Zaidi ya watu 15 wamefariki na wengine 18 kujeruhiwa katika ajali ya basi iliyohusisha basi la abiria la Emirates kutoka Ngara kwenda Bukoba mkoani Kagera, anaripoti Mwandishi Diramakini.
Ajali hiyo iliyotokea leo Oktoba 24,2020 katika eneo la Kumuyange ilihusisha basi hilo lenye namba za usajili T670 DKL baada ya kuanguka na majeruhi wamelazwa hospitali Teule ya Nyamiaga wilayani
Ngara.
Mkuu wa wilaya Ngara, Michael Mntenjele amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema “Ni kweli ajali hiyo imetokea mbele kidogo kutoka hapa Ngara mjini, eneo la tukio kuna mteremko mkali, huenda gari lilimshinda breki, kwa hiyo akawa amepata ajali na kuanguka upande wa mteremko. Majeruhi wanaendelea na matibabu ingawa hali zao si nzuri sana kutokana na ajali yenyewe ilivyokuwa mbaya sana ambapo kipande cha juu cha gari chote kimeondoka,”amesema Mkuu huyo.
Wakati huo huo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli
amepokea kwa masikitiko taarifa ya vifo vya watu 15 vilivyosababishwa na
ajali ya barabarani baada ya basi la abiria kupinduka katika mteremko
wa Kumnyange uliopo katika Wilaya ya Ngara mkoani Kagera.
Ajali hiyo ambayo imetokea leo Oktoba Oktoba 24, 2020 pia imesababisha watu 18 kujeruhiwa. Kutokana na ajali hiyo, Rais Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Kagera,
Brigedidia Jenerali Marco Gaguti na amemtaka kufikisha salamu za pole kwa familia
za Marehemu, ndugu, jamaa na wote walioguswa na vifo hivyo, na
amewaombea Marehemu wote wapumzike mahali pema peponi na majeruhi wote
wapone haraka na kuungana na familia zao.
“Nimesikitishwa na vifo vya Watanzania wenzetu waliopoteza maisha katika
ajali hii, nawapa pole wafiwa wote na nawaomba wawe na moyo wa
uvumilivu na ustahimilivu katika kipindi kigumu cha majozi,”amesema Rais Magufuli.
Aidha,Rais Magufuli amewakumbusha watumiaji wa barabara hasa
madereva wa magari kuzingatia sheria zote za usalama barabarani ili
kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.
Pia amevitaka vyombo vinavyosimamia usalama barabarani kuchukua hatua
dhidi ya watumiaji barabara wanaokiuka sheria za barabarani.
Tags
Habari







