Rais Samia afanya mambo makubwa Shinyanga Mjini, CCM yatoa neno

NA KADAMA MALUNDE

HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Shinyanga Mjini imemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi katika Manispaa ya Shinyanga ambazo zinaendelea kutatua kero za muda mrefu za wananchi katika sekta za afya, elimu,maji,umeme na barabara.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza kwenye Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini kilichofanyika Aprili 11,2022.(Picha na Malunde 1 blog).

Akizungumza wakati akiwasilisha Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM mwaka 2021/2022 kwenye Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini kilichofanyika Aprili 11,2022, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko amesema Manispaa ya Shinyanga inazidi kupiga hatua kimaendeleo kutokana na fedha nyingi zilizotolewa na Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.
"Tunamshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi Manispaa ya Shinyanga ambazo zinaendelea kutatua kero za muda mrefu mfano Hospitali ya Mkoa wa Shinyanga kuletewa fedha za majengo mapya ili hospitali ya Rufaa ihamie Mwawaza kwenye majengo yake ifikapo mwezi Julai mwaka huu.Upatikanaji wa dawa ni asilimia 97,"amesema Mboneko.

"Tunamshukuru Mhe. Rais Samia kupitia fedha alizoleta na miradi kutekelezwa kwa njia ya force account wananchi, mafundi, wafanyabiashara wamenufaika lakini pia tunaendelea kuwashukuru wananchi wa Manispaa ya Shinyanga kwa kuendelea kuchangia na kushiriki shughuli za maendeleo. Tunawaomba wananchi wanapokuwa na kero waziwasilishe Serikalini zitafutiwe ufumbuzi,"ameongeza Mboneko.
"Fedha zilizoletwa upande wa afya kwa upande wa magonjwa ya dharula ni shilingi bilioni 1.99, Emergency Department milioni 650, ICU shilingi milioni 560, Kituo cha afya Ihapa shilingi milioni 500, Zahanati tatu shilingi milioni 150 (Masekelo,Seseko, Mwamashele), Dawa kutoka MSD shilingi milioni 235.44.

"SHUWASA shilingi bilioni 1.91, RUWASA shilingi milioni 149.96, TANESCO shilingi bilioni 1.6, TARURA shilingi bilioni 1.4, Sekondari ya Lubaga shilingi milioni 470, Sekondari ya Wasichana sh. Bilioni 3, Madarasa 35 ya sekondari 700, madarasa tisa shule shikizi milioni 180 na Jengo la utawala la Manispaa ya Shinyanga ghorofa mbili sh. Bilioni 1. Jumla ya fedha zote ni Shilingi bilioni 14.46,"amefafanua Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga.

Aidha, Mboneko amesema Fedha za Makusanyo/Mapato ya ndani ya Manispaa ya Shinyanga zilizotolewa ikiwa ni sehemu ya mapato ya ndani 40% kwa ajili ya shughuli za maendeleo Manispaa ya Shinyanga zinaendelea kuchochea shughuli za maendeleo ikiwemo umaliziaji majengo ya zahanati, shughuli za lishe, Mikopo ya 10%, ukamilishaji na ujenzi wa vyoo, ununuzi wa taa za Solar Stendi ya Mabasi Ibinzamata, Stendi ya Mjini, Soko Kuu na Soko la mbao Chamaguha na uchongaji wa viti, meza na madawati shule zote za msingi na sekondari.
Mkuu huyo wa Wilaya amewasihi watumishi wa serikali ngazi zote kutoa majibu mazuri kwa wananchi au wateja wao na wale wanaotoa majibu mabovu kwa wananchi majina yao yafikishwe kwake ili hatua za kinidhamu zichukuliwe haraka.

Katika hatua nyingine Mboneko amesema tayari Mhe. Rais Samia ametolea ufafanuzi ukarabati wa Uwanja wa ndege Ibadakuli hivyo zinasubiriwa fedha ziingizwe TANROADS ili ujenzi uanze.
"Kampeni ya upandaji miti inaendelea na tunaendelea kuwahimiza wananchi kila kaya kupanda miti kuanzia mitano ya matunda na vivuli na inapatikana bila gharama katika Manispaa ya Shinyanga.

"Pia tunawashukuru waandishi wa habari wote kwa kuendelea kutoa habari za matukio mbalimbali, shughuli za maendeleo na kuibua kero za wananchi katika Manispaa ya Shinyanga na wilaya kwa ujumla,"ameongeza Mboneko.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini Mhe. Abubakar Mukadam amewataka viongozi wa CCM kuanzia ngazi za matawi kuyasemea mambo mazuri yanayoendelea kufanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan badala ya kunyamaza.

“Katika kipindi cha Mwaka mmoja wa Uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan tumeshuhudia mambo makubwa yakifanyika hivyo ni vyema tujitokeze kuyasemea mazuri haya tunayoyaona. Tutumie muda mwingi kueleza mazuri yanayofanywa na Serikali. Na mjitahidi kutatua kero za wananchi badala ya kusubiri kusema kwenye vikao vya chama,”amesema Mukadam.

Kuelekea kipindi cha uchaguzi ndani ya CCM, Mwenyekiti huyo wa CCM wilaya ya Shinyanga Mjini ametumia fursa hiyo kuwaonya wanachama wa CCM kuepuka kuchafuana na kuhakikisha wanavunja makundi na kuwa kitu kimoja kwani kuendekeza majungu na kuchonganisha viongozi wa chama kunaweza kuharibu chama hicho.
“Tunapoenda kwenye uchaguzi naomba twende kwa utulivu,tusitengeneze misingi ya kuchafuana na kuchonganisha viongozi kwa viongozi. Kama mtu flani haumkubali msemee basi kwa mema yake. Kama Mungu amekupangia kuwa kiongozi basi utakuwa Kiongozi, Tusiviziane na kuchafuana kisa huyu hakuniunga mkono,”amesema Mukadam.

“Makundi na majungu yaliyopo yaondoeni kwa maslahi ya chama. Usimwingilie kiongozi kwenye nafasi yake kwa kuingilia majukumu yake,mnawavunja mioyo viongozi wa chama. Acheni haki na wajibu kwa wanachama na viongozi. Kamwe tusikubali kutengeneza chuki miongoni mwetu, naomba twende kwa kuzingatia Katiba na Kanuni zilizopo,”ameeleza.
Katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Agnes Bashemu akizungumza kwenye Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini kilichofanyika Aprili 11,2022.

Naye Katibu wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Agnes Bashemu amesema viongozi wa CCM na Serikali wataendelea kushirikiana katika kuwaletea maendeleo wananchi huku akisisitiza umuhimu wa kila mmoja kutimiza wajibu wake.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Jomaary Satura akizungumza kwenye Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini kilichofanyika Aprili 11,2022.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Jomaary Satura ameahidi Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kuendelea kurekebisha na kutatua changamoto zinazojitokeza katika sekta mbalimbali ikiwemo ya afya ambayo baadhi ya watumishi wa afya wamelalamikiwa kutumia lugha chafu wanapotoa huduma kwa wananchi ambapo amesema ni vyema wakafanya kazi kwa upendo mkubwa na maadili

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news