Waziri Makamba auelekeza uongozi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kuongeza nguvu katika aina nyingine za nishati

NA VERONICA SIMBA-REA

WAZIRI wa Nishati, January Makamba amewaelekeza viongozi na wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kuongeza nguvu katika aina nyingine za nishati kama inavyofanyika kwenye umeme.
Waziri wa Nishati, January Makamba (kulia) akipokea Taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Wakala hiyo, Mhandisi Hassan Saidy. Waziri alizungumza na Wafanyakazi wa REA, Desemba 20, 2021 jijini Dodoma. Kulia kwa Waziri ni Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Wakili Julius Kalolo na wa kwanza kushoto ni Mjumbe wa Bodi, Mhandisi Styden Rwebangira.

Alisema kuwa REA imeendelea kutekeleza kwa ufanisi mkubwa usambazaji nishati ya umeme vijijini hivyo ni vyema pia ikifanya hivyo katika aina nyingine za nishati zenye matumizi makubwa zaidi, hususan zinazotumika katika kupikia.

Waziri Makamba alikuwa akizungumza na wafanyakazi wa REA ili kutoa dira na mwelekeo wa Wizara ya Nishati, ikiwa ni mara ya kwanza kukutana nao rasmi tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo, takribani siku 100 zilizopita. Alizungumza na wafanyakazi hao jijini Dodoma, Desemba 20 mwaka huu.
Waziri wa Nishati, January Makamba akizungumza na wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini – REA (hawapo pichani),kilichofanyika jijini Dodoma.

Alisema kuwa wengi wanaitafsiri REA kuhusika na nishati ya umeme pekee kutokana na kuweka nguvu nyingi kwenye nishati hiyo, hivyo akasema ni muhimu kwa Wakala hiyo kuzipa uzito unaostahili nishati nyinginezo ambazo ni jukumu lake pia.
Waziri wa Nishati, January Makamba (kushoto) akiongozwa na viongozi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) alipowasili Makao Makuu ya Wakala jijini Dodoma, kuzungumza na wafanyakazi, Desemba 20, 2021. Kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo, Mkurugenzi Mkuu wa REA Mhandisi Hassan Saidy na Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi, REA Mhandisi Jones Olotu.

“Kazi ya REA ni kubwa zaidi, siyo umeme tu. Mnafanya kazi nzuri sana kwa upande wa umeme hivyo toeni uzito unaostahili kwa nishati nyingine zenye matumizi makubwa.”

Akitoa mfano, Waziri Makamba alieleza kuwa tafiti mbalimbali zinaonesha kuwa kwa Tanzania, matumizi makubwa ya nishati yako majumbani. Aidha, aliongeza kuwa nishati inayotumika zaidi majumbani hususan katika kupikia ni tungamotaka.
Wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakimsikiliza Waziri wa Nishati, January Makamba (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza nao,kilichofanyika Desemba 20, 2021 jijini Dodoma.

Alisema, asilimia kubwa ya Watanzania wanaishi vijijini na wanatumia nishati ya tungamotaka katika kupikia. “Nataka mfanye mabadiliko kwenye nishati ya kupikia maana ndiyo inagusa Watanzania wengi zaidi,” alisisitiza Waziri.

Akifafanua, alieleza kuwa pamoja na kupeleka umeme vijijini, haitegemewi kuwa wakazi wake watatumia nishati hiyo kupikia hivyo ni jukumu la Wakala kufanyia kazi suala hilo.
Waziri wa Nishati, January Makamba (katikati), akisaini Kitabu cha Wageni, alipowasili Makao Makuu ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) jijini Dodoma, kuzungumza na wafanyakazi.

Sambamba na agizo hilo, Waziri Makamba aliitaka REA kuimarisha Kitengo chake cha Utafiti na kianze mara moja kufanya tafiti mbalimbali zitakazoleta mapinduzi makubwa katika sekta ya nishati, hususan vijijini.

“Mathalani, kuna mawazo au fikra gani mpya kuwasaidia Watanzania wapate nishati safi ya kupikia? Je, nishati ya kupikia ina mchango gani katika kuongeza au kupunguza gharama za maisha? Hizi ni baadhi ya tafiti zinazopaswa kufanyika,” alisisitiza Waziri.
Mwenyekiti wa Chama Cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE), Tawi la Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Swalehe Kibwana (kushoto) akimkabidhi Waziri wa Nishati, January Makamba, Risala aliyoisoma kwa niaba ya wafanyakazi. Waziri alizungumza na wafanyakazi wa REA, Desemba 20, 2021 jijini Dodoma.

Katika hatua nyingine, Kiongozi huyo mwenye dhamana na sekta ya nishati nchini, alitoa maagizo kuwa wakandarasi wanaotekeleza miradi ya umeme vijijini, wanapobainika kufanya udanganyifu kwenye miradi hiyo, wachukuliwe hatua kali ikiwemo kuondolewa kabisa na wasipewe tena fursa ya kufanya kazi hizo.

Vilevile, washitakiwe kwa Mamlaka zote husika pamoja na kufanya ufuatiliaji ili wasipewe kazi nyingine katika eneo lolote ili iwe fundisho kwao kwa kuwaumiza wananchi na kuliingizia hasara Taifa.
Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba akizungumza wakati wa kikao cha Waziri wa Nishati, January Makamba na wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), kilichofanyika Desemba 20, 2021 jijini Dodoma.

Pamoja na maelekezo hayo, Waziri aliipongeza REA kwa kazi nzuri ambayo imekuwa ikifanya na kuitaka kuongeza juhudi zaidi katika kuwatumikia Watanzania.

Alisema kuwa Serikali inajivunia utendaji kazi wa REA na kwamba ni mojawapo ya Taasisi zinazotegemewa sana hivyo akaiasa isiharibu sifa hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy (kulia) akimwongoza Waziri wa Nishati, January Makamba (kushoto) alipowasili Makao Makuu ya REA, Mtaa wa Makole jijini Dodoma, kuzungumza na wafanyakazi, Desemba 20, 2021. Pamoja nao ni Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Wakili Julius Kalolo.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy akizungumza wakati wa kikao cha Waziri wa Nishati, January Makamba na wafanyakazi wa Wakala hiyo,kilichofanyika jijini Dodoma.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu kwa Waziri, alieleza kuwa kazi kubwa imefanyika ambapo hadi sasa upatikanaji umeme vijijini umefikia asilimia 69.6.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini, Wakili Julius Kalolo, akizungumza kwa niaba ya Bodi, alimuhakikishia Waziri kuwa maelekezo yote aliyoyatoa yatafanyiwa kazi.
Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo akizungumza wakati wa kikao cha Waziri wa Nishati, January Makamba na wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA),kilichofanyika jijini Dodoma.

Waziri aliahidi kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili wafanyakazi wa REA ikiwemo upandishwaji madaraja na kukaimu nafasi mbalimbali kwa muda mrefu, kama alivyowasilisha Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi, Tawi la REA, Swalehe Kibwana.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news