Waziri Mkuu ahimiza matumizi sahihi na salama ya mtandao, azindua Wiki ya Vijana Kitaifa

NA MWANDISHI MAALUM

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa amewahimiza vijana nchini kuchangamkia fursa zilizomo kwenye Sekta ya Mawasiliano kwa kuzingatia matumizi bora ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipita kwenye Mtambo wa Usimamizi wa Masafa wa TCRA.

Akizungumza katika Uzinduzi wa Wiki ya Vijana Kitaifa kwenye Viwanja vya Mazaina wilayani Chato mkoani Geita, Mhesihimiwa Waziri Mkuu amewakata vijana kutumia vizuri mifumo ya TEHAMA kwa ajili ya kuboresha maisha na kuleta maendeleo ya nchi kwa kuongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu alianza kwa kutembelea shughuli mbalimbali kwenye mabanda ya maonesho, ambapo aliipongeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa kazi nzuri.

“Asanteni sana TCRA hatunashida nanyi mnafanyakazi sana,”amesema Mheshimiwa Waziri Mkuu ambapo pia alizindua Jumuiya ya Wakimbiza Mwenge wa Uhuru na aliahidi vijana nchini kwamba Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea na juhudi zake za kusaidia makundi ya vijana wajasiriamali.

Amesema Vijana wanamchango mkubwa kwamaendeleo ya Taifa. “Kutokana na umuhimu huo Serikali imeamua kusisitiza matumizi sahihi na salama ya TEHAMA kwenu vijana, kwani ninyi ndio watumiaji wakubwa na wahanga wakubwa wa TEHAMA,"amesema.

Aliongeza kwamba, ni kweli usiopingika kuwa matumizi sahihi ya TEHAMA ni nyenzo muhimu kwa maendeleo endelevu ya kiuchumi, kiutamaduni na kijamii yanayoongeza fursa za ajira kwa Watanzania hasa vijana.

Mhe. Majaliwa amesema, vijana wengi wamefanikiwa kutokana na matumizi sahihi ya TEHAMA hususan kwa kufanya biashara kwa njia ya mtandao, vijana wameweza kuanzisha na kuendesha vituo vya huduma za intaneti na pia kuanzisha wakala wa huduma za kifedha kupitia mitandao ya simu.

Wiki ya Vijana Kitaifa ilianzishwa rasmi na Serikali mwaka 2000 na huratibiwa na wizara yenye dhamana na Maendeleo ya Vijana nchini, kwa lengo la kuwapa nafasi vijana na wadau wa shughuli za maendeleo ya vijana kukutana ili kubadilishana uzoefu na kujifunza mambo mbalimbali yanayowahusu kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni. Lakini pia, wiki hii ya vijana hutumika kuwawezesha vijana kutafakari falsafa, maono pamoja na kazi za Baba wa Taifa alizozifanya kwa uzalendo mkubwa kwa nchi yetu.

Kaulimbiu inayoongoza maadhimisho ya Wiki ya Vijana kwa mwaka 2021 ni:-“TEHAMA ni Msingi wa Taifa endelevu; itumie kwa usahihi na uwajibikaji. Kaulimbiu hii imejikita katika kuhimiza matumizi sahihi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA). Kaulimbiu hii inalingana na kaulimbiu ya Mbio Maalum za Mwenge wa Uhuru za mwaka huu, 2021 ambayo pia inahimiza matumizi sahihi ya TEHAMA.

Waziri Mkuu amesema, vijana ndiyo watumiaji wakubwa wa TEHAMA, "niwakumbushe kujiepusha na matumizi yasiyo sahihi kama vile wizi na utapeli wa fedha unaofanywa kwa njia ya mtandao, kujiunga na makundi yasiyofaa, kujiingiza kwenye majukwaa ya uchochezi baina ya mtu na mtu, baina ya watu na viongozi wao, lakini pia Taifa na Taifa. Vitendo hivi vinavuruga amani, utulivu na mshikamano wetu kama Taifa,"amesema.
Wananchi wakipata Elimu kwenye banda la TCRA.

Aidha, amewasihi vijana kujiepusha na vitendo vibaya vya udhalilishaji, vitisho na hata dhuluma za faragha kwa kutumia mtandao ya kijamii. Ameonya kwamba matumizi hasi ya TEHAMA huathiri mfumo mzima wa malezi na makuzi ya vijana na kusababisha kuporomoka kwa maadili ya Mtanzania, mila, silka, desturi na tamaduni zetu na kupandikiza tamaduni za kigeni katika jamii yetu.

Umuhimu wa Wiki ya Vijana unatokana na ukweli kwamba vijana ni kundi kubwa na nguzo muhimu sana kwa maendeleo ya Taifa letu. Kwa mujibu wa taarifa ya makisio ya watu (Population Projection Report 2013-2035), kati ya kipindi cha mwaka 2013-2035 idadi ya watu nchini Tanzania itaongezeka hadi kufikia watu milioni 89.2 na hii inaashiria kuwa idadi ya vijana pia itaongezeka hadi kufikia milioni 20.7 sawa na asilimia 35% ya watu wote nchini.

Vijana ni kundi lenye uwezo wa kufanya kazi kwa muda mrefu, kundi lenye ubunifu, uthubutu, ujuzi na uwezo wa kufanya kazi zaidi ya moja. Kwa misingi hiyo, vijana ni injini kwa maendeleo ya Taifa na kwamba Taifa lisilokuwa na vijana ni sawa na gari lisilokuwa na magurudumu kwa kuwa haliwezi kwenda mbele.

Maadhimisho na maonesho haya ya Wiki ya Vijana yanalenga kuwakumbusha na kuiwezesha jamii na Taifa kwa ujumla kutambua mchango mkubwa wa vijana katika maendeleo ya nchi na kuwapa fursa nyingi vijana kumuenzi na kumkumbuka Baba wa Taifa Mwl. Julius Kambarage Nyerere ambaye alitoa mchango mkubwa katika kulikomboa Taifa letu akiwa kijana. Hivyo, vijana wote nchini ni lazima watambue kuwa Taifa letu linawategemea sana katika kudumisha amani,uzalendo, umoja, mshikamano wa Kitaifa, uchapaji kazi na usimamizi thabiti wa rasilimali za Taifa kwa maendeleo ya Taifa.

TEHAMA imewezesha shughuli nyingi kurahisishwa katika upatikanaji wake. Huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi kama vile huduma za kibenki, ulipaji wa bili za maji na nishati ya umeme kwa njia ya mtandao, ulipaji wa kodi na mapato ya Serikali, urahisashaji wa upatikanaji wa huduma za afya na tiba, elimu, huduma za ugani, masoko, taarifa za hali ya hewa na upatikanaji wa taarifa mbalimbali na kupunguza gharama za usafiri kutoka eneo moja kwenda lingine kwa ajili ya kupata huduma.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news