Kada wa CCM aliyefariki hivi karibuni azikwa Chalinze

NA MWANDISHI MAALUM

VIONGOZI, wanachama, watumishi wa CCM, wapenzi, wakereketwa wa CCM na wananchi mbalimbali, Januari 3, 2022 wamehudhuria maziko ya aliyekuwa mwanachama, mtumishi, kiongozi na kada mahiri wa CCM Mzee Steven Rehema Kazidi kijijini kwao Vigwaza, Chalinze mkoani Pwani.

Kada huyo alifariki Januari 1, 2022 katika Hospitali ya Mloganzila alipokuwa akipatiwa matibabu.
Waombolezaji wakiuswalia mwili wa Marehemu Steven Rehema Kazidi kabla ya maziko yaliyofanyika Chalinze mkoani Pwani.

Pamoja na viongozi wengine maziko hayo pia yamehudhuriwa na Rais mstaafu wa Awamu ya Nne,Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Akitoa salaam za rambirambi za Chama Cha Mapinduzi kwa niaba ya Katibu Mkuu wa CCM, Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Shaka H. Shaka amesema,Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Samia Suluhu Hassan amemuelezea marehemu Kazidi kuwa wakati wa uhai wake alikuwa mwanachama, kada, kiongozi na mtumishi wa CCM mahiri, mbunifu, aliyekuwa na moyo wa kujitoa na kujitolea muda wote, vipawa na nguvu zake kukijenga na kuitumikia CCM na wananchi kwa uamininifu na utiifu mkubwa.
Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Jakaya Kikwete akizungumza na Katibu Mwenezi wa CCM Taifa,Shaka Hamdu Shaka walipokutana katika msiba wa Kada wa CCM marehemu Mzee Steven Kazidi ambaye amezikwa Chalinze mkoani Pwani.

”Mzee Kazidi alikuwa na sifa ya unyenyekevu na ulezi kwa vijana katika uongozi. Hivyo CCM, tumempoteza mwanachama, kada mahiri, mlezi na mwalimu wa siasa na uongozi kwa vijana,"amesisitiza Shaka.
Rais mstaafu, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiweka udongo kwenye kaburi la marehemu Steven Kazidi wakati wa mazishi yake yaliyofanyika Chalinze.
Mbunge wa Jimbo la Chalinze, Ridhiwani Kikwete akitoa salaam zake kwa waombolezaji wakati aliposhiriki shughuli za mazishi hayo.

Wakati wa uhai wake Mzee Stephen Rehema Kazidi alitumikia nafasi mbalimbali kwa nyakati tofauti ikiwemo Mwenyekiti wa kijiji cha Vigwaza, Diwani wa Kata ya Vigwaza, Mwenyekiti wa Halimashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, Katibu wa Siasa na Uenezi Wilaya ya Bagamoyo, Katibu wa CCM Wilaya, Ukatibu wa CCM Mkoa na Katibu Msaidizi Mkuu Idara ya Oganaizesheni CCM Taifa.
Katibu Mwenezi wa CCM Taifa,Shaka Hamdu Shaka akitoa Salam za chama wakati wa mazishi ya Kada wa CCM Marehemu Steven Kazidi ambaye amezikwa Leo Chalinze mkoani Pwani.

Viongozi wengine mbalimbali wa chama na serikali walishiriki ni Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Pwani, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo na Kilosa watumishi wa CCM toka Makao Makuu Ofisi ndogo Lumumba, Mkoa wa Pwani na Morogoro.

Sote ni wa MwenyeziMungu na kwake tutarejea.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news