WAZIRI MKENDA:VYUO,TAASISI BORESHENI UFUNDISHAJI ILI KUPATA WAHITIMU MAHIRI

NA MWANDISHI WyEST

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Adolf Mkenda (Mb) amevitaka vyuo na taasisi za mafunzo kuona namna ya kuboresha ufundishaji ili vijana wa Kitanzania wawe mahiri kwenye fani wanazosomea.
Ameyasema hayo Juni 13, 2022 jijini Dodoma wakati wa kilele cha maonesho ya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi (TVET) na kuongeza kuwa ni muhimu taasisi na wadau wakashirikiana katika utoaji wa mafunzo hayo.
Amewataka waajiri na wadau wote nchini kuwa karibu na vyuo vya mafunzo ikiwa ni pamoja na kuvijengea uwezo ili viandae wahitimu wanaohitajika katika soko la ajira.
"Changamoto moja kubwa wanayopata wenye vyuo na wanafunzi ni sehemu za kujifunzia kwa vitendo kwani baadhi ya waajiri wamekuwa wakikataa kuwapokea vijana hawa. Kumbukeni kuwa hawa ndio waajiriwa wenu wa kesho hivyo mnao wajibu wa kuwapatia nafasi za mafunzo kwa vitendo," amefafanua Waziri Mkenda.

Aidha, Mhe. Mkenda amesema ni muhimu sana kwa mitaala inayotumika kufundishia ikalenga kutatua changamoto zilizopo kwenye jamii ya Watanzania.
"Wito wangu kwa wamiliki wa vyuo nchini ni kuhakikisha kuwa wanatoa elimu bora na sio bora elimu. Pia NACTVET kuhakikisha vyuo vyote vinazingatia taratibu za uendeshaji na utoaji mafunzo," amefafanua Prof. Mkenda.

Naye Naibu Waziri, Mhe. Omari Kipanga (Mb) amesema awali Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi kabla haijaungana na Mamlaka ya Ufundi Stadi lilikuwa na vyuo zaidi ya 400, lilipoungana na kuunda NACTVET limekuwa na vyuo zaidi ya 1,200 inavyoviratibu.
"Kwa hiyo matumaini makubwa ya Watanzania yapo NACTVET hivyo tuhakikishe tunaratibu na kusimamia vizuri. Tukio la leo linatutengenezea picha au ramani ya wapi tunapotaka kwenda," amesema Mhe. Kipanga.

Kwa upande wake mwakilishi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii, Salome Makamba (Mb) amesema wanatambua kwamba Elimu ya kati ndiyo inayochangia sana katika ajira kwenye viwanda, maofisi na maeneo mengine mbalimbali.
"Sisi kama wabunge tutaendelea kuwa pamoja nanyi katika juhudi hizi, tunaomba muendelee kupeleka maonesho haya ya ubunifu katika ngazi ya Wilaya na Mikoa ili viwanda, wabunifu na vyuo vya kati waje washindane hapa Dodoma kutoka pande zote za nchi," amesema Mhe. Makamba.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news