Timu za Bunge zakomba makombe mashindano ya 11 ya mabunge EAC



NA MWANDISHI DIRAMAKINI

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ameipongeza timu ya Bunge baada ya kuibuka na makombe saba katika michezo mbalimbali kwenye Mashindano ya 11 ya Mabunge ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yaliyomalizika hivi karibuni jijini Arusha.
Ameyasema hayo wakati akizungumza baada ya kuzipokea timu mbalimbali za Bunge zilipowasili katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma zikitokea jijini Arusha ilipofanyika michuano hiyo na hatimaye kuibuka na ushindi ulioliletea Bunge hilo heshima pamoja na nchi kwa ujumla.

Majaliwa amesema, wamefanya kazi kubwa na nzuri,"mmepambana na hatimaye mmeleta zawadi kwa Rais Samia Suluhu Hassan,Bunge,Watanzania na nchi kwa ujumla,”amesema Waziri Mkuu Majaliwa.

Timu ya Bunge la Tanzania imeshinda makombe kwenye michezo ya mpira wa miguu, pete, wavu kwa wanawake na wanaume, kikapu kwa wanawake na wanaume na mchezo wa kuvuta kamba wanaume.

“Ninaleta kwenu salamu za faraja kutoka kwa Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa mliyoifanya, na faraja nyingine ni kuona wachezaji wengi mmerudi salama, nidhamu mlioinesha katika mashindano haya imetujengea heshima kubwa,”amesema.
Amesema kuwa, ushindi wa timu hiyo unapeleka ujumbe kwenye timu nyingine zinazoshiriki mashindano mbalimbali ya kimataifa kushiriki kikamilifu na kuiwakilisha vyema nchi kwenye mashindano husika ikiwemo kuwa na matamanio ya kurudi na makombe.

“Tunatakiwa tuandike historia ya ubora wa michezo nchini ambapo tunaona kwasasa kila sekta inaenda vizuri na hata ile inayokuwa inakufa tunaifufua na hii pia imepelekea kupata heshima na sifa ya kupeleka timu yetu ya watu wenye ulemavu kwenye mashindano ya kombe la dunia,”amesema.

Kwa upande wake, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Mheshimiwa Job Ndugai amesema,kupitia michezo hiyo wametoa somo kwa timu nyingine zilizoshiriki michezo hiyo na hatimaye kulipa heshima bunge.

“Ahadi yetu sisi tutasimama na ninyi kwenye maandalizi zaidi mwakani na ninawapongeza sana kwa nidhamu mlioionesha hata mlipochokozwa hamkuchokozeka,”amesema.

Naye Meneja wa timu, Seif Gulamali amemshukuru Spika Ndugai kwa kuiwezesha timu hiyo kufanya vizuri kwenye mashindano hayo jambo lililowezesha kuibua morali na hatimaye kuibuka na makombe.

“Kwa niaba ya wabunge wote tunaomba usituchoke sisi ni vijana wako, endelea kutulea, tunapoleta maombi yetu basi uyapokee kwa mikono miwili,"amesema.

Gulamali amemuomba Spika Ndugai kuongeza wachezaji wengi ikibidi hata zaidi ya 100 ili wafanye vizuri zaidi katika michuano ya mwaka ujao.

“Mheshimiwa Spika tumepata ushindi huu lakini timu imeenda na wachezaji wachache ambao wamekuwa wakishiriki mchezo zaidi ya mmoja,lakini pamoja na uchovu lakini bado tumepata ushindi,tunaomba tuongezee wachezji ili tufanye vizuri zaidi,"amesema Gulamali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news