongezeka kwa magonjwa yanayosababishwa na vijidudu na uharibifu mkubwa wa mazao na bidhaa kabla ya kufikia mlaji ni moja ya vigezo ambavyo teknolojia hii inapewa nafasi katika kuchangia kutatua.

Bw. Ngamilo amesema, takwimu zinaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 30 ya vyakula duniani vinaharibika kila mwaka kwa sababu ya kuharibiwa na vijidudu au kuoza.

"Upotevu au kuharibika kwa chakula una athari kubwa katika kipato na maisha ya wakulima.

"Kwa mfano inakadiriwa kwamba kila mwaka hasara inayotokana na kuharibika kwa mazao ya nafaka barani Afrika hasa Kusini mwa Jangwa la Sahara inafikia dola za Kimarekani bilioni 4 na hii ni sawa na asilimia 15 ya thamani ya mavuno hayo, sambamba na matukio ya binadamu kuambukizwa vijidudu vya salmonella yanafikia hadi idadi ya watu wapatao 120,000 kila mwaka ambapo maambukizi haya ya bakteria yamekuwa yakisababisha vifo vingi,"amebainisha.

Bw.Ngamilo amesema kuwa,gharama za matibabu yanayosababishwa na madhara ya maambukizi haya ya vijidudu vya salmonella na Ecoli yamekuwa yakisababisha hasara ya dola za Kimarekani bilioni 6 kila mwaka.

Ikumbukwe kuwa, viwanda vya kusindika vyakula ni aslimia 34 ya viwanda vyote nchini hivyo kuchangia asilimia 50 ya ajira kwenye viwanda kwa mujibu wa CTI.

"Teknolojia hii itachangia suluhisho la kudumu kwenye sekta ya kilimo, mifugo na viwanda, kwani teknolojia hii ni salama na ya uhakika, hakuna athari zozote zitokanazo na teknolojia hii wala chembe chembe za mionzi zinazoweza kubakia kwenye vyakula wakati wa zoezi la mnyunyurisho (Irradiation),"amesema Bw.Ngamilo.

Malengo ya Mradi

Bw.Ngamilo anasema kuwa, malengo makuu ya mradi wa tekenolojia hii ya usindikaji kwa kutumia mionzi ni pamoja na:

i. Kuua vijidudu katika bidhaa na vifungashio vya vifaa vya matibabu.

ii. Kuuawa vijidudu katika bidhaa za vyakula, nyama, samaki, viungo, matunda ana mboga mboga ili ziwe salama kwa wananchi wetu na kukubalika katika masoko ya kimataifa.

"Chakula kilichopitishwa katika mnunurisho wa mionzi ni salama zaidi kushinda kilichopitishwa kwenye teknolojia nyingine ikiwemo kemikali,"amesema.

iii. Kuzuia mboga mboga , matunda, viungo visiive au kuota wakati bado havijafika kwa mlaji.

iv. Kuboresha bidhaa za viwandani hasa plastic za polymers ili ziwe ngumu na bora kama ambavyo sehemu nyingi za magari sasa hivi bodi zake zimeundwa na plastiki ngumu.

v. Kuongeza thamani ya vito kwa kubadilisha rangi hivyo kuvifanya viwe na soko ndani na nje ya nchi.

"Manufaa makubwa yatapatikana kwa kufanya kazi mara kwa mara na watu wengi wa kawaida, vikundi vya jamii na mashirika, kupata uelewa wao na kutolea ufafanusi wa hoja zao.

"Jambo lingine muhimu la kufanyia maamuzi katika hatua hii ni kwamba wateja wote na wadau wote watatakiwa kuwa na maoni yao yatazingatiwa katika uanzishaji na uendeshaji wa mtambo huu,"ameongeza Bw.Ngamilo.

Fursa za Biashara

Pia anasema, mradi huu una fursa ya kunufaisha uwekezaji na kuongeza thamani ya bidhaa zetu za viwandani na kupanua ubora wake kwa soko la ndani na nje.

"Mradi huu utatoa teknolojia mbadala wa uhifadhi wa mazao, mboga mboga, matunda na vyakula badala ya matumizi ya kemikali ambazo zina madhara,"anasema.

Bw. Ngamilo ameendelea kusema kuwa, matumizi ya teknolojia hii yatachangia katika kupunguza upotezaji wa mavuno baada ya kuvuna, kupunguza magonjwa yanayotokana na chakula kupata vijidudu na kushinda vizuizi vya karantini ya magonjwa ambayo inawekwa pale magonjwa yanapotokea.

"Teknolojia hii inaweza kufanikiwa kuchukua nafasi ya kuondoa vijidudu viharibifu katika kakao, kahawa na samaki waliokaushwa, tende, matunda yaliyokaushwa na kadhalika. Sekta ya dawa, kwa mfano, imekuwa ikihitaji njia ambayo vifaa vyenye viasilia kama proteni na enzymes kukaushwa bila kutumia joto au kemikali.

"Mionzi hutoa njia mbadala na kuua vijidudu kwenye bidhaa na vifaa vya madawa na gharama ya kutumia teknolojia hii inaweza kufanya bei kwa mtumiaji wa bidhaa kuwa chini,"amesema Bw. Ngamilo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news