SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limewashauri wafanyabiasha na wenye viwanda kushiriki katika mafunzo yanayotolewa na shirika hilo mara kwa mara ili kupata uelewa zaidi kuhusu masuala yanayohusu viwango vya Kitaifa na Kimataifa.
Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo TBS, Bi.Prisca Kisella ameyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Amesema, mafunzo ni muhimu kwani yanasaidia wadau kufikia vigezo vya viwango,taratibu za udhibiti ubora wa bidhaa na mifumo, pamoja na kukidhi matakwa ya kanuni na sheria zinazohusiana na kumpunguzia mteja urasimu pindi anapokuwa anahitaji huduma za TBS.
“Mafunzo haya yanajikita zaidi katika kutoa uelewa kwenye maeneo mbalimbali yakiwemo,viwango na matumizi ya viwango vya Tanzania (National Standards) katika uzalishaji wa bidhaa na huduma mbalimbali,matumizi ya viwango vya Kimataifa katika mifumo ya usimamizi wa kimenejimenti (ISO standards),taratibu za kuthibitisha ubora wa bidhaa,taratibu za kuthibitisha mifumo ya usimamizi ya kimenejimenti katika maeneo ya uzalishaji na huduma,taratibu za kupeleka bidhaa nje (Technical Asssistance for export – TAE) pamoja na taratibu za kuingiza bidhaa nchini hususani kwenye kukidhi matakwa ya viwango na ubora,"amesema Bi.Prisca.
Bi.Prisca amesema,katika mafunzo hayo pia wanatoa mafunzo ya mifumo ya usimamizi wa kimenejimenti (ISO
Training) ikiwemo ISO 9001 – mfumo wa usimamizi wa ubora wa kimenejiment (Quality Management System),ISO 21001 – Mfumo wa usimamizi wa kimenejimenti katika sekta za elimu (Education Quality Management System),ISO 14001 – Mfumo wa kimenejimenti ya usimamizi wa kulinda mazingira (Environmnental Management System),ISO 45001 – Mfumo wa usimamizi wa afya na usalama mahali pa kazi – (Occupational Health and Safety Management System),ISO 22000 – Mfumo wa kimenejimenti wa usimamizi usalama wa chakula (Food Safety Management System).
Amesema, mafunzo hayo yanasaidia kutoa ulewa wa jumla juu ya kiwango husika (Awareness training) hii inafanyika kwa muda wa siku moja hadi mbili kulingana na kundi husika.
