UNFPA kuyawezesha mashirika kupambana na ukatili, Rhobi Samwelly anena

NA FRESHA KINASA

JUMLA ya Simu janja 210 zenye thamani ya Shilingi milioni 21 zimetolewa na Shirika la Kimataifa la UNFPA kwa Shirika la Hope for Girls and Women Tanzania na AFGM Masanga la wilayani Tarime kwa lengo la kusaidia mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia mkoani Mara.

Simu hizo zitakuwa na App Maalum ambazo zitatumiwa na Wanawake watakaopewa Simu hizo bure kueleza madhara ya Ukatili wa Kijinsia Kutoka kwenye maeneo yao. Ambapo baada ya fomu hiyo kujazwa ndani ya simu hiyo ikieleza madhara ya Ukatili, mahala alipo na aina ya Ukatili aliofanyiwa, itatumwa moja kwa moja kwenye APP ya Shirika la Hope for Girls and Women Tanzania na hivyo ufuatiliaji utafanyika.

Akizungumzia hatua hiyo leo Juni 16, 2021 Mkurugenzi wa Shirika la Hope for Girls and Women Tanzania, Rhobi Samwelly amesema kuwa, shirika lake limepokea simu 59 kati ya simu 210 kutoka UNFPA ambapo Juni 17 hadi Juni 18, 2021 watatoa mafunzo kwa wanawake wa Wilaya ya Butiama na kuwapa simu hizo bure ukiwa ni mkakati wa kuwafanya washiriki kufichua taarifa za vitendo vya kikatili katika maeneo yao wakati wowote.

"Kina mama 59 watapewa mafunzo ya siku mbili kutumia simu janja kutoa taarifa ya kesi za ukatili wa kijinisia katika maeneo yao. Kuna APP watazitumia kutoa taarifa na pia kuna App ya kuongeza maeneo katika ramani na kuangalia maeneo gani hatarishi katika masuala ya ukatili wa kijinsia. Hatua hii itasaidia kufahamu aina ya ukatili kutoka eneo husika ili kuongeza nguvu zaidi sisi shirika katika kuchukua hatua,"amesema Rhobi.

Rhobi ameongeza kuwa, mafunzo hayo yalikwishatolewa pia kwa wanawake 87 kutoka Wilaya ya Serengeti pamoja na kuwagawia simu janja bure 2019 ili kuongeza idadi ya watumiaji wa simu janja hasa kina mama katika kuripoti habari za ukatili wa kijinsia bila kuzifumbia macho.

Aidha, Rhobi ameishauri jamii kushiriki kupinga vitendo vya kikatili ambavyo ni kinyume cha haki za binadamu, huku akisisitiza usawa wa kijinsia uzingatiwe kwa masilahi endelevu ya Taifa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news