Serikali inaboresha miundombinu ya barabara,elimu na afya Msomera-Waziri Bashungwa

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mhe. Innocent Bashungwa amesema Serikali imetenga na kupeleka shilingi milioni 503.4 kufanya matengenezo ya barabara Kwenjugo-Mbagwi-Msomera yenye kilomita 32.6.

Ni barabara kuu kutoka makao makuu ya Wilaya ya Handeni hadi eneo la Msomera wanapohamia wakazi kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ili barabara ziweze kupitika wakati wote bila shida.
Pia, Serikali imetenga shilingi Milioni 716 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za mizunguko ndani ya eneo la Msomera yenye kilomita 50 ambapo zitafunguliwa barabara mpya, matengenezo, kujengwa vivuko na kalavati ili kurahisha huduma ya kuingia na kutoka kwa wananchi inayoenda sambamba na utengenezaji wa barabara inayounganisha Kijiji cha Msomera na Wilaya ya Korogwe yenye urefu wa kilomita 22.8

Ameeleza hayo Juni 22, 2022 katika mjadala maalum wa kujadili maendeleo ya zoezi la uhamaji wa hiari kwa wakazi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro kuhamia eneo la Msomera uliofanyika kwa njia ya mtandao wa Zoom na kueleza kuwa, Serikali imetenga fedha nyingine katika bajeti 2022/23 shilingi bilioni 2.53 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara Wilaya ya Handeni.

Mjadala huo umeratibiwa na Watch Tanzania kwa udhamini wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania na Airtel Tanzania.

Mada kuu iliangazia juu ya Zoezi la Uwekaji Alama za Mipaka Tarafa ya Loliondo na Maendeleo ya Zoezi la Uhamaji wa Hiari kwa Wakazi wa Ngorongoro.

Bashungwa amesema, tayari ujenzi wa shule ya msingi mpya umekamilika na shule ya sekondari mpya ambayo vyumba saba vya madarasa vimekamilika, ujenzi wa bweni unaendelea kwa ajili ya wanafunzi wenye uhitaji wa kukaa shuleni, ujenzi vyoo vipya vya kutosha na ofisi za walimu na mahabara kwa ajili ya wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi.

Aidha, ameeleza inakadiriwa jumla ya wanafunzi 765 watahamia eneo la Msomera ambapo wanafunzi 415 wa awali na msingi na wanafunzi 350 wa sekondari, hivyo idadi ya wanafunzi hao itakuwa sambamba na kupeleka walimu katika shule hizo.

Vile vile, Bashungwa amesema tayari Serikali imetoa shilingi milioni 500 kuanza ujenzi wa kituo cha afya kipya na shilingi Milioni 50 kwa ajili ya kupanua na kuboresha huduma za afya katika zahanati ya Kijiji cha Msomera na kujenga jengo la wazazi, kuongeza watumishi na wataalam wapya katika sekta ya afya.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news