WATAFITI MUCE WAGUNDUA DAWA YA KUZUIA SUMU KUVU

Watafiti kutoka Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE) cha mjini Iringa wamegundua dawa ya kuzuia sumu kuvu kwenye mazao ya nafaka inayotokana na mitishamba ugunduzi unaotajwa kuleta suluhisho katika uhifadhi wa mazao hayo,
anaripoti Fredy Mgunda.
Mkuu wa Idara ya Kemia, Dkt. Juma Mongoyo kushoto akitoa maelezo kwa Mkurugenzi wa NIMR, Profesa Yunus Mgaya ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa maonesho ya sita ya utafiti katika Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE).

Akizungumza katika maonesho ya sita ya utafiti, Dkt.Juma Mongoyo ambaye ni mkuu wa idara wa kemia katika chuo hicho aliseama, walifanya utafiti kupitia mmea aina ya Diospyros Mafiensis ambao uligunduliwa Mafia ambapo walitumia mizizi yake katika utafiti na kuleta matokeo chanya ya utafiti huo.

Mongoyo amesema kuwa, katika tafiti za mmea huo wamebaini kuwa mizizi yake hufanya kazi ya kupunguza uzalishaji wa sumu kuvu na kulinda nafaka isishambuliwe na fangasi aina ya Asperigillus flavus na Asperigillus parasiticus wanaozalisha sumu kuvu kutokana na joto kali na unyevunyevu unaotengeneza fangasi hao.

Dkt.Mongoyo amesema kuwa, takwimu zinaonesha kuwa takribani ya watu million 4.5 duniani wanakula sumu kuvu kwa kiwango tofautitofauti ambapo huchukua miaka 30 hadi kujitokeza madhara yake huku akisema kuwa takwimu huonyesha takribani watu laki moja na elfu hamsini na tano hupoteza maisha kila mwaka duniani kote  kutokana na tatizo la saratani ya maini inayosababishwa na ulaji wa sumu kuvu.
Mtafiti Princess Ngowi kushoto akitoa maelezo kwa Mkurugenzi wa NIMR, Profesa Yunus Mgaya ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa maonesho ya sita ya utafiti katika Chuo Kikuu kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE).

Amesema kuwa, mizizi ya mmea huo wa diospyros mafiensis unauwezo wa kulinda nafaka na jamii yote inayoweza kushambuliwa na fangasi hao wajulikanao kama Asperigillus flavus na Asperigillus parasiticus

 Akizungumza mgeni rasmi katika uzinduzi huo ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Magonjjwa ya Binadaamu (NIMR), Prof.Yunus Mgaya alisema kuwa taasisi ya NIMR imeona ipo haja ya kushirikiana na chuo hicho cha Mkwawa kutokana na tafiti hizo wanazozifanya zina lengo moja na taasisi ya NIMR ya kulinda afya ya binadamu.

Amesema kuwa, tafiti iliyofanyika na Chuo Kikuu Kishiriki cha Dar es salaam Mkwawa kuhusiana na mmea unaotumika katika tiba asili ambayo wakatengeneza dawa yenye kemikali inayozuia  fangasi isizalishe sumu ambayo ikiingia kwenye mahindi yanayotumiwa na binadamu husababisha saratani ya ini hivyo utafiti huo unaweza ukakinga jamii dhidi ya magonjwa yatokanayo na sumu kuvu.

Aidha, Profesa Yunus Mgaya ameongeza kuwa, katika kuboresha tiba nchini taasisi ya NIMR inajenga kiwanda cha kuzalisha dawa za asili zitokanazo na mimea ambazo zitakuwa kwa mfumo wa vidonge na unga tofuti na sasa hivi ambapo dawa nyingi za asili ni za maji.

Naye Dkt.Evaristo Haulle kutoka chuo cha Mkwawa amesema kuwa, ushirikiano wa taasisi zote za utafiti na za elimu ya juu kuwa na ushirikiano na asasi nyingine ni muhimu hivyo wamepokea kwa mikono miwili ushirikiano kati ya Mkwawa na NIMR.

Maonesho hayo ya utafiti yanajumuisha wanafunzi na walimu watafiti kutoka chuo kikuu hicho kishiriki cha elimu ikiwa ni maandalizi ya kwenda kushiriki maonesho ya wiki ya utafiti ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam yanayobeba kauli mbiu isemayo “utafiti na uvumbuzi endelevu kwa maendeleo ya viwanda”.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news