Serikali yatoa maagizo kwa NEMC

NA MWANDISHI DIRAMAKINI

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Selemani Jafo ametoa siku 45 kwa Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kukamilisha Mfumo wa Kielektroniki wa Vibali vya Taka hatarishi.
Dkt. Jafo ametoa rai hiyo mara baada ya kuzindua Bodi ya Nane ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira katika Ukumbi wa St. Gaspar jijini Dodoma

Amesema, Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira ni chombo muhimu kinachoishauri Serikali katika masuala muhimu ya Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira.

Dkt. Jafo ameitaka Bodi hiyo, kusimamia utekelezaji wa Sera ya Mazingira ya Mwaka 2021, Sheria, Kanuni na Miongozo mbalimbali ya Serikali na kuagiza kupitia upya muundo na majukumu ya Baraza ili kuimarisha utendaji wake na kutatua changamoto zilizopo katika suala zima la uhifadhi na usimamizi wa mazingira na kutoa ushauri ipasavyo.

“Mkasimamie mapato na matumizi ya fedha, simamieni Baraza kwa niaba ya Ofisi ya Makamu wa Rais ili miongozo inayotolewa na Ofisi hii iweze kutekelezwa kwa weledi,” amesema Jafo alisisitiza.

Amesema, suala la mazingira ni mtambuka hivyo ni wajibu wa Bodi hiyo kuhakikisha Baraza linashirikiana na Taasisi za Serikali, Sekta binafsi na Taasisi zisizo za Kiserikali katika kusimamia hifadhi ya mazingira.

“Wengi wenu ni wabobezi katika masuala ya mazingira hivyo nina imani mtatumia taaluma na uzoefu wenu kuushauri uongozi wa Baraza katika kutekeleza majukumu yake,” alisisitiza Dkt. Jafo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais, Bi. Mary Maganga amempongeza Mwenyekiti Prof. Esnati Chaggu na wajumbe wa Bodi hiyo kwa kuchaguliwa kuongoza Taasisi hiyo yenye jukumu kubwa la kusimamia masuala ya mazingira nchini.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wajumbe wa Bodi, Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC, Profesa Mhandisi Chaggu amesema wana dhamana kubwa katika kuhakikisha ajenda ya mazingira inapewa msukumo wa dhati kwa kuwa ni mjadala wa Dunia kwa sasa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news