MASHINDANO YA KIPANGA CUP YAHITIMISHWA WILAYANI MAFIA

*Timu ya Big Time yaibuka kidedea, yatoka na zawadi ya bajaji

NA MWANDISHI MAALUM

MASHINDANO ya mpira wa miguu ya Kipanga Cup yamefikia tamati Machi 27, 2022 kwa timu ya Big Time, kuibuka mshindi wa goli moja kwa sifuri dhidi ya timu ya Stone Fire .
Fainali ya mashindano hayo yamefanyika katika uwanja wa Dawendege uliopo wilayani Mafia mkoani Pwani ambapo goli la ushindi lilifungwa na mchezaji namba 10, Said Said katika dakika ya 32 ya kipindi cha kwanza cha mtanange huo.

Katika fainali hiyo mshindi wa pili, timu ya Stone Fire iliangukia nafasi hiyo baada ya kukosa mkwaju wa penati katika dakika ya pili ya kipindi cha kwanza cha mchezo huo.
Katika michuano hiyo iliyoandaliwa na Mbunge wa Jimbo la Mafia, Mhe. Omari Kipanga (Mb) na kudhaminiwa na Benki ya CRDB, mshindi wa kwanza alipata zawadi ya bajaji.

Mshindi wa pili alipata zawadi ya pikipiki moja, mshindi watatu alipewa Sh. 500,000, jezi na mpira na mshindi wa nne Sh. 200,000 jezi na mpira mmoja.
Akizungumza baada ya kumalizika kwa mtanange huo, Mhe. Kipanga aliwashukuru vijana wa Wilaya hiyo kushiriki michuano hiyo iliyokuwa na lengo la kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutimiza mwaka mmoja pamoja na kuibua vipaji.
Amewataka mshindi wa kwanza na wa pili kutumia zawadi walizopewa kama kitega uchumi cha kuwaingizia kipato ili kujiimarisha kushiriki mashindano mengine ya kimkoa na kitaifa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news