DODOMA-Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Ajira na Mahusiano imetangaza nafasi 1,000 za ajira kwa Watanzania watakaofanya kazi ya upishi nchini Oman.
Kwa mujibu wa tangazo hilo la Aprili 17, 2026, nafasi hizo zinapatikana katika Mahakama ya Kifalme (Royal Court) nchini humo, zikiwalenga wanaume wenye umri kati ya miaka 21 hadi 45.
Waombaji wanatakiwa kuwa na elimu ya cheti au stashahada ya upishi, uzoefu wa angalau miaka miwili, pamoja na uwezo wa kuzungumza Kiingereza, huku wanaojua Kiarabu wakipewa kipaumbele.
Aidha, mshahara uliotajwa ni Sh milioni 3.5 kwa mwezi, huku mwajiri akigharamia huduma za matibabu, visa, tiketi za ndege, malazi na chakula kwa kipindi chote cha ajira.
Mkataba wa ajira ni wa miaka miwili unaoweza kuhuishwa, na mwisho wa kupokea maombi ni Aprili 21, 2026.
Waombaji wanatakiwa kutuma wasifu binafsi (CV) kupitia anuani iliyotolewa pamoja na kujisajili katika mfumo wa ajira wa serikali.

