Watakaosababisha matumizi mabaya ya ruzuku inayotolewa na TASAF kuwajibishwa

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla amesema hatua kali za kinidhamu zitachukuliwa dhidi ya mtumishi yeyote atakayesababisha matumizi mabaya ya fedha za ruzuku zinazotolewa kwa kaya maskini kupitia Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini nchini, anaripoti James K. Mwanamyoto (OR-Utumishi) Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na ujumbe kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora leo ofisini kwake wakati ujumbe huo ulioongozwa na Mhe. Mchengerwa ulipoenda kujitambulisha na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa baadhi ya majukumu ya taasisi zake. Wa kwanza kulia kwake ni Mhe. Mchengerwa na anayefuatia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Bw. Ladislaus Mwamanga.

Mhe. Makamu wa Pili wa Rais ameyasema hayo leo ofisini kwake alipotembelewa na ujumbe kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ulioongozwa na Waziri mwenye dhamana ya ofisi hiyo, Mhe. Mohamed Mchengerwa.

Mhe. Abdulla amesema Serikali itahakikisha fedha zinazotolewa kwa ajili ya kuzinusuru kaya maskini Zanzibar, zinatumika kwa malengo yalikusudiwa ili kuboresha maisha ya kaya hizo.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akitoa neno la utangulizi kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla wakati Waziri Mchengerwa alipoenda kujitambulisha na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya baadhi ya majukumu ya taasisi zake.

“Ni lazima tuwe na nidhamu ya kutumia vema rasilimali za umma ikiwemo fedha zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuziwezesha kaya maskini.” Mhe. Abdulla amesisitiza.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema ofisi yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar inayoratibu masuala ya TASAF itahakikisha inasimamia vema matumizi mazuri ya fedha za ruzuku zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya kuzinusuru kaya maskini.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amewataka Waratibu wote wa TASAF wa Tanzania Bara na Zanzibar kushirikiana katika kutoa elimu kwa walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini ili kuwawezesha kutumia ruzuku wanayoipata kuboresha maisha yao.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Bi. Riziki Abraham akiwamukilisha Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Bw. Xavier Daudi kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Sekretarieti hiyo kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla leo ofisini kwa Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Wa kwanza kulia kwake ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Omar Mchengerwa na wa kwanza kushoto kwake ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Bw. Faina Idarus.

Akiwa katika ukaguzi wa utekelezaji wa miradi ya TASAF ya Kituo cha Afya cha Kianga na shule ya Sekondari ya Fujoni, Mhe. Mchengerwa amewataka watumishi wa kituo hicho cha afya na wananchi wanaofuata huduma kukitunza kituo hicho ili kiendelee kutoa huduma bora na kuondoa adha ya upatikanaji wa huduma za afya ambazo zilikuwa zikiwakabili kabla ya ujenzi wa kituo hicho.

Akizungumzia ujenzi wa jengo la shule ya Sekondari Fujoni, Mhe. Mchengerwa amesema, jengo hilo litatatua changamoto ya kutokuwepo kwa chumba cha kufanyia mitihani kwa wanafunzi wa shule hiyo ambayo kwa muda mrefu walikuwa wakifanyia mitihani yao chini ya miti na kupata adha kubwa kipindi cha mvua.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), Bw. Ladislaus Mwamanga akitoa maelezo ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa chumba cha kufanyia mitihani kilichopo katika Shehia ya Fujoni wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa ya kukagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na TASAF, Zanzibar.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akizungumza na wananchi wa Fujoni wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na TASAF, Zanzibar.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akipokea taarifa ya utekelezaji ya Kituo cha Afya cha Kianga kutoka kwa Mkuu wa Kituo hicho, Dkt. Islam Seif Salum alipokuwa akikagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na TASAF, Zanzibar.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Ladislaus Mwamanga aliwashukuru wananchi wa Fujoni kwa jitihada zao katika kukamilisha ujenzi wa chumba cha kufanyia mitihani.

Bw. Mwamanga amemueleza Mhe. Waziri kuwa mradi huo umetekelezwa kwa kasi kubwa sana katika kipindi kisichozidi miezi sita tofauti na maeneo mengine ambayo hutumia mwaka mmoja na kuongeza kuwa utekelezaji huo unatokana na ushiriki mzuri wa wananchi ambao walikuwa na hamu kubwa kuhakikisha wanafunzi wanapata eneo zuri la kufanyia mitihani.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news