RC Mahenge azitaka Kamati za Ujenzi wa Madarasa kuimarisha usimamizi

NA MWANDISHI MAALUM

MKUU wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge leo amefanya ziara ya kushtukiza katika shule sita za Sekondari katika Manispaa ya Singida Mjini zinazoendelea na ujenzi wa vyumba vya madarasa kupitia fedha za UVIKO 19 lengo likiwa ni kujionea hatua iliyofikiwa katika ujenzi huo na kusisitizia ukamilishwaji ndani ya wakati.
Akiwa katika ziara hiyo Dkt. Binilith Mahege akazitaka kamati za ujenzi wa shule kutumia muda wao mwingi katika usimamizi wa ujenzi huo ili kupata majengo yenye ubora unaokubalika na kukamilika kwa muda maalum.
Aidha Dkt. Mahenge akakemea vikali kitendo cha kamati za ujenzi wa shule kuwaachia kazi ya usimamizi wakuu wa shule ambapo inafahamika wazi kwamba wanamajukumu mengine ya kusimamia nidhamu na masomo kwa ujumla katika shule zao.
Hata hivyo RC akawataka walimu wakuu wanaosimamia ujenzi huo kuhakikisha kila jengo linakamilika katika kipindi kilichopangwa ambacho ni tarehe 1/12/2021, kwa kuwa kila shule imeonekana kuwa na vitendea kazi vya kutosha.

Dkt. Mahenge akatoa maelekezo kwa watendaji wa Mkoa, Wilaya na Halmashauri kuhakikisha kunakuwepo na wasimamizi kwa kila jengo linalojengwa mkoani hapa.
Aidha RC akamkumbusha Mkurugezi wa Manispaa ya Singida Mjini Zefrin Kimolo Lubuva kuwatumia wakuu wa Idara mbalimbali waweze kusimamia ujenzi na ikiwezekena kila Mkuu wa Idara apewe mradi wake alifafanua.

Amebainisha kwamba changamoto nyingi ambazo zimeonekana katika ujenzi unaoendelea katika Manispaa hiyo ni usimamizi mdogo ambao umeachwa kwa wakuu wa shule peke yao hivyo kila Mkuu wa Idara apatiwe shule ya kusimamia mpaka ujenzi ukamilike alibainisha Dkt. Mahenge.
Awali Mkuu wa Mkoa alitoa pongezi kwa wakuu wa shule kwa namna ambavyo waliweza kuendelea kusimamia ujenzi huo na kufikia hatua nzuri. 

Shule zilizotembelewa ni Chief Senge, Mandewa, Kindai Sekondari, Mitunduruni, Unyambwa na Mnyamikumbi kati ya hizo ni shule mbili ambazo zilikuwa zipo hatua ya msingi wakati nyinge zikiwa katika hatua ya linter na kuezeka.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhe.Pasikas Muragili akafafanua kwamba tayari wameshaunda timu maalumu ya ufuatiliaji ambayo tayari imeshaanza kazi ili kusaidia usimamizi wa kazi hiyo.

DC huyo amewakumbusha mafundi na wasimamizi wa majengo hayo kwamba siku saba zilizobaki zikitumiwa vizuri uwezekano wa kumaliza kazi hizo ni mkubwa endapo kila saa litatumika vizuri.

Amewataka wahandisi kuendelea kusimamia kazi hiyo kwa ufanisi mkubwa na kuhakikisha kunakuwepo na mawasiliano ya kila siku kati yao na Mkurugezi wa Halmashauri ili kuweza kutataua changamoto yeyote itakayoweza kujitokeza.

Naya Mkuu wa Shule ya Sekondari Unyambwa Bwana Charles Mtaturu amesema moja ya changamoto ambayo kwa kiasi kikubwa imekuwa ikitatiza ujenzi huo ni upatikaji wa vifaa vya kazi na mafundi kwa ajili ya ujenzi.

Bwana Mtaturu amebainisha kwamba viwanda vingi vilikuwa vimeshachukua Maagizo kwa watu mbalimbali na mafundi wengi wamewahiwa katika kazi nyingine kwa kwawa mainisapaa hiyo shule ujenzi wa mashule unafanyika kila mahali.

Yagi Maulidi Kiaratu ni Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida mjini akitoa shukrani kwa washiriki wa ziara hiyo amesema ujio wa Mkuu wa Mkoa wa kushtukiza kutaongeza chahu na uhamasishaji katika kukamilisha kazi hiyo.

Amesema, kwa upande wake atashirikiana na madiwani pamoja na chama Tawala CCM ambapo wataaza rasmi ziara kama hiyo kuanzia kesho tarehe 24/11/2021 kutembelea miradi yote ya ujenzi wa vyumba vya madarasa.

Aidha, amemalizia kwa kusema siku zilizobaki zinaweza kukamilisha shughuli zote za ujenzi endapo kila mdau atafanya kazi yake kwa kuzingatia muda na mikakati iliyowekwa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news