Rais Dkt.Mwinyi atoa maelekezo namna ya kuzuia madhara yatokanayo na maaafa

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa, hatua za makusudi zinapaswa kuchukuliwa ili kuzuia na kupunguza madhara yatokanayo na maafa, ingawa ni vigumu kuzuilika moja kwa moja.
Wananchi waliohudhuria katika hafla ya Uzinduzi wa Nyumba za Vijiji za Wananchi walioathirika na mvua za masika mwaka 2017 wakisikiliza kwa makini hotuba iliyotolewa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt.Hussein Ali Mwinyi (hayupo pichani) katika sherehe zilizofanyika katika Kijiji cha Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja,ambapo ujenzi wake umefadhiliwa na Taasisi ya Mwezi Mwekundu kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu.(Picha na Ikulu).

Mheshimiwa Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo hivi karibu katika uzinduzi wa nyumba za maafa katika Kijiji cha Nungwi kilichopo Mkoa wa Kaskazini Unguja pamoja na zile zilizopo Tumbe Mkoa wa Kaskazini Pemba zilivyojengwa kwa ajili ya wananchi walioathiriwa na mvua za masika za mwaka 2017, ambapo hafla ya uzinduzi huo ilifanyika huko Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Katika maelezo yake, Rais Dkt. Mwinyi alisema kuwa miongoni mwa hatua zinazopaswa kuchukuliwa ni kuendeleza mipango miji, ambayo inabainisha sehemu za ujenzi wa makazi, sehemu za mabonde zisizopaswa kujengwa, maeneo ya kilimo, maeneo ya ujenzi wa miundombinu ya barabara na maeneo ya huduma za jamii.

“Ni vyema tukahakaikisha kwamba, tunakuwa na 'Master Plan' ya kila mji tunaoujenga ili kuweka mifumo na taratibu nzuri za kupambana na maafa,”alisema Rais Dkt. Mwinyi.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi alieleza kuwa ujenzi wa nyumba hizo umelenga kuimarisha maisha ya wananchi baada ya kupatwa na maafa.
Rais Dkt. Mwinyi alisema kuwa, maafa na majanga yamekuwa yakijitokeza katika nchi zote duniani kwa namna mbalimbali ambapo hakuna hata nchi moja iliyoweza kuwa na teknolojia ya kuzuia majanga na maafa yasitokee.

Alisema kuwa, hata nchi zilizoendelea hupata taharuki kubwa pale zinapokumbwa na maafa kama vile vimbunga, Sunami, matetemeko ya ardhi, mafuriko, moto na mengineyo.

Alisisitiza kwamba yanapotokea majanga na maafa ya aina hiyo, baadhi ya wakati hata nchi zilizoendela nazo huomba misaada, ili kuhami wananchi wake ambapo kwa lengo la kujikinga au kupunguza athari za maafa nchi nyingi duniani hivi sasa zimekuwa na mifumo ya utabiri na tahadhari dhidi ya maafa na kuanzisha taasisi na sheria za maafa.

Kwa upande wa Zanzibar, Dkt. Mwinyi alisema kuwa hatua zinaendelea kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na kuanzisha Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa kwa lengo la kupunguza athari za maafa kwa maisha ya watu na mali zao kwa kuchukua hatua madhubuti za kujikinga, kujitayarisha, kukabiliana na kurudisha hali ya kawaida ya maisha ya wananchi baada ya maafa kutokea.

Aliongeza kuwa Kikosi cha Zimamoto pamoja na Kikosi cha Uokozi Zanzibar vimepewa mafunzo maalum ya kukabiliana na kutoa misaada wakati wa maafa sambamba na kuwepo kwa mifumo ya utabiri wa hali ya hewa inayosimamiwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ambayo ni taasisi ya Muungano.

Pamoja na hayo, Rais Dkt. Mwinyi aliwahimiza wananchi waliobahatika kupewa nyumba hizo wazitunze vizuri, wadumishe usafi katika eneo lote hilo na waishi kwa kuzingatia misingi ya upendo, udugu na ujirani mwema.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt.Hussein Ali Mwinyi (katikati) akikabidhi cheti cha shukurani kwa Balozi wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) nchini Tanzania Mhe.Khalifa Abdulrahman ALMarzouqi (kushoto) na Naibu Katibu Mkuu wa Red Cresscent, Bw.Humud Al-Junaibi ambao wamefadhili mradi huo. (Picha na Ikulu).

Rais Dkt.Mwinyi alitoa shukurani kwa Ofisi ya Ubalozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu nchini Tanzania na kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Balozi Khalifa Abdulrahman Almarzouqi, Balozi wa (UAE) nchini pia, alitoa shukurani kwa Meneja wa Mradi huo kwa kazi nzuri aliyoifanya pamoja na kumpongeza Mshauri elekezi na Mkandarasi kwa kufanikisha mradi huo.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi aliwaeleza wananchi wa kijiji cha Nungwi azma ya Serikali anayoiongoza katika kuwaondoshea changamoto iliyopo na kuwapelekea huduma muhimu ya maji safi na salama pamoja na ujenzi wa barabara za ndani katika kijiji hicho.

Nae Kaimu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi, Saada Mkuya alisema kuwa jumla ya familia 54 ambazo zina idadi ya watu 291 kwa Unguja na Pemba wanaishi katika vijiji hivyo ambapo pia, wanafunzi wa Maandalizi na Msingi 277 wanasoma katika vijiji hivyo wakiwemo 151 Nungwi na 126 Tumbe.

Alisema kuwa kwa upande wa vituo vya afya tokea vifunguliwe tayari wananchi 954 wamepatiwa matibabu na huduma mbali mbali za kiafya wakiwemo 230 Tumbe na 724 Nungwi ambapo pia, kuna msikiti ambao unachukua waumini 200 ambao unahusisha sehemu ya kusalia kwa akina mama.

Waziri Mkuya alisema kuwa, wananchi waliopata nyumba hizo kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja wanatoka katika Shehia za Gamba, Mkwajuni Kidombo na Mkadini na kwa upande wa nyumba za Tumbe wanatoka katika Shehia ya Mtemani, Tumbe Mashariki, Tumbe Magharibi, Mtemani, Timba, Kipange na Shumba viamboni na Wingwi Mapofu na hakuna mtu aliyekuwa hausiki ambaye amepewa nyumba hizo.

Naibu Katibu Mkuu wa Mwezi Mwekundu alieleza jinsi taasisi hiyo ilivyofarajika katika kuunga mkono juhudi hizo za Serikali pamoja na kuwataja viongozi wakuu wa (UEA) ambao nao wameonesha kuunga mkono juhudi hizo.

Mapema Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera, Uratibu na Baraza la Wawakilishi Thabit Idarous Faina alisema kuwa ujenzi wa nyumba hizo unatokana na athari za mvua za masika zilizonyesha mwaka 2017 ambapo nyumba zipatazo 6005 ziliathirika Unguja na Pemba.

Alisema kwamba hali hiyo ndio ilipelekea taasisi ya Mwezi Mwekundu kutoka Falme za Kiarabu (UAE) kujitokeza kusaidia juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kunusuru maisha ya wananchi kwa kujenga makaazi bora na yalio salama ambapo jumla ya nyumba 15 zenye kuishi familia 30, kituo cha afya, skuli, maabara, msikiti na maduka 15 vyote vimejengwa katika vijiji vya Nungwi na Tumbe kisiwani Pemba.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news