Rhobi Samwelly aijengea uwezo Jumuiya ya Wanawake (UWT) mkoani Mara

NA FRESHA KINASA

MJUMBE wa Baraza Kuu la Wanawake Tanzania (UWT) Taifa Mkoa wa Mara, Rhobi Samwelly ametoa msaada wa mizinga ya nyuki mitano kwa Jumuiya ya Wanawake (UWT) Wilaya ya Musoma Vijijini kwa lengo la kuunga mkono juhudi za jumuiya hiyo kuiwezesha kufuga nyuki, baada ya kuibua mradi huo ambao utakuwa na tija kwao.
Mjumbe wa Baraza kuu la UWT Taifa Mkoa wa Mara, Rhobi Samwelly akikabidhi kiti kwa Katibu wa UWT Mkoa wa Mara,Sarah Kairanya kama ishara ya samani mbalimbali ikiwemo viti, meza, runinga na kabati alivyokabidhi kwa UWT Mkoa wa Mara vikiwa na thamani ya zaidi ya shilingi mililioni tatu.(Picha na Fresha Kinasa).

Pia, Rhobi amekabidhi samani mbalimbali za ofisi ya UWT Mkoa wa Mara zenye thamani ya shilingi milioni 3.3 ikiwemo viti vya kukalia 13 vya ofisi, meza mbili, kabati moja na runinga.
Amekabidhi mizinga hiyo na samahi hizo za ofisi leo Februari 18, 2022 mara baada ya kumalizika kwa kikao cha kawaida cha Baraza la UWT Mkoa wa Mara ambapo amesema jumuiya ina wajibu wa kubuni miradi ili kumudu kujiendesha pamoja na kujikwamua kiuchumi.

Kwa upande Wake Katibu wa UWT Mkoa wa Mara, Sarah Kairanya wakati akipokea vifaa hivyo mbele ya wajumbe wa UWT Taifa Mkoa wa Mara amepongeza hatua ya Rhobi ya kutoa samani kwa ajili ya Ofisi ya UWT Mkoa wa Mara, kwani itawezesha kutekeleza majukumu kwa ufanisi mkubwa.
Naye Katibu wa UWT Wilaya ya Musoma Vijijini, Ester Juma pamoja na Mwenyekiti, Abia Masaule wakizungumza kwa nyakati tofauti baada ya kupokea mizinga ya nyuki, wamesema watahakikisha wanaendelea kufuga nyuki kwa ajili ya kupata asali ambayo baada ya kuuzwa fedha hizo zitatumika kwa shughuli mbalimbali katika ofisi yao.

Katika kikao cha Baraza la UWT kilichofanyika, Rhobi ameahidi kuendeleza kushirikiana na wanawake wote wa Mkoa wa Mara katika kuunga mkono juhudi za maendeleo kwa kutafuta fursa za maendeleo ambazo zitakuwa na manufaa yao na Taifa kwa ujumla.
Amewahimiza wajumbe wa UWT katika maeneo yao kushiriki kikamilifu mapambano ya ukatili wa kijinsia na amesisitiza mkazo ufanywe na kila mmoja kuhakikisha watoto wa kike wanasoma na kufikia ndoto zao ili waje kuwa msaada katika jamii na Taifa pia.

"Tuendelee kushiriki vyema katika mapambano ya ukatili wa kijinsia, tuhimize watoto wa kike wasome kwa bidii na tuwasaidie kuwaondolea changamoto ambazo ni kikwazo kwao. Mimi naahidi kuendelea kushirikiana na jumuiya kutafuta namna ya kuwainua watoto wa kike kadri Mungu atakavyojalia,"amesema Rhobi.

Aidha, Rhobi ametumia fursa ya kikao cha baraza hilo, kuwaaga wanawake wa jumuiya hiyo kuwa anatarajia kuondoka nchini kuelekea nchini Ufarasa ambapo atakaa huko kwa kipindi cha miezi sita, kutokana na mwaliko wa uongozi wa nchi hiyo kumpa mwaliko wa kwenda kupokea tuzo maalum kutokana na juhudi zake za kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia anazozifanya kupitia Shirika la Hope for Girls and Women in Tanzania ( HGWT) analoliongoza.
Awali Mwenyekiti wa UWT Mkoa wa Mara, Wegesa Hassan amewataka wajumbe wa Baraza la UWT Mkoa wa Mara kuachana na tabia ya kusemana wao kwa wao badala yake washikamane na kuthaminiana sambamba na kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya chama hicho mwaka huu.

"Wanaweke wa UWT Mara nawasihi sana tuachane na majungu ya kusemana semana sisi kwa sisi. Mfano ukimsema mtu kwa mwingine kusudi tu upate shilingi 50,000. Pesa hiyo itakusaidia Nini? Tutangulizeni mbele upendo, utu, umoja miongoni mwetu na pia tukisemee chama kwa wananchi kwa kuendelea kutekeleza ilani ya uchaguzi kwa ufanisi mkubwa,"amesema Wegesa.
Aidha, Wegesa amesema kuwa jumuiya hiyo Mkoa wa Mara, itahakikisha inashiriki vyema kuwezesha ushindi wa kishindo wa Rais Samia Hassan katika uchaguzi Mkuu ujao kusudi aendelee kuwaletea maendeleo Watanzania katika nyanja mbalimbali kama anavyofanya sasa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news